KIFO CHA MTU ASIYE NA HATIA - 07

Alisimama wima mbele ya askari magereza wa kike, mtoto wake Alicia akiwa mgongoni, mtoto huyo hakuelewa kitu chochote kilichoendelea aliendelea kulala mgongoni kwa mamaye. Baada ya kujieleza kwa muda mrefu akimbembeleza askari magereza amwitie Prosper ili aonane naye kabla ya kifo chake hatimaye askari alilainika na kuanza kutembea kuondoka eneo hilo na kuingia ndani ya gereza.
Hakurudi mpaka dakika kama kumi na tano hivi baadaye,
askari huyo aliporejea mbele yake akiwepo Prosper! Tayari alishavalishwa nguo
za wafungwa na alionekana kukonda sana.
Prosper
alionekana kutoyaamini macho yake alipomwona Belinda! Alitaka kukimbia kwenda
upande wa pili kumkumbatia lakini alizuiliwa na nondo nzito zilizotenganisha
ndani na nje ya gereza! Ziliwekwa maalum kuwazuia wafungwa kutoroka.
“Afande nifungulie basi nisalimiane na mke wangu kwa karibu zaidi!”
“Haiwezekani hata kidogo Prosper kwanza si ruhusa leo wafungwa kuonwa nimewafanyia upendeleo vinginevyo ningeweza kukataa kwanza haraka kabla mkuu wa gereza hajaja
mnasikia?” Askari magereza aliongea kwa msisitizo.
Hakuna aliyemjibu kitu afande bali Prosper alisogea karibu na uzio wa nondo, Belinda nae alifanya vivyo hivyo
mpaka wakakaribiana kabisa na kupenyeza midomo yao katikati ya nondo na kuanza kupigana mabusu mdomoni mbele
ya askari bila kuogopa wala kuona aibu.
Ghafla kabla hawajasema lolote hata kusalimiana wote walianza
kudondosha machozi na baadaye kulia kwa sauti, walionekana kuwa na uchungu
mkubwa mioyoni mwao! Waliangaliana na kukumbuka mambo mengi yaliyotokea katika
maisha yao tangu walipokutana mara ya kwanza shuleni, yalikuwa ni mateso
makubwa mno waliyoyapitia na bado walikuwa wakiendelea kuteseka.
Waliendelea kulia kwa kwikwi kiasi kwamba hakuna mtu aliyeweza
kumwambia mwenzake chochote hadi Prosper
alipoanza kuvutwa na askari magereza kurudishwa gerezani! Machozi yalimbubujika
Belinda kwa wingi, alimwonea huruma sana Prosper na kabla hajaingizwa ndani aligeuka nyuma na
kuwaanglia Belinda na mtoto wake, roho
ilimuuma sana na alitamani mambo yangekuwa tofauti na ilivyokuwa, ndani ya nafsi yake Prosper
alijilaumu kwa uamuzi wake wa kuyakiri mauaji ambayo hakuyatenda jambo ambalo
hata Belinda hakulifahamu.
Mtu aliyekiri mauaji hayo ili amuokoe kutoka gerezani,yaani mama yake
tayari alikuwa ni marehemu na dada zake nao walishamtelekeza gerezani
baada ya kutoka gerezani na yeye kuingia!
“Nakupenda Belinda, ahsante sana kwa kuja tena, nisamehe kwa kila
kosa nililoliyafanya najua sina maisha marefu duniani, kwa sababu watu wenye
virusi hufa upesi sana gerezani isitoshe nimeshahukumiwa kifo tayari, namuonea
huruma sana mwanangu kwa sababu hataishi kuja kuniona mimi baba yake! Tafadhali
Belinda mtunze vizuri mtoto wetu Alicia lakini usije kumwambia niliua!” Alisema
Prosper huku askari magereza akisubiri amalizie.
“Prosper elewa ninakupenda
sana na nimekwishakukusamehe makosa yako yote
na nimesikitika kujua unakufa na kuniacha mimi!” Alisema Belinda akijua
hiyo ndiyo ilikuwa mara ya mwisho kuonana na Prosper kwani angenyongwa kama
hukumu ilivyotolewa.
Pamoja na kujua Prosper alikuwa na virusi vya Ukimwi kama ambavyo
yeye Belinda aliamini kuvipata kutoka kwake na yeye kuvipeleka kwa mtoto wao
Alicia, bado Belinda hakuwa tayari kukubali Prosper anyongwe, alimpenda mno na
hakutaka kumpoteza! Alitaka waishi pamoja mpaka watakapozidiwa na kufa kwa
Ukimwi ikiwezekana siku moja wote watatu.
“Sipendi Prosper anyongwe na ningekuwa na uwezo wa kuliepusha hili
ningefanya, siku thelathini za kukata rufaa bado zipo kama ningekuwa na pesa
ningeweka wakili ili angalau afungwe kifungo cha maisha si kunyongwa!”
Alishuhudia Prosper akisukumwa na
askari magereza kuingizwa gerezani,
Belinda alibaki akishangaa bila kujua la kufanya na hakujua baada ya
kutoka gerezani angeelekea wapi!
Alitamani kurudi nyumbani kwa baba yake
lakini kila alipokumbuka yaliyompata mara ya mwisho alipokwenda alishindwa
kufikia uamuzi huo.
“Mdogo wangu unaweza kuja
Jumamosi au Jumapili, ndiyo siku ya kuona wafungwa!” Alisema askari magereza
baada ya kurudi na kumkuta Belinda.
“Ahsante sana dada kwa kweli
ninakushukuru mno kwa msaada wako Mungu atakulipa!”
“Huyo ndiye mumeo?”
“Ndiyo na ndiye baba wa
mtoto huyu!”
“Ulisema wewe ni mtoto wa mzee Thomson Komba?”
“Ndiyo!”
“Mama yako ni yupi?”
“Mke wake wa kwanza achana na
huyu aliyepo hivi sasa ambaye ni mama wa David na John!”
“Kwa hiyo wewe mama yako ni aliyefariki?”
“Ndiyo!”
“Sasa kwanini usirudi ukae nyumbani kwa baba yako kama mumeo
amehukumiwa kunyongwa?”
“Dada…wee acha tu!” Belinda aliongea kwa masikitiko.
“Kwanini unasema hivyo?”
“Huwezi kuamini baba yangu hataki hata kuniona, alinifukuza kama
mbwa kila ninapokwenda nyumbani hunifukuza!”
“Kwanini?”
“Eti kwa sababu nilipata mimba ya huyu mtoto hawakutaka iwe
hivyo nimetengwa kabisa na
familia yangu!”
“Pole sana, sasa ukitoka hapa utakwenda wapi?”
“Kwa kweli sijui ila Mungu mwenyewe anaelewa, najua hawezi
kuniacha!”
“Ningeweza kukuchukua ukae nyumbani kwangu lakini nina chumba kimoja tu na nina familia kubwa,
ninakuhurumia lakini sina la kufanya kukusaidia!”
“Hakuna shida Mungu anafahamu yote!”
*************
Baada ya kuondoka gerezani Belinda alianza kutembea kuelekea kituo
cha mabasi cha Segerea, akiwa njiani mvua kubwa ilianza kunyesha na
kuwalowanisha yeye na mtoto wake.
Alihofia mtoto wake kupata kichomi
lakini hakuwa na la kufanya ilibidi aendelee na safari yake hadi kituoni ambako
alisimama peke yake akisubiri magari
lakini halikupita gari lolote kuelekea
mjini, alisongea pembeni na kujikinga mvua chini ya mti na kuendelea kusubiri
gari ambalo lingepita.
Akiwa katika dimbwi la mawazo ghafla alishtukia gari moja likipita
kwa kasi kubwa na mbele kidogo lilisimama na kuanza kurudi kinyumenyume,
Belinda alipoliona alijua ni msamaria mwema
amemwona yeye na mtoto wake akawahurumia na kuamua kuwapa msaada wa
usafiri.
Alianza kukimbia kulifuata gari hilo wakati likirudi nyuma, alipolifikia alizunguka
upande wa dereva na kuinamisha kichwa chake ili aongee naye lakini dirisha
liliendelea kufungwa ilionekana watu waliokuwa ndani walikula kiyoyozi cha
kasi, dakika moja baadaye Belinda akiendelea kulowa dirisha lilianza
kufunguliwa taratibu.
Hakuyaamini macho yake kwa alichokiona ndani ya gari hilo, kulikuwa
na watu wanne na kila mmoja wao alikuwa ameshika chupa ya bia mkononi mwake!
Walionekana ni watu waliolewa na waliongea kwa sauti ya juu kupita kiasi!
“Wee kuku unakipeleka wapi hicho kifaranga chako?” Ilikuwa ni sauti
ya dereva na sauti hiyo haikuwa ngeni kabisa masikioni pa Belinda ingawa dereva
mwenyewe alivaa kofia kubwa iliyofunika uso wake na aliongea akiwa ameinamisha
kichwa sababu ya kulewa!
Wasichana wote ndani ya gari hilo walicheka kusikia mwanamke mwenzao
anaitwa kuku! Dereva alivua kofia yake ndipo Belinda alipotambua alikuwa ni David kaka yake wa kambo! Nyuma alikaa
mdogo wake John naye akiwa amekumbatiwa na
msichana mrembo kupita kiasi! Kila mtu alikuwa na chupa ya bia mkononi
mwake.
“Ingia kwenye buti tukupe lifti kifaranga chako kitapata kichomi!”
Lilikuwa ni tusi jingine tena kwa Belinda kutoka kwa mtu waliyechangia naye
baba, roho ilimuuma sana Belinda ukizingatia mali zilizowatia kiburi zilikuwa
ni za baba yao wote.
“Mpenzi ondoa gari bwana nini achana na kichaa huyo!” mrembo
aliyekaa pembeni kwa David alisema na gari lilianza kuondoka kwa kasi
likimmwagia Belinda matope mengi! Alisikia kitu kama miba kikimchoma moyoni
mwake yalikuwa ni maumivu ya moyo!
Akajikuta amekaa chini kuanza kulia.
Belinda aliona dunia kwake ni kama jehanamu, alikuwa akiadhibiwa kwa
kosa ambalo hakulielewa, kila upande ulikuwa umemgeukia yeye hakuwa tena na
mahali pa kukimbilia, alijihisi kuwa na mkosi.
“Ee Mungu kwanini mimi tu?”Belinda alijiuliza huku akilia machozi.
Sekunde chache baadaye akiwa amekaa chini mvua ikiendelea
kumnyeshea, alisikia honi nyuma yake, kumbe alikuwa katikati ya barabara bila
kufahamu, gari hilo lilikuwa ni daladala!
“Huyu sijui chizi?” Dereva aliwaambia abiria waliokuwa ndani ya
gari.
“Inawezekana ni chizi kweli?”
”Piiiii!Piiiiii!Piiiii!” Dereva
alizidi kupiga honi.
Belinda alijinyanyua taratibu kutoka katikati ya barabara huku
akipunga mkono kumwomba dereva asimamishe gari ili apande lakini dereva aliondoa gari bila kujali, alisimama
aliposikia kelele za abiria zikimwomba
asimame na kumsaidia Belinda na mtoto wake.
“Simama bwana umsaidie hata kama ni chizi ana mtoto mdogo anayelowa
na mvua!” Mama mmoja aling’aka ndani ya gari.
Gari lilisimama na Belinda alikimbia mbio na kupanda ndani ya gari,
nguo zake zilidondosha maji kiasi cha kuwalowanisha abiria wengine ndani ya daladala hilo! Wengi
walifoka na watu wote waliokuwa karibu yake walilalamika vibaya, kabla hajakaa
vizuri kitini dereva alisikika akipiga
kelele kwa sauti ya juu!
“Jamani ajali!Gari
linadumbukia darajani!”
Kufuatia sauti hiyo abiria wote walitupa macho yao mbele kuangalia ni kitu gani kilikuwa kimetokea,
Belinda alikuwa miongoni mwa watu waliofanya jambo hilo kweli gari
lilikuwa darajani tena ndani ya maji
ya mto uliokwenda kwa kasi ni sehemu ya juu tu iliyoonekana.
Dereva alipolifikia daraja alilisimamisha gari pembeni na watu wote
walishuka na kukimbia darajani kwenda
kuona kilichotokea hata Belinda
alifuata nyuma akiwa na mtoto wake mgongoni mvua ilikuwa bado ikinyesha!
“John tuna kamba kwenye gari?” Dereva alimuuliza konda.
“Ndiyo!”
“Itoe ili tujaribu kuvuta hii gari tuone itakuwaje inawezekana kuna
watu ndani!”
“Poa Suka!”
Dereva na utingo wake walikimbia kwenda mahali lilipokuwa gari na
dereva aliligeuza na kuanza kulirudisha kinyumenyume kuelekea darajani, mita kama kumi hivi
alilisimamisha na likafungwa kwa kamba
na kuanza kuvutwa!
Ilikuwa kazi ngumu
lakini kama saa nzima baadaye
magari la watu wengi wakiwepo eneo la tukio kutoa msaada gari
liliopolewa kutoka majini.
“Masikini kuna watu ndani, tena wamekufa tena wakiwa wamekumbatiana”
Mtu mmoja alipiga kelele baada ya kuchungulia ndani ya gari lilipotolewa
majini.
Belinda hakutaka kuwa mvumilivu alisogea karibu ili naye ashuhudie
kwa macho yake! Tukio hilo lilionekana kumsahaulisha kidogo matatizo
aliyokuwa nayo hivyo alisogea karibu. Milango ya gari
ilipofunguliwa mbele ya macho yake na maiti
kuanza kutolewa, alianguka chini na kulia alipogundua kuwa walikufa
walikuwa ni kaka zake waliompita kituo cha basi na kumkebehi, pamoja na
kumfanyia kitendo kibaya.
“Ni kaka zangu! Ni kaka zangu! Jamani ni kaka zangu!”Belinda alizidi
kulia na kupiga kelele akipita katikati
ya makundi ya watu, alionekana kuwa amechanganyikiwa na wanawake
wawili walimnyang’anya mtoto na wengine
walimshikilia ili asifanye vurugu zaidi.
“Unakaa wapi dada?” Mtu mmoja aliuliza lakini Belinda hakujibu kitu, alishindwa kusema moja
kwa moja kuwa aliishi kwa mzee Thomson Komba kwa sababu alikuwa na muda mrefu
tangu afike eneo hilo.
“Nyumbani kwenu ni kwa nani dada?” Dereva wa gari hilo naye aliuliza
swali hilo hilo!
“Kwa mzee Thomson Komba!”
“Mzee Thomson Komba? Una uhakika?”
“Mimi ndiye mtoto wake wa kwanza na hawa waliokufa ni kaka zangu ila
wasichana wao ndiyo siwafahamu!” Belinda aliongea huku akilia machozi.
“Una namba za simu ya nyumbani kwenu?”
“Ndiyo ni 0744-382856, hiyo ndiyo namba ya simu ya baba ya mkononi”
“Jamani nani ana simu kati yetu?” Dereva aliuliza abiria mmoja
aliyejitokeza na kutoa simu yake itumike, walimpigia mzee Komba na pia
kuwataarifu polisi.
Mzee Komba alipata mshtuko mkubwa sana na saa moja tu baadaye
alifika eneo la tukio akiwa na mke wake na kukuta maiti za watoto wake zikiwa
zimelazwa chini kwenye nyasi! Alilia machozi kwa uchungu, Belinda alijificha
katikati ya watu akilia alimwogopa sana
baba yake na alijua angeweza kumuaibisha mbele za watu!
“Watoto wangu hawa niliwaeleza kila siku juu ya tabia yao mbaya ya
ulevi na hawakunisikia, hatimaye leo
mabaya yamewakuta!” Alisema mzee Thomson Komba kwa uchungu na mkewe aliitikia
kwa kilio.
“Masikini sina mtoto tena zaidi, hivi sasa tegemeo langu ni kwa
mwanangu Belinda! Nitamtafuta popote alipo ili arudi nyumbani haraka
iwezekanavyo! Nitamtafuta kwa gharama
yoyote ile!” Alisema mzee Thomson kwa
sauti huku akilia, maneno hayo yalimfikia Belinda moja kwa moja akiwa katikati ya watu.
Belinda hakuamini kama maneno yale yalitoka mdomoni mwa baba yake
aliyemchukia siku zote! Belinda alijikuta
akimwonea huruma baba yake na
chuki yote aliyokuwa nayo moyoni juu ya baba
yake iliyeyuka! Belinda akitetemeka
alianza kutembea kupita katikati ya watu kwenda mbele alitaka amwambie baba
yake kuwa alikuwa maeneo yale.
“Baba!Baba!Baba!” Hatua tatu kabla hajamfikia baba yake Belinda
alimwita mzee Thomson na aliisikia sauti
hiyo na kugeuka nyuma kuangalia na kuanza kumfuata akiwa amepanua mikono yake
ili amkumbatie.
“Mwanangu Belinda kaka zako wameku… ! Kabla mzee Thomson
hajaimalizia sentensi yake, Belinda kwa macho yake alimshuhudia baba yake
akilegea na kuanguka chini kama mzigo na kugeuza macho juu! Belinda akiwa na
mtoto wake mgongoni alianguka juu ya baba yake na kuanza kumtingisha baba
yake lakini hakuitikia, na alianza
kutoa damu mdomoni na puani watu wote walishangazwa na kilichokuwa
kimetokea.
“Yaani watoto wamekufa na baba pia?” Abiria mmoja aliuliza kwa
huzuni.
Maiti zote zilibebwa na kupakiwa ndani ya magari yaliyokuwepo
eneo la tukio na mzee Komba akiwa hoi alipakiwa katika gari lake akifuatana na
mkewe pamoja na Belinda akiwa na mwanae mgongoni wote ndani ya gari hilo
walilia machozi, ilikuwa huzuni kubwa mno kwao.
Pamoja na kulia kwa uchungu mke wa mzee Komba
bado alionyesha chuki yake kwa Belinda waziwazi, kila mara alimwangalia kwa macho ya hasira na kumsonya, alionekana
kutopendezwa na kuwepo kwa Belinda na
mtoto wake katika tukio hilo.
“Na wewe umefikaje hapa na hicho kitoto chako si nilisikia ulikuwa
Tabora?” Aliuliza mama huyo kwa nyodo.
“Mamaaa!” Belinda aliongea kwa sauti.
“Mama yako nani?”
“Tuyaache yote haya
ninachotaka kusema ni kuwa tusahau tofauti zetu ili tushughulikie
matatizo yaliyopo , David na John wamefariki na baba ndiye huyu anaumwa kupita
kiasi!” Alisema Belinda kwa uchungu.
Maneno ya Belinda yalimchoma sana mama huyo moyoni mwake na
kumkumbusha watoto wake wawili ambao tayari walikuwa marehemu na walikuwa ndani
ya gari lililokuwa mbele yao likielekea chumba cha maiti cha hospitali ya Muhimbili.
Kwake yote yaliyotokea yalikuwa ni kama ndoto! Hakuamini kama David
na John walikuwa wamekufa, Belinda alimshika begani na kuanza kumbembeleza
ili asilie zaidi lakini aliendelea kulia zaidi, mama huyo aliushika
mkono wake na kuutupa pembeni akionyesha kutofurahishwa kabisa na kitu ambacho
Belinda alifanya.
“Toka hapa unanibembeleza kitu gani? Si ni heri ungekufa wewe na
hicho kitoto chako kama kuzimu wahitajika watu wawili badala ya kufa watoto
wangu!” Alisema mama huyo huku akimwangalia Belinda kuanzia miguuni, macho yake
yalipofika kichwani yalianza kushuka
tena hadi miguuni kisha akasonya kwa
nguvu!
Belinda alijisikia kudhalilishwa kiasi cha kutosha alijisikia kama
yu uchi wa mnyama! Alitamani kuwa na mama aliyempenda lakini mama yake hakuwepo
duniani alishafariki miaka mingi na baada ya kufariki mama yake na kumwacha
Belinda akiwa mtoto mchanga ndiyo baba yake alipomuoa mwanamke huyo.
Walipofika hospitali ya Muhimbili walipokelewa, gari lililobeba
maiti lilipitiliza hadi chumba cha maiti
ambako miili ya John na David pamoja na wasichana waliokuwa nao
ilihifadhiwa katika majokofu, baadaye
taarifa ilitolewa polisi juu ya
ajali hiyo.
Haikuchukua muda mrefu habari zikawa zimekwishasambaa kila
sehemu ya jiji la Dar es Salaam kuwa
watoto wa mzee Komba walikuwa wamefariki dunia baada ya gari lao kuacha njia na
kudumbukia mtoni! Shule ya makongo waliyosoma
watoto hao iligubikwa na masikitiko makubwa, karibu kila mtu shuleni
hapo hadi walimu walilia.
*********************
“Hiki ni kiharusi mzee huyu alishtuka sana ndiyo maana hali hii
ilitokea!”!” Alisema daktari baada ya kumpima mzee Komba
Baada ya kupimwa alichukuliwa
na kupelekwa katika wodi ya wagonjwa mahututi, iliyotumiwa na watu wenye pesa na
viongozi mbalimbali na kuanza kupewa matibabu ya uhakika, fahamu
zake hazikurejea mpaka baada ya siku
pili alipozinduka na kumkuta
Belinda pembeni ya kitanda chake akiwa na mtoto wake mgongoni.
“Baba!Baba!Baba!” Belinda aliita
hakuamini kama baba yake alikuwa amefumbua macho baada ya kukaa bila
fahamu kwa masaa zaidi ya arobaini na
nane.
Mzee Komba aliangaza macho yake huku na kule chumbani hakuona mtu
mwingine zaidi ya Belinda.
“Ma..ma..ya..ko..yu..po..wapi?” Aliuliza mzee Komba.
“Yupo nyumbani baba!”
“Nyumbani wapi?”
“Nyumbani kwetu!”
“Kwani hapa ni wapi?”
“Hapa ni hospitali!”
“Kwanini nipo hapa?” Mzee Komba aliuliza lakini Belinda alishindwa
kumsimulia kilichotokea kwa kuogopa kumsababishia matatizo zaidi.
“Kwanini nipo hapa?” Mzee Komba aliuliza tena.
“Uliugua ghafla!”
“Niliugua ugonjwa gani na kwanini?”
Kabla hajajibu mlango ulifunguliwa na daktari akaingia na kundi la
wauguzi na madaktari kama watano hivi!
“Ha! Leo mzee Komba anaongea?” Daktari mkuu aliuliza, watu wote
walionekana kushangazwa sana na hali hiyo, kila mtu alisogea karibu na kitanda
cha mzee Komba na kuanza kushangaa.
“Dada tunaomba utupishe
kidogo tumpime mzazi
wako!”Daktari alimwomba Belinda na bila kusita
alifungua mlango na kutoka nje
akiwaacha madaktari bado wanamshangaa baba yake.
Akiwa nje ya wodi mawazo yake yalimrejesha tena gerezani na kuanza kumfikiria Prosper, kila fikra kuwa angenyongwa na kufa zilipomwijia
kichwani mwake aliumia zaidi na kulia!
Kila upande kwake ulikuwa na maumivu, baba alikuwa mgonjwa na Prosper alikuwa
gerezani.
Baadaye madaktari walitoka nje na kumwomba Belinda aingie lakini
walimuonya juu ya kuongea habari yoyote ya
kusikitisha na baba yake, alipofika ndani alimkuta baba yake
akibubujikwa na machozi, Belinda
aliinama na kuanza kumfariji.
“Tafadhali nieleze usifiche kitu ni nini kilichotokea hadi nikawa hapa?”
“Uliugua tu baba!”
“Ugonjwa gani?”
“Homa!”
“Homa? Haiwezekani hata kidogo, hii siyo homa mbona mwili wangu
umepooza wala sijisikii kabisa?”
“Usiwe na wasiwasi baba utapona tu!”
“Mwanangu Belinda naomba sana unisamehe kwa yote niliyokutendea ni
mama yako wa kambo aliyesababisha! Najuta kwanini nilifanya hivyo! Hali yangu
ni mbaya na ninafahamu nitakufa, sitaki
kukuachia matatizo baada ya kifo changu
ninaelewa ni kiasi gani mama yako hakupendi hivyo kuna uwezekano ukakosa
kitu chochote kutoka katika mali zangu
nenda upesi ukalete karatasi nikuandikie urithi!”
Maneno hayo ya mze Komba yalimtisha
Belinda, alijua pamoja na
kuonyesha hali nzuri kulikuwa na jambo baya ambalo lingetokea katika muda mfupi!
“Nipe maji ya kunywa kwanza kabla hujaondoka mwanangu!” Mzee Komba
alisema.
Mara nyingi Belinda
alishasikia watu wakisema kitendo cha
mgonjwa kuomba maji akiwa katika hali mbaya ni dalili ya kuaga dunia!
Aliyakumbuka maneno hayo lakini hakutaka kuyatilia maanani wala kuyachukulia
kuwa ni kweli, aliiona ni imani ya watu na kunyanyuka kwenda kumimina maji katika glasi na kumpa baba yake.
“Belinda fanya haraka
uniletee karatasi, sitaki upate shida nina wasiwasi mama yako hatakupa
kitu chochote kile baada ya kifo changu!”
Belinda alitoka mbio hadi ofisini kwa wauguzi na kuomba msaada wa
karatasi na kalamu, wauguzi walimpatia
vitu vyote alivyohitaji na kuondoka mbio
ofisini! Hali hiyo iliwashtua wauguzi ikabidi wamfuatilie, walimkuta mzee Komba akiandika maneno fulani
kwenye karatasi huku mkono wake
ukitetemeka, mwandiko ulikuwa mbaya mno na aliandika maneno machache sana
yaliyotaja nyumba mbili zilizokuwa katikati ya jiji la Dar es Salaam kuwa zilikuwa mali ya Belinda tangu siku
hiyo! Alipomaliza kuandika aliwapa wauguzi wakaisoma karatasi hiyo.
“Man...esi nyie ndi..o mmes..huhudia jam...bo hili tafadhali
nitili...eni sahihi ze..nu hapo juu
kabla sijafa!” Alisema mzee Komba na kuwapa manesi karatasi.
“Mzee Komba huwezi kufa utapona tu!”
“Mimi mwenyewe najua hali niliyonayo!”
Bila kusita wauguzi walifanya hivyo na kuanguka sahihi zao juu ya
karatasi hiyo nyeupe, wauguzi wote pamoja na Belinda walikodolea macho karatasi
na kumsahau mgonjwa kitandani kwa muda! Walipomaliza kutia sahihi waliirudisha
karatasi hiyo kwa mzee Thomson Komba lakini
hakuipokea ingawa mkono wake ameunyoosha kama mtu aliyetaka kupokea
kitu!
Walipoiweka barua hiyo mkononi ilidondoka chini, kila mtu alishangaa
sana na Belinda alipotupa macho yake
usoni kwa baba yake alichokiona kilimfanya
alie kwa sauti ya juu macho ya mzee Komba yalikuwa yametoka nje na
alikuwa akitupa shingo yake huku na kule kama mtu aliyekuwa akikata roho!
Mmoja wa wauguzi alipoona hivyo alitoka mbio kwenda hadi chumba cha
daktari lakini hakumkuta, alikuwa wodini akiendelea na raundi yake, alikimbia hadi wodini ambako alimkuta daktari
na kumpa taarifa za tukio hilo na wote
waliondoka mbio kwenda hadi chumbani kwa mzee Komba.
Walipoingia chumbani walimkuta Belinda akilia machozi kwa sauti ya
juu! Daktari alinyoosha hadi kitandani na kuanza kumpima mgonjwa, alinyanyua
uso wake dakika kama mbili hivi baadaye alikuwa na huzuni kubwa alimkumbatia
Belinda na kuanza kumpigapiga mgongoni.
“Binti nasikitika mzee amefariki! Nini kimetokea wakati nimemwacha anaongea?”
Alisema daktari.
“Hali yake ilibadilika ghafla!” Alijibu Belinda.
********************
Taarifa za kifo cha mzee Komba zilipelekwa nyumbani kwake ambako shughuli za mazishi ya watoto wake
wawili David na John ziliendelea, mke
wake alilia kupita kiasi kufuatia habari hizo na kuondoka kwenda hadi
hospitali kuuchukua mwili wa mumewe! Ilikuwa ni siku ya huzuni kubwa mno kwake
kupoteza watu watatu katika siku moja
kila mtu jijini Dar es Salaam alihuzunishwa na tukio hilo na mamia ya watu walikusanyika nyumbani kwa mzee
Komba ambako mazishi yalifanyika.
Wote watatu wakawa wamezikwa kwa siku moja na Belinda akiwa nyumbani
kwao kushuhudia mazishi hayo, alilia mno kila alipomfikiria baba yake na
alijisikia kumsamehe kwa yote aliyomtendea.
Pamoja na kufiwa na baba na ndugu zake bado Belinda hakusahau hata
siku moja kuwa Prosper alikuwa gerezani, Jumapili iliyofuata alikwenda tena
gerezani na kuonana naye na alimpa taarifa juu ya kifo cha baba yake, Prosper alionyesha masikitiko makubwa
sana!
“Bahati mbaya sikuwahi kukutana na baba yako ana kwa ana!”
“Usijali Prosper haikupangwa mkutane!”
Wiki moja tu baada ya kifo
cha baba yake matatizo mazito yalianza kumpata Belinda nyumbani kwao, mama yake
wa kambo alianza kumfukuza pale nyumbani akidai arudi alikotoka! Hilo
halikumsumbua sana Belinda ukizingatia tayari alikuwa na wosia
wa kurithishwa nyumba mbili za mamilioni ya pesa katikati ya jiji, alichofanya
ni kuondoka nyumbani na kwenda kwenye moja ya nyumba zake na kujitambulisha kwa
wapangaji ili wafahamu kama mmiliki wa nyumba walizoishi.
Moja ya nyumba iliyokuwa mtaa wa Mafia namba 30, ilikuwa na chumba kimoja katika ghorofa yake ya pili kilikuwa na kila
kitu ndani, kabla ya kifo chake baba yake alikitumia kupumzika kila
alipokuwa na mawazo.
Belinda alitafuta mafundi wa
ujenzi na mlango wa chumba
ukavunjwa, akaingia ndani hicho kikawa ndiyo chumba chake na maisha
yake na mtoto wake yakahamia hapo, pesa
aliyopata kutoka kwa wapangaji ilimsaidia kuendesha maisha yake ya kila siku. Mambo
yalianza kuwa mazuri Belinda alianza
kunawiri lakini mawazo yake yaliendelea kubaki kwa Prosper gerezani, wazo la kumsaidia kutoka gerezani lilianza kumwingia akilini.
“Labda nikikata rufaa
inawezekana kumfanya asinyongwe,
nitauza nyumba yangu moja pesa nitakayopata
nitamlipa wakili wa kunisaidia katika kesi kwani nyumba ni bora kuliko Prosper?” Aliwaza
Belinda na kweli siku iliyofuata alikwenda moja kwa moja ofisini kwa mzee Rutashobya, mmoja wa mawakili
maarufu katika jiji la Dar es Slaam na kumweleza matatizo aliyokuwa nayo ili aone
kama angeweza kumsaidia.
“Ni lini hukumu ilitolewa?”
“Wiki iliyopita tu!”
“Basi bado tuna muda wa kukata rufaa nitajaribu kufanya hivyo lakini
utanilipa shilingi milioni tano unazo
pesa hizo?”
“Pesa sina ila nina nyumba ambayo nitaiuza kisha nitakulipa pesa
hiyo!”
“Kwanini usinipe hiyo nyumba
mimi tumalizane?” Wakili aliingiwa na tamaa ya kujipatia mali kwa njia rahisi.
“Hapana ni vyema tu niiuze na
nikulipe pesa unayodai na nyingine
inisaidie mimi na mtoto wangu!”
“Sawa, basi kesho nitasafiri
kwenda Tabora kukata rufaa, nitakusaidia binti usiwe na shaka!” Alisema wakili
Rutashobya mzee mwenye umri kati ya hamsini na sitini hivi!
Siku iliyofuata Belinda alitafuta madalali wa City Auction Mart na kuwaeleza nia ya kuiuza
moja ya nyumba zake na aliwaonyesha barua aliyoachiwa na marehemu baba yake,
waliichukua barua hiyo hadi kwa mama yake wa kambo na kumwonyesha, hakuwa na
kipingamizi chochote kwa sababu mali aliyoachiwa
ilikuwa nyingi zaidi.
Nyumba ikapigwa mnada kwa shilingi
milioni 25! Belinda alifurahi kupata pesa na bila
kuchelewa alifungua akaunti katika benki
ya NBC na kuziweka pesa zote benki ili zimsaidie katika kesi! Alitaka
sana kumtoa Prosper gerezani pamoja na kuambukizwa Ukimwi bado Belinda
alimpenda kupita kiasi.
“Sitaki afe kwa kunyongwa!
Nataka mimi na yeye na Alicia mtoto wetu tuishi pamoja tena tukisubiri kifo chetu cha Ukimwi basi!”
Aliwaza Belinda.
Post a Comment