ad

ad

KIFO CHA MTU ASIYE NA HATIA - 06



 Dunia ilionekana kubadilika na kuwa sehemu ya mateso makubwa kwa Belinda. Hakuamini  kama   binadamu wote waliishi katika shida kama alizokuwa nazo yeye, alibadili matatizo kama nguo! Likitoka hili linaingia jingine, Belinda alihisi kukata tamaa. Baya na lililomsumbua zaidi lilikuwa ni la virusi za Ukimwi ambavyo alihisi Prosper aliambukizwa na Savimbi katika mchezo wa  wanaume kwa wanaume kuingiliana gerezani.
Belinda alikuwa ameamua kuufahamu ukweli  wa majibu ya damu kutoka kwa Prosper ili auondoe wasiwasi moyoni mwake
“Ulipimwa damu?”Belinda alimuuliza Prosper!
“Ndiyo nilipima Belinda!”
“Majibu yako wapi?”
“Ninayo!”
“Nipe basi niyaone!”
“Naogopa kukupa!”
“Kwa nini? Wewe nipe tu!”
“Sijui kama utaweza kuyakubali!”
“Kwani una virusi katika damu yako Prosper?”
“Nd….i…o Belinda ila nisamahe sana!” Prosper alianza kulia machozi na alishindwa kumwangalia Belinda usoni.
“Kweli?” Belinda aliuliza tena, hakuliamini jibu alilopewa.
“Prosper tafadhali nionyeshe cheti chako cha majibu!” Aliendelea kusisitiza Belinda.
“Niamini na  naomba unisamehe sana Belinda!”
“Nipe cheti Prosper siwezi kuamini hivi hivi!” Belinda alisema kwa ukali.
Katika maisha yake Prosper  hakuwahi kumwona Belinda katika hali hiyo, ilimlazimu aingize mkono ndani ya kaptura yake, alionekana   akivuta  kitu fulani ndani ya nguo yake ya ndani na mkono ulipotoka ulikuwa na kikaratasi kidogo kilichokunjwa kikiwa kimelowa jasho alimkabidhi Belinda!”
Huku akitetemeka Belinda  alianza kukikunjua kikaratasi hicho na kuanza kukisoma, kadri alivyozidi kusoma ndivyo machozi yalivyozidi k ummiminika  hatimaye alijikuta akilia machozi huku kichwa chake akiwa  amekiinamisha chini! Kilionyesha tayari Prosper alikwishaambukizwa virusi vya Ukimwi.
“Hivi mimi nina mkosi gani?”
“Wewe huna mkosi hata kidogo Belinda, mwenye mkosi ni mimi niliyewaua  wewe na mwanangu bila hatia”
“Prosper ni heri  ningekufa mimi kuliko  Alicia ana makosa gani mtoto huyu?” Aliongea Belinda huku akizidi kulia.
Prosper alipomwangalia mwanae Alicia mikononi mwa mama yake naye alijikuta machozi mengi zaidi yakimtoka, alijilaumu kwa  kila kitu kilichotokea na  alijilaumu kwa kuua watu wasio na hatia, alijisikia mkosaji mbele za Mungu na mbele za Belinda na Alicia! Kwa kosa hilo aliamini hakustahili kuishi.
“Prosper nimejitahidi kuwa mwaminifu kwako lakini bado umeniua, nimeacha mambo mengi pamoja na utajiri wa baba yangu kwa ajili yako na   ninateseka leo hii tena umenitia virusi vya Ukimwi mwilini mwangu!”
“Belinda ni shetani aliniingia usinilaumu sana  Belinda utanifanya nikose sababu ya kuishi!” Prosper alipiga magoti mbele ya Belinda na kuanza kumshika miguu kama ishara ya kumwomba msamaha!
“Hii haitoshi Prosper umekwishaniua basi inatosha!”
“Sikujua itakuwa hivyo Belinda ilitokea  kama ajali  na kama ningepewa nafasi nyingine nisingefanya hivyo na ninajuta   moyoni mwangu  nisamahe Belinda kwa kukatisha maisha yako!”
Belinda hakujibu kitu alibaki amesimama wima   mtoto wake akiwa  mgongoni, alihisi akili yake kuchanganyika, ubongo wake kusimama kufanya kazi sawasawa, alijilaumu kwa kila kitu alichokifanya maishani mwake.
Hakuwa na kimbilio tena maishani kwake  na alikiona kifo chake kikija kwa kasi! Katika maisha yake hakuna kitu alichoogopa kama kifo cha Ukimwi kwani kiliwatesa   watu wengi  na kilionekana kama kifo cha aibu na hakutaka kufa katika jina la umalaya  kama jinsi watu wengi walivyokitafsiri  kifo cha Ukimwi, Belinda aliamini hakuwahi kuwa malaya katika maisha yake.
“Prosper!”
“Naam Belinda!”
“Sitakusamahe maishani mwangu na hata kama nitakusamahe basi sitasahau siku zote!” Alisema Belinda na kuanza kutembea  kwa haraka kutoka chumbani kwenda nje ya gereza.
“Belinda! Belinda! Belinda usiondoke!” Prosper aliita wakati Belinda  akitoka chumbani lakini  hakugeuka kuangalia nyuma alizidi kutembea kwa haraka huku akilia.
            *****************
Alitoka hadi nje ambako alitembea hadi kituo cha mabasi madogo na muda mfupi baadaye daladala moja lilikuja na kusimama pembeni yake,  alimbeba vizuri mtoto wake na kuingia ndani  na kuchukua kiti cha nyuma kabisa, alikuwa bado na hofu ya kusababisha harufu lakini alipokumbuka kuwa alishafanyiwa operesheni na kuwa mkavu hofu hiyo ilitoweka mara moja.
Belinda aliendelea kububujiwa  na machozi  hadi wakati anafika mjini, watu wote ndani ya gari walimshangaa na walipomuuliza ni kwanini alilia machozi kiasi kile hakueleza chochote.
Alipomwangalia mtoto wake mzuri Alicia, aliyekuwa ameketi mikononi mwake roho yake ilimuuma zaidi, alikuwa mtoto mzuri mno kufa kwa Ukimwi! Ilimuuma sana Belinda kujua kuwa hata mtoto wake hakuwa na maisha marefu mbele yake, lakini Alicia hakuwa na taarifa na kilichokuwa kikiendelea aliendelea kutabasamu huku akimpigapiga mama yake usoni.
Alipofika mjini Tabora aliteremka ndani ya basi, alihisi kukata tamaa ya kila kitu! Hakuona sababu ya kurudi tena  Tutuo, kijijini kwao Prosper  alichofikiria wakati huo ni kurudi tena  Dar es Salaam kwa baba yake na kujaribu kumwomba msamaha! Lakini alipokumbuka jinsi baba yake alivyomfukuza  kama mbwa roho iliingiwa wasiwasi na kujikuta akisita kuchukua hatua hiyo.
“Kwa kweli baba asingekuwa na matatizo ningerudi Dar , acha tu nirudi  Tutuo!”
Baada ya kuwaza sana hatimaye mawazo yake yalimfikisha katika hatua  hiyo lakini  alipokumbuka kuwa  nyumba aliyofikia ingekuwa tayari imekwishabomolewa na mwarabu aliyeinunua ili ajenge mashine, Belinda  alikosa mahali pa kuelekea kwa sababu hakuona   mahali  pengine popote pa kufikia kijijini Tutuo.
“ Lakini acha tu niende, Wanyamwezi ni watu wakarimu sana, nitaomba kukaa kwa mtu yeyote au nitarudi tena kuomba kazi nyumbani kwa Mwarabu Mzee Mohamed nafikiri safari hii atakubali kwa sababu sina mimba na sinuki kama ilivyokuwa zamani!”
 Belinda aliamua kurudi kijijini na alichofanya  ni kwenda stendi ya basi ambako alipanda basi la kumpeleka kijijini Tutuo, njia nzima aliendelea kulia alijua maisha yake yalikuwa yamefika mwisho! Alihisi hakuwa na maisha tena  mbele yake, binafsi  hakujionea huruma sana  aliyemtia simanzi zaidi alikuwa ni  mtoto wake Alicia.
“Masikini Alicia anakufa kwa kosa lisilo lake akini kwanini hasa mtu amuue mtoto  asiye na hatia?  Prosper alishindwa  kuvumilia shida? Nasema sitaki kumwona tena maishani mwangu!” Alisema kwa uchungu Belinda, hakujua alikuwa akiongea kwa sauti kiasi kwamba watu wote ndani ya basi waligeuka kumwangalia.
            *******************
Gerezani:
Baada ya kuachwa chumbani Prosper alinyanyuka kwa unyonge na kutembea hadi chumba cha mahabusu  na kwa muda mrefu aliendelea kulia na hakuona tena sababu ya kuendelea kuishi, alitamani kufa kukwepa aibu ya kuwaua mke na mtoto wake kwa Ukimwi lakini alishindwa kuelewa ni kwa njia ngani angeweza kujitoa uhai  akiwa ndani ya gereza.
Alilia usiku mzima hadi asubuhi, alijuta kwa yote aliyoyafanya  na  alitamani sana kuonana tena na Belinda  ili apate kuongea naye na kumwomba msamaha!  Alijua hilo lisingewezekana hata kidogo kwani  alikuwa na  uhakika Belinda  asingerudi  tena.
“Laiti ningejua nisingejiingiza katika mchezo huo  mbaya, shida za gerezani zingeniua mbona watu wengine wanaishi?” Aliwaza Prosper huku akilia.
Prosper alikuwa na  watu wengi sana wa kuwalaumu kuhusiana na suala hilo lakini watu waliopaswa kuzibeba lawama zote hizo walikuwa ni mama  na dada zake kwa kitendo chao cha kumuua baba yake, bila wao kufanya hivyo Prosper aliamini asingeingia gerezani  katika maisha yake!
“Ni wao ndio walilaumiwa niliingia gerezani kumwokoa mama na dada zangu, mama mwenyewe amekwishakufa na hata hao dada zangu hakuna hata mmoja anayefika hapa  gerezani kunitembelea na bado nyumba na  kiwanja alichoacha baba wameuza na kupotea, huu ni ukatili wa hali ya juu sana!” Aliendela kuwaza  Prosper.
Baada ya siku hiyo Prosper hakuwaona tena Belinda  na mtoto wake Alicia, kesi yake  iliendelea katika mahakama kuu kanda ya Tabora na miezi mitatu baada ya Belinda kuondoka kesi   hiyo ilifikia hukumu yake, alionekana kuwa na hatia mbele ya sheria  baada  ya yeye mwenyewe kukiri  mauaji hayo ya baba yake mzazi  mbele ya  jaji Mohamed Simbila na  kuhukumiwa kifo  kwa kuchomwa sindano ya sumu
Mahakama nzima ilipigwa na butwaa baada ya hukumu hiyo,   Prosper hakuonyesha huzuni wala kulia  badala yake alitabasamu kwa furaha baada ya hukumu hiyo kutolewa.
“Una namna yoyote ya kujitetea?”
“Sitaki kujitetea  Mhesimiwa Jaji, hukumu yako ni sahihi na hii ndiyo niliyoisubiri ili iniepushe na kifo cha mateso kilichopo mbele yangu!Nakushukuru sana mheshimiwa jaji na ninakupongeza sana kwa  hukumu hiyo nzuri!” Alisema Prosper huku akicheka.
Bila kuchelewa maaskari walimpiga pingu mkononi na kumwondoa mahakamani, jaji aliyemkuhumu alibaki na maswali mengi sana kichwani mwake, alishafanya kazi ya kuhukumu watu kwa miaka  karibu ishirini na alishahukumu watu wengi  kifo lakini hakuwahi hata siku moja kumhukumu mtu kifo akicheka! Wengi walilia na kuomba kupunguziwa kifungo!
Siku iliyofuata  Prosper  ilitolewa amri  Prosper  ahamishiwe gereza  la Keko  jijini Dar es Salaam  ambako angepambana na kifo chake! Alipakiwa ndani ya treni la abiria kutoka Mwanza kwa safari ya kwenda Dar es Salaam.
Prosper alilia lakini  hakulia sababu ya hukumu ya kifo  aliyopewa ila alilia kwa sababu alikuwa anapelekwa  kufa bila kuonana na mke na mtoto wake kwa mara ya mwisho, alikuwa anakwenda kufa bila Belinda kufahamu ukweli juu yake! Pia alilia sababu yeye alikuwa anakwenda kufa na kuwaacha mkewe na mwanae wakiteseka kwa ugonjwa wa Ukimwi aliowaambukiza  yeye.
               *****************
Alicia, kijijini Tutuo:
Tayari alishazoea maisha ya nyumbani kwa mzee Mohamed, alifanya kazi kwa nguvu zake zote ili aweze kumridhisha mama mwenye nyumba, alipewa chumba kidogo ambacho alilala na mtoto wake kwa kutandika jamvi chini kila siku!
 Ilikuwa ni kawaida yake siku zote kudamka mapema na kufanya kazi  zote za ndani na ilipotimu sawa nne aliacha kazi hizo na kuanza kupasua kuni,   baada ya kupasua kuni alianza kupika chakula cha mchana na baadaye alianza shughuli za ufuaji   wa nguo za kila mtu nyumbani.
Zilikuwa ni   kazi ngumu  lakini Belinda alizifanya ili aweze kuishi na mtoto wake, katika miezi yote    aliyokaa nyumbani kwa mwarabu Mzee Mohamed hakuwahi kumkumbuka Prosper lakini asubuhi ya siku hiyo  akipasua kuni kumbukumbu  za Prosper zilimsumbua kichwani, alitamani sana kumwona na  aliona uamuzi aliouchukua  haukuwa wa  busara kwa sababu usingeweza kuubadilisha kitu chochote  katika maisha yake kama ni virusi alishavipata na ni lazima yeye na mtoto wake wangekufa.
“Ninaamini hivi sasa Prosper anahitaji msaada wangu  kuliko wakati mwingine wowote katika maisha yake!” Aliwaza Belinda huku akiendelea kupasua kuni.
Alimfikiria Prosper kwa muda mrefu hatimaye aliamua kuliweka shoka pembeni na kuketi chini, mawazo juu ya Prosper yaliendelea kumiminika mwake.
“Hapana nakwenda gerezani!” Alisema Belinda na kulitupa shoka pembeni, akambeba mtoto wake mgongoni na kwa kutumia khanga yake iliyochanika alimfunga vizuri na kuondoka kuelekea ndani ambako alimkuta mke wa mzee Mohamed na kumwomba ruhusa lakini hakuruhusiwa kuondoka.
“Belinda wewe hapana ondoka iko kazi nyingi leo!”
“Hapana mama ni lazima nikamwone Prosper   nikishindwa leo ni  mpaka wiki ijayo!”
“Hapana!” Mke wa mzee Mohamed alikataa katakata.
“Mama nimekwishasema naondoka,nitafanya kazi nikirudi!” Belinda alisema na kunyanyuka.
“Wewe ondoka kwa nguvu eh! Pana rudi hapa!”
“Sawa mama!”
           *****************
Alifika gerezani saa nne asubuhi, kitu cha kwanza alichofanya ni kuomba kuitiwa Prosper.
“Dada yangu ulikuwa wapi siku zote hizi?”
“Nilikuwa safarini!” Belinda alidanganya!”
“Karibu sana!”
“Ahsante! Prosper yupo!”
“Prosper?” Askari magereza aliuliza.
“Ndiyo mbona unauliza kwa mshangao!”
“Amesafirishwa jana kwenda gereza la Keko Dar es Salaam,  alihukumiwa kifo!
Belinda alichanganyikiwa na kwa kutumia basi alirudi hadi mjini ambako alipanda basi jingine lililompeleka hadi  Tutuo. Hakukaribishwa tena  nyumbani kwa mzee Mohamed na  kwa sababu hakuwa tena na haja ya kufanya kazi aliomba mishahara yake na kuondoka tena hadi stesheni ya treni  mjini Tabora ambako alipanda treni jioni ya siku hiyohiyo kurejea Dar es Salaam lengo lake likiwa ni kuishi kabla Prosper hajanyongwa!
             *******************
Treni iliingia Dar es Salaam saa saba mchana, Belinda aliona bado muda ulimruhusu kwenda gerezani Keko kuonana na Prosper,  hakutaka kabisa afe kabla hajaongea nae na kumjulisha kuwa tayari alishamsamehe yote yaliyotokea.
Kutoka stesheni ya reli ya Dar es salaam hadi gereza la  Keko ilikuwa kama nusu kilometa hivi, kwa umbali huo mdogo Belinda hakuhitaji gari  alitumia njia ya mkato hadi kufika gerezani.
“Dada mwenye mtoto nikusaidie nini?” Askari magereza aliyekuwa akilinda nje ya gereza alimuuliza
“Nimekuja hapa kumwona mume wangu!”
“Leo siyo siku ya kuwaona wafungwa njoo Jumamosi ama Jumapili umesikia!”
“Sawa lakini……..!” Alisema Belinda huku akimsogelea askari.
“Lakini  nini? Dada hiyo ni sheria ya gereza!”
“Nilikuwa naomba kukuuliza kitu sababu sijui!”
“Kitu gani?”
Belinda alimsimulia askari huyo kila kitu juu ya Prosper na kwamba alitaka kuhakikisha kama kweli alikuwepo  gerezani au la!
“Katokea gereza gani?”
“Isanga Tabora!”
“Nisubiri hapa niulizie!” Alisema askari huyo na kuingia hadi ndani ya gereza na  alipotoka alikuwa na jibu la Belinda.
“Nasikitika hayupo!”
“Hayupo? Hayupo vipi wakati mimi Tabora wamenieleza amehamishiwa gereza hili!”
“Amepelekwa gereza la Segerea sababu hapa hakuna nafasi ya wafungwa kama yeye!”
“Ah! Sawa nashukuru sana kaka yangu!” Belinda alishukuru lakini hakuwa tayari kusubiri hadi jumamosi ndio aonane na  Prosper alihisi kufikia siku hiyo tayari angekuwa  amekwishayongwa!
“Na nitakwenda huko segerea       wakinizuia nitatumia hata hii pesa kidogo niliyonayo mpaka nimwone!” Aliwaza Belinda.
Kutoka gerezani  Keko hadi kituo cha mabasi cha Shule ya Uhuru ambako mabasi ya Tabata na Segerea yaliegeshwa ilimchukua dakika 30  na kutoka shule ya Uhuru sababu ya ubovu wa  barabara ya Tabata  ilimchukua saa nzima  hivyo alifika gerezani segerea saa tisa na nusu ya jioni na kwenda moja kwa moja hadi mapokezi ambako alimkuta askari magereza wa kike.
“Shikamoo dada!” Belinda aliamkia.
“Marahaba, nikusaidie nini mdogo wangu?”
‘Dada unavyoniona hivi ninatoka Tabora, huyu ni mwanangu nimekuja hapa kumfuata mume wangu anaitwa Prosper, yeye  kahamishwa kutoka gereza la Isanga huko Tabora ni mfungwa aliyehukumiwa kifo, nataka kumwona kabla ya kifo chake.
“Kwani vipi mbona unanieleza vitu vingi kwa wakati mmoja?” Askari magereza aliuliza.
“Nisaidie dada, nisaidie mimi mwanamke mwenzio!” Aliendelea kusema Belinda na baadaye kumsimulia askari huyo kila kitu kilichotokea katika maisha yake na Prosper, askari alishindwa kujizuia na kujikuta akichukua kitambaa chake na kujifuta machozi usoni mwake.
“Ni sawa nimehuzunishwa sana lakini sina jinsi ya kukusaidia kwa sababu si rahisi kukuingiza gerezani  siku ya leo mdogo wangu,nenda uje Jumapili!”
“Dada tafadhali nisaidie!”
“Haiwezekani labda nimwite tu umwone kwa mbali lakini siwezi kukuruhusu uingie ndani ya gereza, kwani unaitwa nani?”
“Naitwa Belinda!”
“Belinda nani?”
“Belinda Thomson  Komba!”
“Thomson Komba yule mfanyabiashara?”
“Ndiyo!”
“Sawa wewe mbona una hali hiyo?”
“Maisha tu dada yangu!” Belinda alijibu huku akilia.



No comments

Powered by Blogger.