ad

ad

Singidani (A Story From My Heart) -9



 
ILIPOISHIA...
“Kaka unatafutwa na maaskari. Kumbe yule mwanamke uliyekuwa naye chumbani ni mke wa polisi, tena ni mkuu pale Central. Wamekuja maaskari wanne na silaha wanakutafuta. Mimi nakushauri usirudi tena. Tafuta mahali ulale mpaka asubuhi wakati tukitafuta ufumbuzi wa hili jambo,” alisema dada yule harakaharaka huku akionekana kujawa na wasiwasi mwingi.
Pombe yote ilimruka!
SASA ENDELEA...
I kama alikuwa hajanywa hata tone moja la pombe. Kichwa kilikuwa tupu kabisa. Bado alikuwa na maswali mengi kichwani mwake; inawezekana kweli Laura akawa mke wa mtu? Labda inawezekana lakini vipi amwache mumewe na kwenda kujirusha klabu?
Kichwa kiliwaka moto. Aliumizwa na mengi. Achana na kukamatwa na pengine kufunguliwa mashitaka lakini alijilaumu kwa kujichelewesha kumpata. Angalau angekuwa amefaidi uzuri wake, kidogo ingepooza maumivu ya kile alichoelekea kukikabilia.
Alimwangalia yule msichana kwa jicho lenye maswali lukuki, lakini alionekana kama ambaye hana majibu sahihi ya maswali yaliyozunguka kichwani mwake.
“Sikia dada, mimi huwa sipendi mizaha kabisa. Hebu niambie ukweli, kuna maaskari wamekuja pale?”
“Ndiyo!”
“Wamevaa nguo za polisi?”
“Ndiyo, tena kuna mwingine amevaa koti jeusi.”
Moyo wa Chis ukalipuka.
“Wamenitaja jina?”
“Ndiyo. Wamesema wanamtaka Dk. Chris. Tena alitaka tuwafungulie mlango ili wakague chumba chako, tukakataa. Kwa inavyoonekana itakuwa ni kweli. Hili ni tatizo kaka yangu, tafuta mahali pengine pa kulala.”
Chris akatulia kidogo.
Mawazo yakazidi kumwandama. Kuna kitu aliwaza; iweje leo hii Laura awe mke wa mtu? Mbona hakuwa na pete kidoleni? Laura si mwanafunzi?
“Au kuna mchezo nachezewa?” akajiuliza Chris.
“Halafu kama ni mchezo mtu wa kunisaidia hapa ni mmoja tu, Maulanga.”
Ni kweli Maulanga, dereva taksi aliyekuwa akimtumia kwa mizunguko yake pale mjini ndiye ambaye angeweza kumsaidia kujua ukweli wa tukio lile. Ni Maulanga huyohuyo ndiye aliyempeleka Laura kwenye nyumba anayoishi.
“Kwahiyo dada unanishauri nisije kabisa pale?”
“Huna haja ya kufanya hivyo, lakini kama unaona nakudanganya nenda. Wamesema watarudi tena baadaye, maana wameagizwa na mkuu wao, ukamatwe kabla ya asubuhi.”
Moyo wa Chris ukapiga.
“Sawa, ahsante kwa taarifa. Ngoja nitulize kichwa, nitajua cha kufanya. Kwa sasa naomba tu unisaidie namba yako ya simu tafadhali,” akasema Chris, yule dada akatekeleza.
“Unaitwa nani vile?”
“Mwanjaa.”
“Ok.”
Palepale Chris akaamua kubadilisha kiwanja ili atulize kichwa chake wakati akitafakari cha kufanya. Mwanjaa alirudi zake alipotoka, Chris akachukua bodaboda na kumwambia dereva ampeleke Baa ya Serengeti iliyokuwa katikati ya mji.
***
Chris akiwa Serengeti Bar, alimpigia simu Maulanga na kumwambia amfuate pale haraka sana. Maulanga hakuwa mbali  na eneo, alikuwa ameegesha jirani na Benki ya CRDB, lilipo Jengo la TRA la Mkoa wa Singida. Dakika mbili baadaye alikuwa pale.
“Hivi yule msichana uliyempeleka hosteli jana usiku  unamfahamu?”
“Namuona sana klabu karibu kila wikiendi, huwa anakuja na rafiki zake.”
“Unajua kuwa ni mke wa mtu?”
“Mke wa mtu? Sina hakika kwa kweli.”
“Kivipi?”
“Yaani sifahamu chochote ingawa nahisi kwamba atakuwa ni mwanafunzi. Si anasoma chuo?”
“Kwanini unasema unahisi? Kwani siku ile hukumfikisha hosteli?”
“Kuna nyumba aliingia, akasema anaishi hapo na dada yake.”
“Lakini mimi aliniambia anaishi hosteli. Dah! Sijui hii ishu ikoje! Nasikia wamekuja maaskari pale gesti, wananitafuta.. eti wanasema niliingia na mke wa mtu mle ndani na mumewe ni askari.”
“Mh! Mbona majanga haya kaka. Sasa unafanyaje?”
“Niachie mwenyewe, nitajua cha kufanya. Wewe nenda, nitakuita baadaye.”
“Poa.”
Chris alianza kunywa upya kabisa. Baadaye akapata wazo. Alitakiwa kupumzika ili siku inayofuata aweze kwenda zake kijijini kwao. Wazo la Laura alishalifuta kabisa. Aliona tatizo likiwa mbele yake waziwazi kabisa!
Akatoka pale Serengeti Bar na kutafuta gesti nyingine jirani na eneo lile, akalala. Katikati ya usiku, simu yake ikapigwa. Alipoangalia kwenye kioo cha simu, alishtuka sana.
Alikuwa ni Laura anampigia!
Itaendelea.
Powered by Blogger.