Tambwe: Yanga njooni tuzungumze
Tambwe, raia wa Burundi ambaye mpaka sasa anaongoza kwa kufumania nyavu mara 19 kwenye Ligi Kuu ya Tanzania Bara, anazitoa udenda timu nyingi za ligi kutokana na umahiri wake wa kuchungulia nyavu.
Alipoulizwa kama yupo tayari kujiunga na mahasimu wa Simba nchini, Yanga SC, alisema kuwa mpira ndiyo kazi yake, hivyo atacheza popote ilimradi kuna maslahi.
“Nitacheza popote kwa kuwa mpira ndiyo kazi yangu, timu itabaki kuwa timu na mimi ni mchezaji nitabaki kuwa mchezaji ambaye leo nipo huku kesho nipo kule na kama timu ikinitaka mimi bado ni mali ya Simba, ikazungumze na uongozi kwanza.
“Mimi sitakuwa na shida yoyote kama uongozi utaniambia umekubaliana kuhusu mimi kuondoka, lakini pia kama mkataba wangu na Simba utakuwa umekwisha nitakuwa tayari kuzungumza na yeyote hata kama ni hao Yanga.,” alisema Tambwe huku akionyesha kujiamini.
Tambwe aliwahi kusema kuwa Yanga ilikuwa inamtaka awali kabla hajajiunga na Simba akitokea Vital’ O ya Burundi.
Hata hivyo kwa sasa itakuwa vigumu Simba kumruhusu kuzungumza na klabu nyingine kwa kuwa ndiye amekuwa mkombozi wao kwenye ligi kuu.

Post a Comment