Wabunge CCM wambana Spika
Afuta kesi ya wabunge CHADEMA, awataka wafungue ukurasa mpya.
SPIKA wa Bunge, Anne Makinda, amepata wakati mgumu
kuwashawishi wabunge wakubali mabadiliko ya kanuni mpya zitakazotumika
wakati wa mjadala wa bajeti.
Hali hiyo ilitokea jana ndani ya Ukumbi wa Pius Msekwa ambapo wabunge
wote walikutana pamoja na mambo mengine kupitia mabadiliko ya kanuni
zitakazotumika kwa ajili ya utaratibu mpya wa kupitisha bajeti.
Habari kutoka ndani ya kikao hicho, zilisema kuwa kanuni iliyopingwa
na wabunge wengi, hasa wa Chama Cha Mapinduzi ni ile iliyotaka majina
ya wachangiaji wa mijadala ya bajeti za wizara mbalimbali yapitie na
kuteuliwa kwenye vyama vyao.
Kanuni hiyo ni tofauti na ya sasa ambapo majina ya wabunge wanaotaka
kuchangia, hupelekwa kwa Spika moja kwa moja na wabunge wenyewe na
ndiye anayeteua majina ya wachangiaji.
Kwa mujibu wa habari hizo, idadi kubwa ya wabunge waliopinga ni wa
CCM, ambao walidai kuwa utaratibu huo utakuwa na upendeleo, kwani
viongozi watakaoletewa majina hayo wanaweza wasiyateua kutokana na
tofauti miongoni mwao.
”Sisi tumekataa kwa sababu majina ya wabunge wanaotaka kuchangia
yatapitia kwa viongozi wa vyama bungeni, kisha wao wanayapeleka kwa
Spika. Viongozi hao ni kina Jenister
Mhagama. Kama hakupendi,
hatapeleka jina,” alisema Mbunge mmoja wa CCM.
Mbunge machachari mwingie ambaye amewahi kuitwa mara kadhaa na
viongozi wa chama chake na kumtaka aache kuishambulia serikali, alisema
kuwa utaratibu huo utamnyima haki ya kuchangia bungeni kwani anaamini
hata viongozi wa CCM walio nje ya Bunge, wataingilia kati kutaka asipewe
nafasi.
Mbunge huyo ambaye jina lake tunalihifadhi, alimtaka Spika kuacha
kukwepa majukumu yake.
Endapo kanuni hiyo itapita, itaanza kutumika leo baada ya Waziri
Mkuu, Mizengo Pinda, kusoma hotuba ya bajeti ya wizara yake kwa mwaka
wa fedha 2013/2014.
Kabla ya Pinda kuwasilisha bajeti ya ofisi yake, wabunge wanatarajiwa
kupitisha mabadiliko machache ya kanuni na huenda kukawa na mvutano wa
kupitisha kanuni hizo.
Bunge litaanza kupitia na kujadili hotuba za bajeti za wizara
mbalimbali ambapo mwaka huu zitaanza wizara kabla ya kusomwa kwa bajeti
ya serikali.
Katika hatua nyingine, Spika wa Bunge, Makinda, amefuta kesi ya
wabunge wa CHADEMA waliodaiwa kufanya vurugu katika mkutano wa 10 wa
Bunge mjini Dodoma.
Spika aliwataka wabunge hao kusahau yaliyopita na kuanza moja, kwani lengo la wabunge ni kuwatumikia wananchi waliowachagua.
Habari kutoka ndani ya kikao hicho, zilisema kuwa baadhi ya wabunge
wa CHADEMA walimwonya Spika kuwa kama ataendelea na staili yake ya
kuwabana wapinzani na kukiuka kanuni hawatavumilia.

Post a Comment