Tarehe
3 feb 2013, Chama Cha Mapinduzi kimefanya sherehe zake za kuadhimisha
miaka 36 ya kuzaliwa kwake ambapo kitaifa zilifanyika Kigoma.
Naandika haya kutoa shukrani lakini pia kutoa pongezi zangu za dhati
kabisa kwa wanakigoma. Kwani hapo nyuma tuliambiwa kuwa Kigoma ni ngome
ya UPINZANI lakini hivi sasa nimeshuhudia kuwa SI HIVYO.,bali leo naweza
kutamba kifua mbele na kunadi popote kuwa KIGOMA sasa ni ya CCM.
Nimezungumza nao na kupata ushuhuda wa haki kutoka kwao, wala sikupata
kwenye ripoti bali kutoka katika midomo ya wanakigoma kuwa Hakuna Kama
CCM.
Nguvu ya Chama Chetu inatokana na wanachama wetu na
wanakigoma wameuthibitishia UMMA wa watanzania na Dunia kuwa CCM ina
nguvu.,uwingi wenu kwenye mikutano yetu umetoa tafsiri kubwa na umebeba
taswira halisi ya Imani ya watanzania kwa Chama Cha Mapinduzi.
Natafuta maneno mazuri ya kuelezea shukrani zangu kwenu lakini Kiswahili hakina maneno zaidi ya AHSANTENI SANA.
Pamoja na Hilo, hapo nyuma tulisema kuwa Sherehe hizi zitaambatana na
Tathmini ndani ya Chama, tathmini juu ya kasi na Ufanisi katika
utekelezaji wa Ilani ya Chama. Tumepata fursa adhimu ya kukagua miradi
na kushiriki shughuli za kijamii ndani ya Kigoma na Hakika KIGOMA
imekuwa sample space thabiti katika tathmini wakiwakilisha watanzania wa
maeneo mengine.
Miongoni mwa mambo tuliyojifanyia tathmini ni pamoja na;
i) Katika mikutano mbali mbali iliyofanyika katika wilaya zote, tumeona
umuhimu wa kuboresha mfumo wa kupokea maoni, kero, malalamiko,
mapendekezo na Ushauri wa Wanachama na Watanzania wa kutoka pande zote
za ndani ya nchi na nje ya nchi kupitia simu, barua pepe, mitandao ya
kijamii kama facebook, twitter na blogu na tovuti na pia kwa njia ya
posta. Lakini muhimu zaidi ni kuwa na ofisi maalum ya kusikiliza kero.
Chama kimejifanyia tathmini katika eneo hili muhimu, ambalo ndilo kwa
kiasi kikubwa linaboresha mahusiano ya Chama na wanachama lakini pia na
Umma kwa Ujumla. Kitengo cha mawasiliano na Umma ambacho kipo chini ya
Idara yangu ya Itikadi na Uenezi, kitaratibu na kusimamia mchakato nzima
wa maboresho hayo.
ii) Lakini kuna umuhimu pia wa Kukamilisha
na Kuimarisha task force ya kusimamia zoezi la Utafiti juu ya
Utekelezaji wa sera, Ilani na mambo mengine muhimu ambayo chama
kimeyatekeleza na yale ambayo yanaendelea kutekelezwa. Hii itasaidia
kuwa na Ripoti maalum na zilizo sahihi zitokanazo na Chama chenyewe, na
kuacha utaratibu wa kutegemea taarifa za serikali pekee.
iii)
Eneo jingine, linahusu misingi ya Chama Chetu. Misingi ndiyo nguzo ya
utamaduni wa Chama na wanachama wake; misingi ndiyo nguzo ya nidhamu na
maadili ya Chama na wanachama. Katiba ya Chama Chetu imetaja misingi
mikuu kuwa ni uhuru, haki, udugu, amani, Demokrasia. Misingi hii ndiyo
nguzo ya mshikamano na utulivu wetu. Ni muhimu kutilia mkazo ujenzi wa
itikadi moja na pia Chama kuendelea kuisimamia misingi hii ili kujenga
na kuimarisha Umoja wa kitaifa ili kupinga Ubaguzi, uonevu na unyanyapaa
unaojitokeza katika maeneo mbalimbali nchini.
iv) Na mwisho,
ni malengo muhimu na misingi ya mwelekeo wa shughuli za Chama. Kutokana
na ripoti na taarifa za kazi za Chama iliyotolewa na wajumbe na
watendaji wa Chama Kigoma. Maazimio yalitoa kipaumbele katika Ujenzi wa
Chama ktk maeneo ya Uchumi na kirasilimali ili kukijengea uwezo wa
kuisaidia jamii, kusimamia na kushiriki utekelezaji wa Ilani.
Malengo haya ndiyo ndoto (vision) ya wanachama na wananchi. Malengo haya
ndiyo yanajumuisha matumaini ya Wanachama kuhusu aina ya Chama
wanayoitaka. Mgawanyo wa majukumu kwa vitengo mbali mbali ndani ya Chama
unakusudiwa kuhakikisha kwamba malengo haya yanafikiwa.
Leo tarehe 5 February 2013 ni tarehe rasmi ya Kuzaliwa kwa Chama Cha Mapinduzi,tuendelee kulinda uimara wa Chama Chetu.
Lazima tusisitizane kuhusu uimara na ubora wa chama chetu, tukitambua
hoja na haja ya kuchukua hatua zaidi za kukiimarisha zaidi Chama kwa
kushirikiana kwa karibu na wanachama na viongozi.
Kwa pamoja tunaweza kukijenga kukidumisha na kukiimarisha Chama Chetu ili kiendelee kuwa tumaini na kimbilio la watanzania. “…UMOJA NI USHINDI…”
Post a Comment