ad

ad

She is too young to die (4)




Gilbert anamruhusu mke wake mjamzito Salome kwenda kijijini kwao  huko Kahunda Sengerema kuwaona wazazi wake kabla hajajifungua! Akiwa huko, mvua kubwa zinanyesha  yakiwa yamebaki masaa machache tu kabla hajaondoka kurejea Dar es Salaam ambako yeye na mume wake wanaishi maisha ya kifahari, Gilbert akiwa Mkurugenzi wa kampuni yake binafsi iliyojishuhusisha na masuala ya kompyuta, WorldCom Ltd.
Madaraja yote yamevunjika na kuna mafuriko ya kutisha, kifupi eneo lote la Kahunda limekuwa kisiwa na hakuna mawasiliano kati ya Salome na Gilbert jambo ambalo limefanya achanganyikiwe kabisa hasa kwa sababu anafahamu siku za mke wake kujifungua zimefika! Akitafakari nini cha kufanya anapata ujumbe wa  polisi kwamba mke wake yu katika hali mbaya, anavuja damu nyingi kabla ya wakati na huko aliko hana jinsi ya kutoka.
Jambo hili linamfanya Gilbert afikie uamuzi wa kukodisha helkopta ambayo   anaruka nayo  kutoka Dar es Salaam hadi Mwanza na baadaye   kuelekea maeneo hayo, alichokishuhudia akiwa angani kilimsikitisha! Maeneo yote yalikuwa yamejaa maji, nyumba nyingi zilikuwa zimebakiza mapaa tu juu,  akaamini mke wake alikuwa kwenye matatizo makubwa! Moyoni mwake akajuta ni kwanini  alimruhusu Salome aende kwao.
Upande wa pili Salome anachukuliwa katika gari la kukodi  kwenda  wilayani Sengerema ambako kuna hospitali kubwa, hali yake ni mbaya lakini walipofika kijiji la Bilulumo walikuta daraja kubwa limevunjika, hakuna  mahali pa kupita!  Je, nini kitaendelea? SONGA NAYO…

“Vipi baba?” Mama yake Salome aliyekuwemo ndani ya gari akibubujikwa na machozi bila kutoa sauti alimuuliza dereva.
“Mama hapa hatuwezi kupita!”
“Tutafanyaje mwanangu, kweli Salome afie hapa?”
“Sina jinsi mama!”
“Gari yako haiwezi kupita kwenye maji?”
“Haiwezekani, itavutwa na sote tutakufa! Nashauri tumtegemee Mungu”
Mama  alinyanyuka mahali alipokuwa ameketi ndani ya gari na kushuka chini ambako watu wote walimshuhudia akipiga magoti  na kuanza kusali huku akilia na machozi yake  kuchukuliwa na matone ya mvua yaliyokuwa yakidondoka mashavuni mwake! Alionekana kabisa kukata tamaa ya mwanae kupona,  nusu saa baadaye aliponyanyuka uso wake ulikuwa umejaa tabasamu,  akapandisha tena kwenye gari na kumgusa Salome usoni, mwili wake wote ulikuwa wa baridi na damu ziliendelea kutiririka  na kuchafua  sakafu ya gari.
“Pole mama!” dereva aliongea.
“Katika hili napaswa kumwamini Mungu, kwa imani mwanangu  Salome atapona! Mungu ninayemwabudu ana nguvu, uwezo wangu umekomea hapa,  lakini ninapokomea mimi ndipo yeye anapoanzia!” aliongea mama huyo uso wake ukiwa umekunjuka kuliko alivyokuwa  kabla hajasali.
Baada ya kusema maneno hayo  mama huyo alilala kando ya mtoto wake na kumkumbatia akitarajia muujiza wa Mungu utokee. Akili yake ikamrudisha  nyumbani, akamkumbuka mumewe na namna alivyoondoka usiku kwa lengo la kwenda nyumbani kwa mkunga mama Mataluma lakini hakurejea tena! Hakuwa na jibu juu ya kitu gani kingempata lakini alikuwa na uhakika kutoka moyoni mwake lazima alipatwa na jambo baya,  alikuwa baba mzuri mno kukimbia tatizo la mtoto wake.
“Najua yuko tayari kufa kwa sababu ya mtu anayempenda,  iweje leo amkimbie Salome? Atakuwa amepata tatizo kubwa” aliwaza akiwa amemkumbatia mwanae.
***
“Hapa kuna mwinuko kidogo, tunaweza kutua kwenye huu uwanja!”
“Wewe tu, nakutegemea wewe rubani, ninachotaka mimi ni kumpata mke wangu!”
“Haya tulia, nashuka sasa. Umefunga mkanda?”
“Hapana!” aliitikia Gilbert
“Funga haraka!” Rubani aliamuru.
Gilbert alipotekeleza hilo,  Rubani  kwa taratibu  alianza kuishusha helkopta chini na kuikaribia ardhi, hatimaye ikatua kwenye uwanja ulionekana kuwa wa shule.  Kilikuwa ni kitu kigeni sana kwa helkopta kutua katika maeneo hayo, jambo lililofanya wanakijiji waanze kukimbia kutoka sehemu mbalimbali kuelekea uwanjani kwenda kuishangaa,  ndani ya  dakika kumi na tano tu tayari ilishazungukwa na wananchi  wakiishangilia na wengine kusogea karibu kuigusa.

“Habari  yako ndugu yangu?” Gilbert alimsalimia mzee mmoja aliyekuwa jirani yake.
“Nzuri tu habari za leo?”
“Salama!”
“Poleni na mafuriko!”
“Ahsante bwana,  vipi mmetuletea misaada?”
“Hapana,  mimi naitwa Gilbert, natokea Dar es Salaam, mwenzangu?”
“Naitwa Mwalimu Mchele, ndiye mkuu wa shule hii! Wewe Gilbert gani? Uliyemuoa Salome?”
“Unamfahamu?”
“Ah! Kuna mtu asiyemfahamu Salome huku?”
“Basi huyo ndiye mke wangu,  nimemfuata!”
“Nilisikia yuko kijijini kwao Kasheka, atakuwa hajaondoka kweli?”
“Ilikuwa tayari awe amekwishaondoka lakini mvua zikamfungia huku, bahati mbaya sana hivi sasa  anaumwa na yuko katika hatari ya kufa kwa sababu ya kuvuja damu nyingi! Naomba unisadie kufika kijijini kwao!”
“Hakuna shida, twendeni tu!”
“Ni umbali gani kutoka hapa?”
“Kilometa  ishirini na tano hivi!”
“Tunaweza kupata baiskeli?”
“Kwani hii helkopta yenu haiwezi kuruka na kutua kijijini kwao?”
“Hakuna sehemu ya kutua, kote kumejaa maji!”
“Basi twendeni kwa miguu maana baiskeli nina uhakika haitatusaidia chochote, barabara ni mbovu mno, tutafika tumeibeba”
“Sawa! Hata kama ni kukimbia tutafanya hivyo!”
Mwalimu Mchele  na kwenda nyumbani kwake kuaga na  wakaondoka hadi kijiji cha Bupandwa ambako pia walikuta daraja limejaa maji,  wakavushwa kwa mtumbwi hadi upande wa pili  wakaendelea kwa miguu,  sehemu zenye maji mengi wakivushwa mpaka wakaingia kijiji cha Kasheka wakiwa wamepita  njia ya mkato iliyokatisha  katika kijiji  cha Chamanyete. Wakiwa kijijini kwao na Salome walinyoosha moja kwa moja nyumbani kwao,  njiani wakakutana na watu wengi waliobeba maiti wakiongoza kwenda njia waliyokuwa wakienda wao.
“Poleni wazee!” Gilbert aliwaambia baada ya kusalimiana na baadhi yao.
“Ahsante, mzee wetu bwana hapa kijijini jana usiku alichukuliwa na maji ya mvua hadi mtoni ambako alizidi kuvutwa mpaka ziwani, akafa!”
“Aisee, bahati mbaya kwa kweli!” mwalimu Mchele aliingilia kati.
“Tena bahati mbaya sana kwake, binti yake mmoja  anayeishi Dar es Salaam pia ana hali mbaya kupita kiasi, usiku alianza kuvuja damu nyingi mzee akaondoka nyumbani kwenda kumtafuta mkunga, ndipo alipokutana na kifo cha…” mwanakijiji huyo hakumalizia sentensi yake, akashtuka  alipomwona Gilbert akiangua kilio.
“Masikini mzee……………………?”
“Unamfahamu?”
“Mkwe wangu,  huyo binti yake uliyemtaja ndiye mke wangu,  mimi naitwa Gilbert!”
“Aisee kumbe ni wewe, mimi naitwa Innocent, pole sana aisee!”
“Ahsante,  kwa hiyo mke wangu  yuko wapi?”
“Waliondoka asubuhi kwa machele hadi kijiji cha Mwangika ambako walikodisha Landrover  kuwapeleka Sengerema lakini taarifa nilizonazo ni kwamba hawajafika, huko mbele kuna daraja limevunjika, wapo hapo mpaka hivi ninavyoongea na wewe!”
Je, nini kitaendelea? Fuatilia siku ya Jumatatu

No comments

Powered by Blogger.