ad

ad

Brazil, Hispania kiama leo -Kombe la Mabara katika mechi ya fainali.

MABINGWA wa dunia, Hispania, leo wanakabiliwa na kibarua kigumu cha kuivua Brazil taji la Kombe la Mabara katika mechi ya fainali itakayochezwa usiku kwenye Uwanja wa Maracana, jijini hapa.

Timu hizo zinakutana zikiwa na rekodi tofauti, Hispania ikiwa bingwa wa dunia na Kombe la Ulaya, Brazil ni mabingwa wa kihistoria wa Kombe la Dunia wakijitwisha mara tano na mara tatu Kombe la Mabara, mwaka 1997,2005 na 2009.

Hiyo inazifanya timu hizo zishuke dimbani zikiwa na hofu kutokana na zote kucheza soka ya kiwango cha juu, ingawa Brazil inashika nafasi ya 22 kwa ubora wa soka duniani huku Hispania chini ya kocha wake Vicent del Bosque ikiwa nafasi ya kwanza.

Hispania wanashuka dimbani wakiwa na nguvu ya kutosha kupigania rekodi ya kuwa timu ya kwanza duniani kutwaa mataji manne makubwa mfululizo, baada ya kutwaa ubingwa wa Mataifa ya Ulaya ‘Euro 2008,’ Kombe la Dunia 2010 na Euro 2012.

Kwa Hispania, ni fainali ya kwanza baada ya mwaka 2009 kufungwa na Marekani mabao 2-0 katika hatua ya nusu fainali. Wafungaji walikuwa Jozy Altidore dakika ya 27 kabla ya Clint Dempsey kufunga la pili dakika ya 74.

Kipigo hicho kikaipeleka Hispania katika mechi ya mshindi wa tatu, ambapo walifanikiwa kuwafunga wenyeji Afrika Kusini mabao 3-2 katika muda wa nyongeza baada ya kumaliza dakika 90 kwa sare ya 2-2.

Wakati Hispania wakiwania rekodi hiyo, Brazil wanaingia Maracana wakitaka kutwaa taji la tatu mfululizo la michuano hiyo baada ya kutwaa miaka ya 2005 na 2009, ambalo litakuwa la nne katika historia ya nchi hiyo, baada ya awali kutwaa mwaka 1997.

Hispania inatoka kuifunga Italia kwa mikwaju ya penalti 7-6, katika nusu fainali, iliyoisha kwa sare ya 0-0 kwa dakika 120 za mpambano huo juzi, saa 24 baada ya Brazil kutangulia fainali kwa kuichapa Uruguay kwa 2-1.

Ingawa dunia inaishuhudia Hispania iliyoimarika katika miaka ya karibuni, Brazil wameonesha uimara mkubwa katika michuano hii na nyota wao wakiongozwa na Neymar, wana hamu ya kushinda wakiwa Maracana, dimba ambalo Brazil ilitwaa Kombe la Dunia mwaka 1970.

“Timu hizi zina historia na utamaduni mkubwa wa soka. Hispania wana nyota mahiri kikosini, hali kadhalika iko hivyo kwa Brazil,” amekaririwa akisema Neymar, muda mfupi baada ya Hispania kuitoa Italia na kuwafuata ‘Samba Boys’ fainali.
Hata hivyo, Neymar na wenzake wanakabiliwa na ukosoaji mkubwa kutoka kwa nguli wa zamani wa soka ya nchi hiyo na dunia, Pele, ambaye anadai kuwa kikosi cha sasa cha Brazil hakina ‘nguvu ya kutosha’ kuambulia kombe ama zawadi za daraja la juu.

Kocha wa Brazil, Luiz Felipe Scolari, amesema: “Hispania imeshinda kila kitu katika kipindi cha miaka mitano au sita iliyopita. Lakini sisi tutacheza katika aina yetu ya mchezo,” alisisitiza, huku akikana kuwabeza wapinzani wao baada ya kufuzu kwa mikwaju ya penalti.

“Wao walianzia katika mechi laini, hatua ya makundi ilikokuwa kundi moja na nchi dhaifu ya Tahiti. Sisi bado tunawaheshimu wao, lakini tutaonesha na kuthibitisha ubora wetu dimbani,” alisisitiza Scolari.

Wakati Brazil ilichomoka kutoka kundi A, ikizipiga kumbo Italia, Mexico na Japan, mpinzani wake Hispania, alitokea kundi B, akizipiku timu za Uruguay, Nigeria na Tahiti.
BBC Sport/Super
Powered by Blogger.