Yanga kulinda heshima ya ubingwa leo.
WAKIWA tayari na uhakika, mabingwa wa Ligi Kuu ya Vodacom msimu
2012/13 Yanga, wanashuka katika dimba la Taifa jijini Dar es Salaam leo
kuvaana na Coastal Union ya Tanga, ikiwa ni kati ya mechi nne za ligi
hiyo zitakazopigwa kwenye viwanja tofauti.
Yanga licha ya kuwa bingwa tayari, imedai itateremka katika dimba hilo
kuibuka na pointi tatu muhimu ili kulinda heshima na hadhi yao kama
vigogo vya soka hapa nchini na Afrika Mashariki na Kati.
Kiburi hicho cha Yanga kinatokana na maandalizi ya mwisho
waliyoyafanya wiki hii katika gym ya Quality Center pamoja na mazoezi
kwenye uwanja wa Shule ya Sekondari Loyola, Mabibo jijini Dar es Salaam.
Kwa mujibu wa Ofisa Habari wa klabu hiyo, Baraka Kiziguto, kikosi
kizima kipo fiti kwa ajili ya mechi mbili zilizosalia na kudai kuwa,
Salum Telela aliyekuwa anasumbuliwa na nyama za paja naye kajumuika na
wenzake.
Katika hatua nyingine, Ofisa Habari wa Shirikisho la Soka Tanzania
(TFF), Boniface Wambura, alisema mchezo huo namba 172 utachezeshwa na
mwamuzi Simon Mberwa kutoka Pwani akisaidiwa na Said Mnonga na Charles
Chambea wote wa Mtwara wakati mwamuzi wa mezani atakuwa Hashim Abdallah
wa Dar es Salaam na Kamishna David Lugenge kutoka Iringa.
Wambura alisema viingilio katika mechi hiyo itakayoanza saa 10:15
jioni ni sh 5,000 kwa viti vya rangi ya bluu na kijani, sh 8,000 rangi
ya chungwa, sh 15,000 kwa VIP C na B wakati VIP A itakuwa sh 20,000.
Mechi nyingine itakuwa ni kati ya Mtibwa Sugar na African Lyon
itakayochezeshwa na mwamuzi Dominic Nyamisana wa Dodoma kwenye Uwanja wa
Manungu ulioko Turiani mkoani Morogoro.
Nayo Kagera Sugar iliyo katika nafasi ya tatu kwenye msimamo wa ligi
hiyo itakuwa mgeni wa Polisi Morogoro kwenye Uwanja wa Jamhuri mjini
Morogoro huku Azam Complex Chamazi, maafande wa JKT Ruvu na Tanzania
Prisons watapigishana kwata, wakati Ruvu Shooting itakuwa nyumbani
kwenye uwanja wake Mabatini Mlandizi, Pwani kuwakabili ndugu zao Oljoro
JKT ya Arusha.
Post a Comment