Azam kuipa Yanga SC ubingwa wa Bara leo?.
INGAWA timu za soka za Azam na Coastal Union ya Tanga ndizo zinakumbana leo kwenye Uwanja
wa Mkwakwani jijini Tanga, matokeo ya mechi hiyo yanaweza kuipa Yanga ubingwa wa 24 tangu kuanza kwa ligi hiyo mwaka 1965.
Yanga inayoongoza ligi hiyo kwa pointi 56, inahitaji pointi moja tu
katika mechi mbili zilizosalia kabla ya kufungwa kwa pazia la ligi hiyo
iliyoanza Septemba 15, mwaka jana ikishindanisha timu 14.
Kwa vile uwezo wa Azam inayoifuatia kwenye msimamo wa ligi hiyo ni
pointi 56 kama itashinda mechi zake zote tatu zilizobaki ikiwemo ya leo,
sare tu katika mechi hiyo itatosha kuipa Yanga ubingwa bila kutoka
jasho.
Hiyo ni kutokana na mazingira kuwa kama Azam itatoka sare au kufungwa,
haitakuwa na ubavu wa kufikisha pointi 56 ambazo tayari zimefikiwa na
Yanga chini ya Kocha wake Ernis Brandts huku ikisaliwa na mechi mbili
dhidi ya Coastal Union na Simba.
Kama Azam itashinda katika mechi ya leo, Yanga italazimika kusubiri
majaliwa ya ubingwa kutoka kwa Coastal Union ambapo matokeo ya sare tu
yatatosha kuipa ubingwa.
Akizungumzia mechi ya leo, Stewart John Hall alisema jana kuwa kwa
maandalizi waliyofanya na ubora wa nyota wake, hawana sababu ya kufungwa
na kuwasihi wapenzi na mashabiki wao kujitokeza kwa wingi
kuwashangilia.
Hall alisema licha ya soka kuwa na matokeo ya kufungwa, kushinda au
sare, wao wamejiandaa kushinda kwani ingawa Yanga imebakisha pointi moja
kutwaa ubingwa wa ligi hiyo uliotemwa na Simba, lakini katika soka
lolote linaweza kutokea.
“Matokeo ya mechi ya kesho (leo) kila mtu anayapeleka kwa Yanga,
lakini mimi na vijana wangu tutajitahidi kushinda ili kuzidi kujiongeza
pointi hata kama hazitatosha kutupatia ubingwa, sio matokeo yetu yaipe
Yanga ubingwa kabla ya kwisha kwa ligi,” alisema Hall.
Katika hatua nyingine mechi kati ya Ruvu Shooting na Simba iliyokuwa
ichezwe jana Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam, imesogezwa hadi Mei 5
kutokana na uwanja huo kwa jana kutumiwa kwa maandalizi ya sherehe za
maadhimisho ya Mungano wa Tanganyika na Zanzibar.
Kwa mujibu wa Ofisa Habari wa Shirikisho la Soka Tanzania (TFF),
Boniface Wambura wanawaomba radhi wapenzi na mashabiki wa soka kwa
usumbufu uliojitokeza na kusema Jumapili ijayo Simba sasa watacheza na
Polisi Morogoro kwenye Uwanja wa Taifa jijini Dar es Salaam.
“TFF inawaomba radhi mashabiki kwa usumbufu uliojitokeza kutokana na
mabadiliko hayo ya ghafla,” alisema Wambura na kuongeza kuwa Simba
watashuka dimbani Jumapili kucheza na Polisi Morogoro katika Uwanja wa
Taifa.

Post a Comment