ad

ad

Rufaa zote zatupwa TFF..Malinzi, Nyamlani, Manji, Wambura wapeta


KAMATI ya Uchaguzi ya Shirikisho la Soka Tanzania (TFF), jana ilitoa matokeo ya pingamizi zilizowasilishwa dhidi ya wagombea kwenye Uchaguzi Mkuu wa Shirikisho hilo na Bodi ya Ligi Kuu huku wagombea wote waliopingwa wakipeta.
Ikitumia kanuni za uchaguzi ibara ya 11(4), kamati hiyo iliyokutana Januari 30 ilipitia pingamizi hizo zilizowasilishwa kwao na wadau mbalimbali wa soka ambapo siku hiyo walitakiwa kuzitetea hoja zao kwa vielelezo kama ilivyokuwa kwa watuhumiwa.

Jamal Malinzi aliyekuwa akipingwa na Agape Fue kuwania nafasi ya urais kwa madai ya kuvunja katiba kwa kufanya juhudi za kukwamisha juhudi za shirikisho hilo kuitaka mikoa kuridhia mabadiliko ya katiba kwa waraka kutekeleza agizo la Shirikisho la Soka Afrika (Caf) na Kimataifa (Fifa), ameshinda.

Fue pia alidai Malinzi hana sifa ya uzoefu wa miaka mitano katika uongozi wa soka, pia amekosa.
Pingamizi kuhusu uadilifu na haiba ya kuliwakilisha shirikisho hilo kimataifa, zote hizo mbili zimetupiliwa mbali kutokana na mpingaji kushindwa kutokea kuthibitisha madai yake.

Kwa mujibu wa taarifa ya shirikisho hilo iliyosainiwa na Katibu Mkuu wake, Angetile Osiah, mgombea mwingine wa nafasi hiyo Athuman Nyamlani aliyekuwa akipingwa na watu wawili: Mintanga Yusuph Gacha na Medard Justinian, pia ameshinda tuhuma dhidi yake.
Tuhuma zilizokuwa zikimkabili Nyamlani ni kwamba kwa vile ni Hakimu Mkazi wa Mahakama ya Tanzania, hivyo anakosa kigezo na sifa ya kugombea nafasi hiyo kwa mujibu wa Judicial Service Act, Public Service Act 2002 na Code of Conduct for Judicial Officers of Tanzania.

Hoja nyingine za kumpinga Nyamlani ni kuwa akiwa rais wa TFF kutakuwa na mgoganao wa kimaslahi pia alikosa umakini na uadilifu kwa kushindwa kutimiza vema wajibu wake hadi akaunti ya shirikisho hilo kufungiwa na Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA).
Vilevile kamati hiyo imetupa pingamizi dhidi ya Michael Wambura aliyekuwa akipingwa kuwania nafasi ya Makamu wa Rais wa Shirikisho hilo na wadau Saidi Rubea na Josea Samuel Msengi kwa tuhuma mbalimbali.
Wakati Msengi akiondoa pingamizi lake, tuhuma za Rubea hazikukidhi matakwa ya Kanuni za Uchaguzi za TFF Ibara ya 11(2), hivyo anabaki kupambana na Nasib Ramadhan na Wallace Karia.

Kamati ya Uchaguzi imetupilia mbali tuhuma hizo baada ya Mintanga Yusuph Gacha kushindwa kutokea kutetea pingamizi huku Medard Justinian akishindwa kuithibitishia kamati kuwa alikuwa na ufahamu wa kutosha wa pingamizi lake ikiwemo viambatanisho vyake, hali iliyoonyesha kuwa pingamizi lilikuwa la hila na udanganyifu.
Kwa upande wa wagombea ujumbe wa Kamati ya Utendaji waliokuwa wakipingwa, Athuman Kambi, Eliud Mvela, Epaphra Swai, Vedastus Lufano na Mugisha Galibona, pia zote zimetupiliwa mbali kwa kukosa nguvu kwa mujibu wa kanuni za uchaguzi.

Aidha kamati hiyo imetupa pingamizi dhidi ya Yusuf Manji anayewania nafasi ya uenyekiti wa Bodi ya Ligi Kuu iliyokuwa imewekwa na wadau Daniel Kamna na Juma Magoma, kwamba hana uzoefu wa miaka mitano, pia hajawahi kucheza soka au kuwa kocha, mwamuzi au kushiriki uendeshaji ngazi ya mkoa au Ligi Daraja la Kwanza.
Kamati hiyo imetupa pia pingamizi dhidi ya Saidi Muhamed anayeomba nafasi ya Makamu wa Bodi ya Ligi iliyowekwa na Frank Mchaki kwamba si Mwenyekiti wa Azam, hivyo anakosa sifa, pia ameandika maelezo ya uongo kwenye fomu.

Madai hayo yametupwa kwa kutokidhi matakwa Kanuni za Uchaguzi za TFF Ibara ya 11(2) kwani haikuambatanishwa na vielelezo kuthibitisha maelezo ya pingamizi.
Pingamizi nyingine iliyotupwa ni dhidi ya Hamad Yahya Juma anayeomba kugombea nafasi ya Mwenyekiti wa Bodi ya Ligi, aliyekuwa akipingwa na Mchaki kwamba si Mwenyekiti wa Klabu ya Mtibwa, hivyo hana sifa.
Uchaguzi Mkuu wa Shirikisho hilo umepangwa kufanyika Februari 24, ukitanguliwa na ule wa Bodi ya Ligi Kuu utakaofanyika Februari 22.
Powered by Blogger.