ad

ad

Singidani (A Story From My Heart) - 23



 

ILIPOISHIA...
Bibi alipowaona, alionekana kuukunja uso wake. Hata Chris alipojaribu kutabasamu, bado bibi aliendelea kukunja uso wake.
SASA ENDELEA...
HAKUaliyejua kilichokuwa moyoni mwa bibi, hakuwa ameukunja uso wake kwa hasira. Uso ulikunjamana kwa mshangao wa kumuona mjukuu wake sasa alifikia uamuzi sahihi wa kuachana na ukapera.
Chris na baba yake mdogo walipiga hatua za taratibu kumfuata bibi. Shamakala alikaa pembeni, bibi akawasogelea, wakakutana katikati. Alichokifanya bibi ilikuwa ni kuinama kidogo.
Haraka Shamakala akamwonyesha Laura ishara kuwa apige magoti chini. Akafanya hivyo. Bibi akamshika mkono Chris. Akatema mate kidogo mkononi mwake kisha akampaka Chris usoni.
Akamsogelea Laura, akamshika mikono yote miwili na kumwonyesha ishara asimame. Akafanya hivyo; akamvutia kwake na kumkumbatia, kisha akamtemea mate kidogo kwenye paji lake la uso.
Laura akatabasamu!
Kwao ilikuwa heshima kubwa sana, kutemewa mate na bibi, ilimaanisha baraka na kukubalika katika familia. Bibi akamshika mkono na kumwongoza hadi sebuleni, kwenye nyumba ile ya zamani ya tembe.
“Karibu sana mjukuu wangu,” bibi akamkaribisha Laura.
“Ahsante bibi.”
Tayari kifungua kinywa kilikuwa kimeshaandaliwa na mke wa Shamakala. Chai ilitengwa na vitafunwa vya maboga na mahindi ya kuchemsha. Wakaketi kwenye jamvi na kuanza kula. Wanaume walikula nje, wanawake ndani.
Ilikuwa siku mpya kwa Chris. Siku ya utambulisho wa ‘Laura wa Kijijini!’. Ukweli wa mambo ulijulikana na Laura, Chris na Shamakala pekee.
***
Moto ulikuwa unawaka huku moshi  ukitoka. Ulikuwa usiku wa mbalamwezi. Watu wawili walikuwa wameuzunguka moto uliowashwa kwa kutumia kinyesi cha ngo’mbe. Ndani ya moto huo kulikuwa na karanga zikichomwa.
Kazi yao ilikuwa ni kuchomoa na kuendelea kula taratibu. Hapakuwa na mazungumzo. Muda kidogo bibi alifika.
“Hivi huyu msichana ni wa hapa Mkalama kweli?” bibi akamwuliza Chris.
“Hapana bibi. Ni kutoka Mpambala kama tulivyokuambia,” Chris akajibu.
“Lakini mbona hafahamu kinyumbani?”
“Bibi hajakulia hapa, wazazi wake walihamia Mwanza muda mrefu sana, tangu akiwa mdogo, amesomea huko na sasa hivi anamalizia masomo yake Singida Mjini ndiyo maana hajui vizuri kinyumbani. Ni kama mimi tu.”
“Hapo sawa.”
“Vipi lakini bibi, umegundua tatizo lolote kutoka kwake?”
“Tatizo? Hapana... ni msichana mzuri sana, mchapakazi na anayejua kujituma. Hana tatizo kabisa. Naweza kusema kwamba, mjukumuu wangu pale umepata mke sahihi.”
“Ahsante sana bibi.”
“Sasa lini mipango yako?”
“Bado kidogo, nasubiri amalizie masomo yake tu. Amebakiza miezi sita. Hatutakuwa na muda wa kusubiri zaidi. Akimaliza kinachofuata ni ndoa.”
“Sawa. Nyie endeleeni kuota moto lakini chakula kipo tayari, sasa hivi kinakuja.”
“Sawa bibi.”
***
Siku tatu zilitosha kabisa kwa Laura kuthibitishwa kuwa mke mtarajiwa wa Chris. Bibi alishatoa baraka zote. Ilikuwa furaha kubwa sana kwao. Waliagana wakiwa wenye furaha sana.
“Karibu kwenye ukoo wetu mjukuu wangu, hakuna atakayepinga uamuzi huu. Hata kama nikifika leo, kabla ya ndoa yenu, watu wote wanaonihusu watambue kuwa nimeridhia ndoa yenu,” akasema bibi.
“Ahsante sana bibi, nimefurahi sana kusikia hivyo,” Chris akasema.
Chris na Laura wakaondoka. Walikwenda hadi kituoni ambapo walichukua pikipiki iliyowapeleka moja kwa moja hadi mji mdogo wa Ibaga. Walifikia kwenye gesti ileile, Sayuni.
Walipoingia tu chumbani, wote walikumbatiana kwa furaha ya ushindi. Laura machozi yalimtoka kama maji yanavyotiririka kwenye mfereji uliopo bondeni.
“Tulia mpenzi, najua ni kiasi gani una furaha moyoni mwako. Ni furaha yetu sote na ni haki yetu kufurahi,” akasema Chris.
“Sikutegemea kama mambo yangeisha kwa wepesi kiasi hiki.”
“Najua lakini usijali. Sasa tumebakiza eneo moja tu. Nyumbani kwenu. Lazima hili jambo lijulikane mpenzi wangu kama kweli tuna lengo la kuoana. Kuna kitu lazima kifanyike mpenzi.”
“Ni kweli baba, nakuamini kwa mawazo yako, tunaanzia wapi?”
“Nashauri tukitoka hapa, wewe usikae kabisa mjini, nenda moja kwa moja Mwanza, kazungumze na wazazi wako kuhusu hili suala ili nao pia wawe wanajua.
Maadamu tunapendana na bibi amesharidhia, naamini ni jambo jepesi sana kumhadaa mzee Shila!”
“Kweli dear?”“Kabisa!”“Sawa.”
Ikawa asubuhi nyingine yenye kupendeza zaidi. Furaha yao haikubaki mioyoni mwao pekee, ilitoa msukumo mkali na kuchemsha damu za miili yao. Wote wakawaka!
Walijua namna ya kukitumia chumba kile vizuri kabisa!
Usikose
Powered by Blogger.