ad

ad

Lowassa ataja vipaumbe vyake 13 ndani ya siku 100

Mgombea urais aliyesimamishwa na Umoja wa Katiba ya Wananchi (Ukawa) kupitia Chadema, Edward Lowassa, ametaja vipaumbele vyake 13 ambavyo atavitekeleza ndani ya siku 100 akichaguliwa kuwa Rais wa Tanzania Oktoba 25, mwaka huu.
 
Lowassa alitaja vipaumbele hivyo wakati akizungumza katika mikutano mbalimbali ya kampeni jijini Dar es Salaam jana.
 
Alivitaja vipaumbele atakavyovitekeleza ndani ya siku 100 kuwa ni, upatikanaji wa dawa na vifaa vya uzazi kwa kina mama, umeme wa uhakika nchi nzima, kupunguza foleni jijini Dar es Salaam, kuondoa kero kwa wafanyabiashara wadogo wadogo na bodaboda na kutengeneza mkakati wa kumaliza tatizo la maji nchini ikiwamo Dar es Salaam.
 
Vingine ni kutengeneza mfumo bora na rafiki wa wafanyabiashara wakubwa na wadogo, kufuta ada na michango kwa wanafunzi, kupunguza kodi ya mshahara kwa wafanyakazi, kufuta kodi zote za mazao ya wakulima, mkakati kabambe wa kukuza michezo na sanaa, kuunda tume ya kutatua migogoro ya wafugaji na wakulima, kuanzisha kituo kila wilaya kwa ajili ya kutoa huduma za serikali na kuboresha maslahi ya polisi, wanajeshi na walimu.
 
Aidha, Lowassa alisema akichaguliwa kuingia Ikulu, kuanzia Januari, mwakani hakuna Mtanzania atakayelipa ada ya shule wala mchango wa aina yoyote.
 
Alisema zipo fedha nyingi na za kutosha kwa ajili ya kuwasomesha Watanzania bure na kwamba akiingia Ikulu pia atafuta utaratibu wa serikali kununua magari ya kifahari ili fedha hizo zitumike kuboresha elimu nchini.
 
Kuhusu kuondoa umaskini, Lowassa alisema anauchukia, hivyo atahakikisha anauondoa na kuwataka vijana kuhakikisha wanampigia kura ili kumuingiza ikulu Oktoba 25, mwaka huu.
CHANZO: NIPASHE
Powered by Blogger.