Udini wamkera Kinana.
KATIBU Mkuu wa CCM,Abdulrahman Kinana amekerwa na chokochoko za
kidini zilizoanza kujipenyeza hivi karibuhi na kutoa wito kwa madhehebu
ya dini na taasisi zake hapa nchini,kuendelea kuhubiri amani kwa
kuliombea taifa , ili wananchi waendelee kujivunia amani iliyoachwa na
Baba wa Taifa Mwalimu Julius Nyerere.
Kinana alisema kuwa upo umuhimu mkubwa kwa viongozi wa dini na taasisi zake kuendelea kuienzi amani kwa kuhubiri suala la kudumisha amani na kuonya kwamba Serikali haitasita kuchukua hatua za haraka kwa mtu ama kikundi chochote cha dini kitakachojihusisha na uvunjivu wa amani.
Alisema pamoja na changamoto zinazojitokeza hivi sasa kwa baadhi ya dini kukashifu dini zingine ,Serikali ipo macho kuhakikisha kwamba inadhibiti hali yoyote ya ukiukwaji wa maadili ya kidini nakusisitiza kwamba dini zote nchini ziendeshe shughuli zake kwa kuheshimiana.
‘’Usidharau imani ama itikadi ya mtu mwingine lazima dini ziendeshwe kwa maadili na sio kiholela,kama hupendi kubaguliwa kwa dini usiwe mwepesi kubagua dini ya mwingine’’alisema Kinana. Alisisitiza kwa kuyataka madhehebu ya dini kuiga mfano wa kujenga ushirikiano na mshikamano katika kutangaza neno la Mungu na kuepuka mifarakano inayoweza kuwagawa watanzania kiimani,na kuwataka viongozi wa dini kuwa wa kwanza kukemea hali hiyo.
Kwa upande wa Mwenyekiti wa Jumuiya ya Khoja Shia, Gulam Hussen alisema kuwa lengo la maadhimisho hayo ni kuendelea kukumbuka mazuri yote aliyokuwa akiyafanya Mtume Muhammad kwa lengo la kukumbushana na kuyaenzi.
Alisema maadhimisho yao yaliyotambulika kwa jina
la ‘Hussein Day’yanalenga kujenga undugu ,kufahamiana na kupinga ufisadi
unaolinyemelea taifa kwa baadhi ya viongozi wenye tamaa ya
kujilimbikizia mali.
Aliitaka jamii ijifunze kuishi maisha ya kitume huku ikijali haki na usawa duniani na kuepusha migogoro ya kidini ambayo haina tija ,aliwataka waislamu wajifunze kuishi kwa upendo.Naye mkuu wa wilaya ya Monduli, Jowika Kasunga aliyekuwa amemwakilisha mkuu wa mkoa wa Arusha, Magesa Mulongo,alisema serikali inatambua mchango wa madhehebu ya dini katika kuboresha huduma za maendeleo kwa wananchi.
Alizitaka dini zote hapa nchini ziendelee
kudumisha amani na kudai kuwa iwapo amani itaachwa ichezewe ,gharama za
kuirudisha ni kubwa sana hatua ambayo inaweza kusababisha machafuko na
vifo .
Alisema kuwa tayari serikali imepata taarifa kuwa wapo watu ambao wamekuwa wakijipenyeza kwa ajili ya kuvuruga amani kwa kutumia mgongo wa dini ,na kusema kuwa imejipanga kuhakikisha kuwa kila mwananchi ana uhuru wa kuabudu popote bila kubughudhiwa na kwamba itakabiliana na wenye nia ya kuleta chokochoko za kidini.
CHANZO MWANANCHI
Post a Comment