ad

ad

Amber Lulu Acha Uchafu wa Mapicha, Fanya Muziki

                Lulu Auggen ‘Amber Lulu’.
NIANZE kumsh-ukuru Mungu kwa kila jambo katika maisha yangu na yako msomaji wa Barua Nzito, hasa baada ya kumaliza wiki ngumu na ya majonzi kwa Watanzania wote kupatwa na msiba mkubwa wa kufiwa na wanafunzi 32 kwa wakati mmoja.
Kama mwanajamii, nina kila sababu ya kutoa maoni yangu kwa jamii na wanajamii wenyewe katika kushauri juu ya mazuri au mabaya wanayofanya. Leo hii nimeandika waraka maalumu kwa rafiki na dada yangu mpendwa, Lulu Auggen ‘Amber Lulu’ aliyeanza kutambulika kwenye baadhi ya video za wasanii wa Bongo Fleva kama ‘video queen’ ikiwemo Usimsahau Mchizi ya R.O.M.A, Inde ya Dully Sykes na nyingine kibao.


Kama ilivyo kawaida maisha ni kupanda na kuongeza kitu kila kukicha, nashukuru rafiki yangu, Amber Lulu ameongeza wasifu mwingine wa kuwa msanii wa Bongo Fleva, tayari ameachia ngoma ya Watakoma aliyomshirikisha mkali wa kurap, Country Boy. Inafanya vizuri, imepenya, ni ngoma ambayo inachezeka na kama unapenda kuicheza na hata ukitembelea baadhi ya kumbi za starehe utasikia inachezwa.


Simzungumzii Amber Lulu kwa kujifananisha na Amber Rose wa Marekani, simzungumzii kwa kufanana kiana na kuiga mtindo wake wa nywele, ‘kujibinua’ kama wanavyofanya watoto wa mjini kwa sasa, kwa sababu kuiga mtu si vibaya kama utaiga mazuri yake, ila ukiiga mabaya basi utaonekana wa ajabu sana.
Kiukweli Amber unakera dada yangu kwa tabia yako ya kupiga picha za ajabu, juzikati nimeona picha ambayo umechuchumaa mbele ya mwanaume kama unafungua sehemu ya zipu yake vile. Nikiwa bado natafakari kuhusu picha hiyo, ghafla naona picha nyingine ukiwa umemshika sehemu nyeti mwanamke mwenzako.
Nini tafsiri ya picha hizi mbili? Umelenga kufikisha ujumbe gani kwa jamii? Kwamba unashiriki mapenzi ya jinsia moja au umepinda kupindukia, au ndiyo ‘kitu cha Arusha’ kinafanya kazi yake.

Najaribu kuvaa uhusika wa mimi kama baba, kaka au ndugu yako wa kiume halafu naona picha zako za utupu mitandaoni unadhani nitajisikiaje, nitawaza nini juu yako?
Hivi Amber kama una wazazi wako unahisi unawaweka kwenye wakati gani huko wanakoishi, mbaya zaidi picha zilizoko mitandaoni si kwamba zimepigwa kwa kuibia au bahati mbaya la hasha, si kweli kwamba zimepostiwa na wabaya wako kwa kusudi la kukuchafua ni picha ulizojiandaa kwa pozi za uchafu huo kisha ukaziposti mitandaoni.
Waswahili wanasema akili za kuambiwa changanya na za kujiongeza, Amber umekuwa ukifanya mambo ya ajabu kwa sababu ya kumuiga ‘role model’ wako, Amber Rose wa Marekani, lakini unasahau kuwa Afrika na Marekani ni vitu viwili tofauti, kuna mambo yakifanyika kule au kwingineko huonekani wa ajabu lakini mambo hayohayo ukiyafanya kwetu unaonekana ni mwendawazimu.


Rafiki yangu mbona unajiabisha hivyo, kwa nini usijikite zaidi kwenye kufanya muziki kuliko kupiga picha za uchafu na kutupia mitandaoni.
Nakukubali sana kwenye muziki lakini kwenye mapicha ya uchafu siko nawe, nikisema nakukubali namaanisha na hata siku za nyuma niliandika makala inayosema

VITA YA WAUZA SURA WA KIBONGO, ndani ya makala hayo nilizungumzia vita yako na Gigy Money na Lulu Diva kuanzia kwenye video queen hadi kuwa wanamuziki na nikachambua kuwa mtu ambaye nyota yake inaonekana kung’ara kwenye muziki ni wewe, sina nia mbaya ya kukupaka matope lakini kwa hili la mapicha ya ajabu acha tu nikupake.

Mapicha picha hayo si tu nimeyaona mtandaoni lakini hata maisha yako ya kawaida yamejaa ulimbukeni fulani hivi. Nakumbuka hata kwenye bethidei yako iliyofanyika Bunju nje kidogo ya Jiji la Dar ulikata mauno ya ajabu kwa kushika meza na kufanya kila aina ya mbwembwe.
Sikatazi usicheze ila cheza kwa staha, unachokifanya ni ushamba, ulimbukeni, ni kushindwa kufikiria nje ya boksi kuwa kuna maisha nje ya sanaa ya mapichapicha machafu.


Nilibahatika pia kusikilia mahojiano yako na kituo kimoja cha redio, Amber hata watangazaji waliokuhoji walikuambia kuwa kati ya video queen walioachia ngoma zao ni wewe tu ndiyo unaonekana kung’ara na una nafasi kubwa ya kutoboa kwenye muziki.
Ulikazia kile walichosema kuwa unashukuru Mungu kwa sababu umekuwa ukiongozana na baadhi ya mastaa wakubwa kwenye shoo zao za mikoani, hilo linajidhihirisha kwako kuwa nyota njema imeonekana asubuhi.
Kwa nini rafiki yangu usitumie nyota iliyong’ara kuing’arisha zaidi kuliko kupigania kufifisha bila kujua kama unaififisha?


Amber nakupenda ndiyo maana nakwambia lakini kwa kuwa umeshavurugwa na ukakubali kuvurugika si rahisi kunielewa lakini naamini siku zijazo utanilewa tu.
Kama kaka na rafiki yako nakushauri, kaa chini ujitafakari upya, achana na maisha ya mtandaoni, fanya muziki, jikite zaidi kwenye kuimba, unaweza rafiki yangu au unasubiri hadi msemo wa kusikia kwa kenge atokwe damu masikioni?



CHANZO: RISASI JUMATANO

No comments

Powered by Blogger.