ad

ad

Singidani (A Story From My Heart) - 13



UKIMYA wa Dk. Chris ukamshangaza sana baba yake, akajiuliza kichwani mwake; iweje ashindwe kujibu swali hilo wakati mwanzo alimhakikishia kuwa ameshapata mchumba?
“Chris....” akaita mzee Shila.
“Naam baba.”
“Nataka kujua nilichokuuliza.”
“Baba nimeshakuambia  nimeshampata mchumba.”
“Sawa, vipi kuhusu mipango ya ndoa?”
“Inahitaji muda kidogo baba.”
“Kwanini?”
“Kila kitu nimemwachia baba mdogo Shamakala. Yeye ndiye anayefuatilia kila kitu.”
“Huyo msichana ni wa wapi?”
“Ni wa Kijiji cha Chemchem baba. Wao wanaishi Mpambala.”
“Anaitwa nani?”
“Njile.”
“Njile?”
“Ndiyo baba, Njile.”
“Nitawasiliana naye, tena hivi karibuni nina safari ya kwenda nyumbani. Nitazungumza na baba yako mdogo vizuri.”
“Sawa baba.”
“Ulimjuaje?”
“Nilizungumza na baba mdogo kuhusu hilo suala, yeye ndiye aliyenipeleka kuonana na huyo binti. Anasema anamjua vizuri na ana tabia nzuri.”
“Sawa. Si unalala hapa nyumbani leo?”
“Hapana baba, lazima nirudi nyumbani. Nilikuwa nakusubiri tu wewe hapa muda wote.”
“Hapana, pumzika, utakwenda kesho.”
“Baba nina ratiba nyingi sana, naogopa nitashindwa kwenda na wakati. Kuna baadhi ya mambo lazima niyashughulikie usiku huu.”
“Kama nini?”
“Nina mikataba ya watu tayari. Lazima nikatulie usiku huu, nipitie script maana kesho nahitajika kurekodi.”
“Unaona sasa? Umeshaanza mambo yako ya filamu!”
“Siyo hivyo baba.”
Maneno yaliyofuata hapo hayakuwa ya kupendeza. Kama kawaida, mzee Shila alimlaumu mwanaye kwa tabia yake ya kupenda sanaa badala ya taaluma yake ya udaktari aliyomsomesha kwa fedha nyingi.
Dk. Chris alijitahidi kuzungumza na baba yake lakini hakuelewa, mwisho wake Chris aliondoka bila kuwa na maelewano mazuri na baba yake.
***
Dk. Chris alitoka na kuchukua gari moja linalotumiwa na mama yake, akaingia na kuondoka zake. Kutoka Mbezi Beach hadi Kijitonyama anapoishi kwa usiku huo, asingetumia muda mrefu sana.
Barabara nzima hapakuwa na foleni kabisa. Akiwa anakaribia mataa ya Mwenge, simu yake ikaita. Alipoangalia kwenye kioo cha simu, akakutana na jina la Ramsey, msanii mwenzake.
Tayari alikuwa ameshafika kwenye mataa ya Mwenge kabisa, mbele yake kukiwa na magari manne tu yanayonyoosha kuelekea Barabara ya Ali Hassan Mwinyi. Hapo ni kwenye makutano ya Barabara ya Bagamoyo, Coca-Cola, Sam Nujoma na Ali Hassan Mwinyi.
Mara moja akapokea!
“Kaka vipi, umeshaingia mjini?”
“Ndiyo kaka, leo jioni.”
“Uko wapi?”
“Natokea home kwa mdingi, naenda mara moja hospitali  halafu narudi nyumbani kwangu.”
“Hatuwezi kuonana mzee?”
“Wapi sasa?”
“Mimi nipo nyumbani lakini najiandaa kutoka kwenda Mzalendo Pub.”
“Nusu saa nitakuwa hapo.”
“Poa.”
Tayari taa nyekundu ilizima, ikawaka ya njano kwa sekunde mbili kisha kijani ikaachia. Magari yakaanza kutembea. Dk. Chris alinyoosha moja kwa moja hadi alipopita kwenye makutano ya Barabara ya Ali Hassan Mwinyi na Shekilango, akaifuata barabara hiyo mpaka alipokutana na mataa ya Morocco, akakata kulia.
Alishika Barabara ya Kawawa hadi Biafra alipokata kulia kwenye muunganiko wa mtaa unaoelekea Kinondoni - Kanisani, akaegesha nje ya Hospitali ya Kinondoni alipokuwa akifanya kazi.
Alifikia ofisini kwake, Sista  Sandra akaingia na  kusalimiana naye. Dk. Chris alitaka kujua hali ya ofisi ilivyo kwa siku ambazo hakuwepo ofisini.
“Vipi mkuu hajaniulizia sana?”
“Hapana, siku mbili hizi hapakuwa na mishe sana. Hata oparesheni zilikuwa chache.”
“Aisee, poa basi. Nimepita mara moja, kesho asubuhi nitaamkia hapa. Naingia na nani?”
“Utakuwa na Dk. Masanja na Dk. Kileo... wewe umepangwa na Sista Jenifer.”
“Sawa, endelea na kazi.”
“Ahsante dokta.”
Dk. Chris alipitia mafaili kadhaa pale mezani kwake, kisha akaweka ratiba yake ya siku inayofuata, akaondoka zake kuelekea Mzalendo Pub. Alikuwa akimfuata msanii mwenzake Ramsey.
Itaendelea.

Powered by Blogger.