ad

ad

She is too young to die- 5




Mke wa kijana mwenye mafanikio, Salome  ambaye  ni mjamzito amekwama kijijini kwao  sababu ya mafuriko! Damu nyingi zinamtoka na amepoteza fahamu,  mume wake ameamua kukodisha helkopta kutoka Dar es Salaam hadi kijijini kwao Kahunda lakini anamkuta amekwishaondoka kwa Landrover ambayo pia anataarifiwa imeshindwa kuvuka mto sababu daraja limevunjika. Je, atafanikiwa kumpata na kumwokoa? SONGA NAYO…

Gilbert hakuweza hata kusubiri mazishi ya mkwe wake mzee Magoma,  alichoomba ni kuonyeshwa  mwili wa marehemu ili atoe heshima zake za mwisho kwa sababu mzee huyo alipoteza  uhai wake kwa ajili ya mke wake, wanakijiji wakamfanyia kama alivyoomba na baada ya hapo akiongozana na  mzee Mchele walitembea tena mpaka kijiji cha  Bupandwamhela shuleni walikoiacha helkopta, wakakuta wanakijiji wengi zaidi  wamekusanyika kuishangaa! Gilbert akamsimulia Rubani juu ya yote aliyoyakuta kijijini na kumwomba  waruke mpaka eneo ambalo  mke wake alidaiwa kuwepo, hakuwa na uhakika kama angemkuta hai lakini  angalau afanye jambo Fulani, wakati akiongea machozi yalimtoka Gilbert kama mtoto mdogo, ndani ya moyo alijihukumu kwa kumruhusu Salome kuja maeneo hayo wakati alikuwa mjamzito.
“Lakini sikujua…hata yeye aling’ang’ania sana kumbe ndio kifo kilikuwa kinamwita!” Aliwaza moyoni mwake akipanda ndani ya helkopta pamoja na mzee Mchele aliyejitolea kuwaelekeza mahali daraja lilipokuwa.
Wakaruka juu kama  mita mia  tano hivi na kuanza  kuelekea  mbele wakipita juu ya vijiji vya Bupandwa,  Kafunzo  macho yao yakiwa yameangalia chini,  mzee Mchele akiwaelekeza na hatimaye wakafika  kwenye mto wenye daraja lililovunjika, hapo ndipo  wakaiona gari aina ya Landrover ikiwa imeegesha barabarani  hatua chache tu kutoka kwenye mto uliopita maji mengi. Upande wa pili pia kulikuwa na magari mengi yaliyokuwa yameshindwa kuvuka mto.
“Nafikiri ni wale!” mwalimu Mchele aliongea.
“Hapo ndio kwenye daraja?”
“Hapa ndio Bilulumo, daraja limekwenda na maji!”
“Sasa?” rubani aliuliza.
“Anza kushuka,  tutamchukuaje kama kweli hiyo ndiyo gari yenyewe maana hakuna sehemu ya kutua?”
“Tutatumia kamba, nitakufunga wewe halafu utashuka hadi chini ambako  utambeba kisha nitakuvuta tena kuja juu kwa kutumia mashine, sawa?”
“Hakuna shida!”
“Haya sogea hapa  karibu!” rubanin alisema na  Gilbert akatii kisha kumwelekeza mahali kulikokuwa na kamba,  akamwamuru aifunge kiunoni na kumwelekeza namna ya  kushuka na kuteremka hadi chini, baada ya hapo alianza kuiteremsha helkopta chini mpaka umbali wa kama mita mia kutoka ardhini.
“Ni mwenyewe, ni mke wangu! Amelala ndani ya gari,  anaonekana amekufa…!”
“Jikaze Gilbert, shuka sasa!” Rubani alisema baada ya mlango kufunguka na Gilbert akaruka na kuanza kushushwa kwa kamba hadi chini ambako aliingia ndani ya Landrover na kumkuta mama mkwe wake amelala kando ya Salome, akamwamsha na kumwamkia huku akimgusa Salome kifuani, moyo ulikuwa bado unapiga ingawa alikuwa amelala katikati ya mabonge ya damu.
“Pole mama!”
“Ahsante!”
“Tunaondoka naye kwenda hospitali!”
“Hakuna shida baba! Mimi?”
“Wacha kwanza nimpandishe yeye,  halafu nikifika juu nitaongea na Rubani!”
Gilbert alichukua mkanda aliopewa na Rubani, akajifunga kifuani na pia kuufunga kifuani kwa mkewe ukipita chini ya   kwapa zake, alipomaliza alionyesha ishara juu na mkanda ukaanza kumvuta taratibu mpaka ndani ya helkopta ambako alifungua mkanda na kumlaza mke wake chini.
“Salome!Salome!Salome!” akaita mara  nyingi bila kuitikiwa.
“Tuondoke?” Rubani aliuliza.
“Mama mke wangu pia anataka kuondoka na sisi!”
“Haya shusha kamba!”
Gilbert akafanya hivyo kisha kushuka hadi chini ambako alimkuta mama yake Salome akimsubiri,  akauchukua mkanda tayari kujifunga pamoja na mama mkwe wake, ghafla alimwona mama mkwe akishtuka na kurudi nyuma. Gilbert akashindwa kuelewa ni kitu gani kilikuwa kimetokea.
“Vipi mama?”
“Baba wewe ni mkwe wangu tukumbatiane?”
“Mama tuko kwenye hali ya hatari!”
“Mh! Ni mwiko!”
Je, nini kiliendelea? Fuatilia

No comments

Powered by Blogger.