NCHAMBI ATAKA MAWAZIRI MIZIGO WATOSWE
MBUNGE wa Kishapu, Suleiman Nchambi, ameungana na Katibu wa Itikadi
na Uenezi wa Chama cha Mapinduzi (CCM), Nape Nnauye, kumtaka Rais Jakaya
Kikwete awatimue mawaziri mizigo ambao wameshindwa kutimiza majukumu
yao.
Nchambi (CCM), alisema anakusudia
kwenda kumuona Rais Jakaya Kikwete kulalamikia uzembe wa Waziri wa
Kilimo, Chakula na Ushirika, Christopher Chiza, kwa jinsi alivyoshindwa
kutatua kero ya wakulima katika jimbo la Kishapu.
Mawaziri wengine wanaolalamikiwa na kupendekezwa watimuliwe, wamo
Naibu Waziri wa Kilimo, Chakula na Ushirika, Adam Malima, Waziri wa
Fedha na Uchumi, William Mgimwa, na Waziri wa Elimu na Mafunzo ya
Ufundi, Dk. Shukuru Kawambwa.
“Mimi naungana na Nape na Kinana kwamba Chiza hafai, hajatembelea
maeneo ya kilimo, wizara haitendi haki na kama ni mzalendo anapaswa
kujiuzulu mwenyewe maana kama nguo hazikutoshi, vua mwenyewe,” alisema
Nchambi.
Alisema amewahi kumuomba Waziri Chiza aende Kishapu akashuhudie na
kuyatafutia ufumbuzi matatizo ya wakulima, lakini hadi leo hajafika.
Alisema katani na pamba inayozalishwa Kishapu ni bora zaidi kuliko
sehemu yoyote nchini, lakini wakulima hao hawajafikiwa na wizara katika
kuwajengea uwezo wa kuzalisha zaidi ili wanufaike na kilimo chao.
“Baadhi ya kata za jimbo la Kishapu zina maji ya kutosha na
unahitaji utaalamu; huhitaji kuchimba ni kuzuia tu, waziri hayupo! Ni
bora mawaziri hao watoke wenyewe,” alisema.
Mbunge huyo alimshambulia Waziri Chiza na Naibu wake kwa tabia zao za
kutaka kukaa ofisini Dodoma na Dar es Salaam badala yake waende mikoani
kuonana na wakulima.
Mbunge huyo alimpongeza Waziri John Magufuri kwamba anapaswa kuwa
mfano wa kuigwa na mawaziri wengine kutokana na staili yake ya uchapaji
kazi.

Post a Comment