Yanga yailiza Rhino, Simba yakaa kileleni
MABINGWA watetezi wa Ligi Kuu ya Tanzania Bara, Yanga, jana
walivuna ushindi wa mabao 3-0 dhidi ya Rhino Rangers ya Tabora katika
mechi iliyochezwa Uwanja wa Taifa, jijini Dar es Salaam, ikiwa ni siku
tatu tu tangu watoke sare ya mabao 3-3 na mtani wao Simba.
Wakati Yanga wakivuna ushindi huo hivyo kupoza machungu ya sare ya
Jumapili, ambapo licha ya wakali hao wa Jangwani kuwa mbele kwa mabao
matatu, hadi mapumziko, Simba ilifanikiwa kusawazisha yote katika
kipindi cha pili.
Kwa ushindi huo, Yanga wamefikisha pointi 19 huku mtani wao Simba
ambaye jana alitoka sare ya bila kufungana na Coastal Union kwenye
Uwanja wa Mkwakwani, jijini Tanga, akifikisha pointi 20, hivyo kukaa
kileleni mwa msimamo wa ligi hiyo.
Katika Uwanja wa Taifa, Yanga walipata bao la kwanza dakika ya 15,
likifungwa na nyota wake wa kimataifa, Hamis Kiiza, aliyefunga mabao
mawili dhidi ya Simba, akimalizia pasi ya Simon Msuva.
Bao hilo lilionekana kuongeza kasi ya mchezo kwa kila moja kufanya
mashambulizi na kama nyota wa Yanga wangekuwa makini wangeweza kupata
mabao zaidi lakini hadi mapumziko walikuwa mbele kwa bao hilo moja.
Kipindi cha pili, Rhino walikianza kwa kasi huku mabeki wa Yanga
wakiwa imara kuonkoa hatari zote katika lango lao ambalo lilikuwa
likilindwa na kipa Deogratius Munish ‘Dida’ huku Rhino wakifanya
mabadiliko kadha kwa kumtoa Iman Ndely na kumwingiza Msafiri Hamisi.
Dakika ya 73, Yanga walipata bao la pili likifungwa na Frank Domayo
aliyemalizia kazi nzuri ya kiufundi iliyokuwa imefanywa na Ngasa
aliyewahadaa mabeki wa Rhino kabla ya kutoa pasi ya uhakika ambayo
ilitendewa haki.
Bao hilo lilizidi kupata nguvu Yanga ambao walizidi kupanga
mashambulizi na Kiiza kurejea tena katika nyavu za Rhino na kufunga bao
la pili kwake na la tatu kwa timu yake, akimalizia kazi nzuri iliyokuwa
imefanywa na Ngasa.
Hadi filimbi ya mwisho, Yanga wakatoka uwanjani na ushindi huo mnono
wakifikisha pointi 19, nyuma ya Simba, Azam na Mbeya City zenye pointi
20 kila moja.
Yanga: Deogratius Munishi ‘Dida’, Juma Abdul, David Luhende, Mbuyu
Twite, Kelvin Yondani, Rajab Zahir, Simon Msuva, Frank Domayo, Hamis
Kiiza, Mrisho Ngasa na Haruna Niyonzima.
Rhino Rangers: Mohamed Othman, Ally Mwanyiro, Julius Masoga, Ladislaus
Mbogo, Stanslaus Mwakitosi, Shija Mongo, Iman Ndely, Victor Hangaya,
Saad Kipanga na Nurdin Bakar.
Kutoka Uwanja wa Sokoine, jijini Mbeya, Mwandishi Wetu, Kenneth
Ngelesi, anaripoti kuwa Tanzania Prisons jana walitoka sare ya bao 1-1
dhidi ya Kagera Sugar.
Kagera Sugar walitangulia kupata bao dakika ya 58, likifungwa na Themi
Felix kabla ya Ernest Mwalupaji wa Kagera Sugar kujifunga katika
harakati za kuokoa.
Ligi hiyo inatarajiwa kuendelea kutimua vumbi kesho katika viwanja mbalimbali.

Post a Comment