ad

ad

Mfanyabiashara adai kuibiwa mil. 700/-

MFANYABIASHARA wa madini ya tanzanite, Pendaeli Mollel, ameitaka Benki Kuu ya Tanzania (BoT), kuingilia kati ili aweze kupata fedha zake zaidi ya sh milioni 700 alizodai zimepotea baada ya kuziweka kwenye akaunti zake katika Benki ya Exim tawi la Arusha.
Mollel aliwasilisha malalamiko hayo kwenye Idara ya Usimamizi wa Mabenki ya BoT, kupitia mwanasheria wake, Omar Iddi Omar, wa Kampuni ya Law Bridge ya jijini hapa, Julai 26 mwaka huu, akitaka imsaidie namna ya kupata fedha hizo.

Omar alidai kuwa katika kipindi cha miezi minne, mteja wake aligundua upotevu wa fedha katika akaunti zake tatu ambazo ni 5789633006, 5792261005 na 5789633334.

Alisema moja ya akaunti hizo ilikuwa ya dola za Marekani na nyingine ya fedha za Tanzania.

“Kama unavyoona, mteja wetu ameshuhudia upotevu huo katika akaunti hizo unaofikia dola za Kimarekani 361,722 pamoja na sh 225,000,000.

“Kiasi hicho ni kikubwa, na kwa ujumla kinamletea usumbufu, mfadhaiko na hali ngumu kwa biashara zake na familia yake ikizingatiwa yeye ni mfanyabiashara ndogo na ambaye anategemea fedha hizo katika mzunguko wa biashara yake,” ilisema sehemu ya barua hiyo.

Wakili Omar alisema kuwa hadi sasa mustakabali wa mteja wake uko shakani baada ya benki hiyo kukataa ombi lao la kutaka kulipatia ufumbuzi tatizo hilo kutokana na kukaa kimya bila kujibu barua yao waliyowapelekea Juni 6, mwaka huu.

“Tumeona ni vema kuomba uingiliaji kati wa idara yako adhimu tukiamini wewe ndiye msimamizi wa mabenki yote hapa nchini kisheria na mwenye mamlaka ya kuhakikisha mabenki yanatimiza wajibu wao wa kutoa huduma sahihi na zenye ubora kwa wateja,” iliongeza barua hiyo.

Akizungumza na Tanzania Daima, Mollel alisema kuwa aliamua kupeleka malalamiko yake BoT akiamini kuwa taasisi hiyo ya fedha itachukua hatua stahiki ingawa hadi sasa ni miezi miwili imepita bado hajapata majibu ya kuridhisha.

Alisema kuwa fedha hizo zilitolewa kwenye akaunti zake kwa njia tofauti ikiwemo kwa kuhamisha hundi pamoja na utoaji katika mashine za fedha (ATM).

“Nashangaa taarifa za benki zinaoyesha kuwa nimetoa au kufanya malipo kwa hundi na mashine za ATM wakati benki hiyo haikuwahi kunipa hundi yoyote au kadi ya ATM na mara zote naweka na kutoa fedha kwa kujaza fomu maalumu ya kutolea fedha.

“Nimeshitushwa kuona kuwa nimefanya malipo kwa njia ya hundi ya dola 50,000 kwa mfanyabiashara mmoja wa Arusha (jina linahifadhiwa) ambaye hata simfahamu wala hatukuwahi kufanya biashara ya aina yoyote, lakini pia sikuwahi kupewa kitabu cha hundi,” alisema Mollel.

Akizungumzia madai ya mfanyabiashara huyo, Mkurugenzi wa Idara ya Usimamizi wa Mabenki wa BoT, Kened Nyoni alikiri kupokea barua hiyo ya Mollel akilalamikia benki ya Exim na kupotea kwa fedha zake.

Wakili wa Exim Bank, Albert Msando alikiri kupokea barua za malalamiko ya Mollel na kwamba alizijibu huku akisema kuwa baada ya kupitia vielelezo vya karatasi ya kuweka fedha hizo benki (bank-in slip) pamoja na taarifa za benki (bank statement) walizoambatanisha, alibaini kuwa zina upungufu mkubwa.

Alisema kuwa mapungufu hayo hayawezi kujadilika nje ya mahakama kwa kile alichoeleza kuwa baadhi ya makaratasi hayo ya kuweka fedha yalikuwa hayajaandikwa namba ya akaunti, huku mengine yakiwa hayajasainiwa, hivyo akasema kuwa ni vema suala hilo likapatiwa ufumbuzi mahakamani.

Suala hili limeibuka huku kukiwa na shauri jingine la jinai kwenye Mahakama ya Hakimu Mkazi Arusha la kula njama na kuiba zaidi ya sh bilioni 7 linalowakabili wafanyakazi 14 wa benki hiyo akiwemo meneja wa tawi la Arusha, Bimal Gondalia.

Katika shauri hilo la jinai namba 309 la mwaka huu, washitakiwa hao ambao ni wafanyakazi wa Benki ya Exim tawi la Arusha, walisomewa shitaka la kula njama na kuiba zaidi ya sh bilioni 7 sanjari na kuiibia benki hiyo, fedha za Marekani dola 400,000 katika kipindi cha miaka mitatu.
HABARI NA TANZANIA DAIMA
Powered by Blogger.