ad

ad

Polisi wadaiwa kumpora mgeni Sh11 mil

WATU wanaodaiwa kuwa ni polisi kwa kushirikiana na raia wanaoaminiwa kuwa ni matapeli, wanadaiwa kumpora raia wa Yemen dola za Marekani 7,000 zinazokadiriwa kufikia Sh11 milioni pamoja na mali nyingine.
Raia huyo, Saleh Khalfan Abdulah Al Wahaibi alifika nchini mwishoni mwa mwaka 2011 kwa lengo la kutafuta fursa za biashara ya madini na baadhi ya kampuni za hapa nchini.
 Akizungumza na Mwananchi Jumapili Al Wahaibi alisema tukio hilo lilitokea Juni 25, 2012 katika baa ya Masai iliyopo Kinondoni, jijini Dar es Salaam na kwamba alikwenda kutoa taarifa kituo cha Polisi Osterbay na hakuna hatua zozote zilizochukiliwa hadi sasa.
Aliongeza kuwa anaamini kuwa polisi wanawafahamu watu hao lakini kwa sababu ambazo hazifahamu, hakuna hata mmoja aliyekamatwa na amekuwa akizungushwa mara kwa mara hadi alipoamua kwenda Kituo Kikuu cha Polisi, makao makuu lakini hata huko anadai bado anazungushwa.

Kwa mujibu wa Al Wahaibi alipozidi kulalamika katika Kituo cha Polisi Osterbay walichukuwa maelezo yake na kuyahifadhi katika kumbukumbu za kipolisi namba OB/RB/11569/2012.
Anasema alipokwenda makao makuu kupeleka malalamiko yake, alikabidhiwa kwa mmoja wa maofisa wa polisi ambao anakumbuka kuwa ni miongoni mwa watuhumiwa wa tukio hilo jambo ambalo linampa wasiwasi.

“Nilipoambiwa ofisa huyo (jina linahifadhiwa kwa sasa) kuwa ndiye atakeshughulikia kesi yangu, niliogopa kwa kuwa namkumbuka kuwa ni miongoni mwa walioshiriki kunipora fedha zangu,”alisema.
Katika barua yake kwa Mkurugenzi wa Upelelezi wa Makosa ya Jinai (DCI) ya Septemba 11, 2012 ambayo Mwananchi Jumapili imeiona, raia huyo wa Yemen ameomba kusaidiwa kupatiwa haki zake ikiwa ni pamoja na kuwakamata wahusika wa utapeli huo na kufikishwa kwenye vyombo vya sheria.

Akielezea mkasa mzima katika barua hiyo kwenda kwa DCI, Al Wahaibi alisema alipigiwa simu na mtu mmoja aliyemtaja kwa jina la Mohamed Bakari akimkaribisha Tanzania na kumtaka wakutane kwa mazungumzo ya kibiashara.
Kwa mujibu wa Al Wahaibi, anahisi Bakari alipata namba yake kutoka kwa mwanamke ambaye alianzisha mazoea naye alipokuwa akifika katika baa ya Masai, iliyopo Kinondoni. 

“Baada ya kuwasiliana kwa muda mrefu na kukutana naye, siku moja alinipigia simu akiniambia anahitaji kuonana na mimi sababu anajambo muhimu,” anaeleza Al Wahaibi.
Anasema alipofika alikuta Bakari katika nyumba moja ambayo haikumbuki vizuri lakini ipo maeneo ya Buguruni akiwa na mtu mwingine  ali yemtambulisha kama rafiki yake anayeitwa Sadik Salim Bakari na kumweleza kuwa mke wa Sadik ana matatizo na anahitaji fedha dola 5,000 ambazo anadaiwa na bosi wake kazini na kwamba amekuwa akitembea na mke wake kwa mgongo wa deni hilo.
Aliongeza kuwa watu hao walimwahidi wangemlipa deni hilo ndani ya siku mbili kwani wanasubiri fedha zao na kwamba wangemlipa na faida ya dola 5,000 zaidi kama riba.

Raia huyo ambaye kwa sasa anaishi Mbagala Kimbangulile anasema siku ya makabidhiano ya fedha hizo na kusaini mkataba ambayo walikubaliana yafanyike Masai baa, Bakari alimpigia simu kuwa anakuja na muuzaji wa dhahabu aliyemtaja kwa jina la Hamis Ngwamangwa.
“Walipofika niliwataka wanioneshe vitambulisho vyao na kumtaka Sadik anikabidhi hati yake ya kusafiria (passport), lakini walisema wamevisahau na hapo niligundua kuwa watu hao ni matapeli kwani hata dhahabu alizokuja nazo Ngwamangwa zilikuwa feki pia,” anaeleza.
Anasema Bakari ndiyo aliyemtolea bastola na kumlazimisha kusaini mkataba wa makubaliano ya kuwapa fedha na kumrudishia baada ya siku mbili, kisha alimsukuma chini na kuchukua fedha zake dola 7,000 na simu na kumtishia kuwa wangemuua kama angejaribu kufanya chochote.
                                                CHANZO GAZETI LA MWANANCHI
Powered by Blogger.