ad

ad

Ngassa, Van Persie, Messi sahani moja

MSHAMBULIAJI wa Taifa Stars na Simba, Mrisho Ngassa ametajwa kwenye orodha ya wafungaji bora wa mwaka 2012 pamoja na Lionel Messi, Neymar, Falcao, Robin van Persie na Samuel Eto’o. Katika orodha iliyochapishwa na mtandao www.iffhs.de unaojihusisha na masuala ya takwimu za soka unamwonyesha Ngassa akiwa katika nafasi ya 65 katika orodha ya wafungaji 90 bora kwa mwaka jana akiwa amezifumania nyavu mara saba akiwa na kikosi cha timu ya taifa ya Tanzania.
 
Ngassa amefanikiwa kuingia kwenye orodha hiyo baada ya kuwafunga mabingwa wa Afrika, Zambia bao 1-0, pia alifunga bao Stars ilipotoka sare 3-3 na Botswana pamoja na mabao matano aliyoyafunga dhidi ya Somalia kwenye Kombe la Chalenji nchini Uganda.
Awali mshambuliaji wa TP Mazembe, Mbwana Samatta mwezi Septemba aliingia katika orodha hiyo akiwa ameshika nafasi ya 61 baada ya kufunga mabao 6 akiwa na klabu yake.
Hata hivyo, Samatta ameshindwa kuingia kwenye orodha ya wafungaji bora wa mwaka kutokana na nyota huyo kushindwa kufunga bao lolote akiwa na Taifa Stars au Kilimanjaro Stars mwaka jana.
 
Mshambuliaji wa Argentina na Barcelona, Messi amefanikiwa kutetea taji lake la kuwa mfungaji bora duniani akiwa amezifumania nyavu mara 25, kati ya hayo mabao 12 amefunga akiwa na timu ya Taifa na 13 Ligi ya Mabingwa Ulaya na kuifikia rekodi ya dunia ya Vivian John Woodward (England) aliyefunga mabao 25 katika michezo ya kimataifa katika mwaka 1909.
 
Chipukizi wa Brazil, Neymar ameshika nafasi ya pili akiwa na mabao 21 baada ya kufunga mabao matatu kwenye Michezo ya Olimpiki, London.
Hata hivyo bila ya mabao hayo angeendelea kubaki nafasi ya pili katika wafungaji bora wa 2012 kwa sababu ya kufunga mabao mengi kwa timu ya taifa kuliko Cristiano Ronaldo (18) anayeshika nafasi ya tatu.
 
Mshambuliaji wa PSG na Sweden, Zlatan Ibrahimovic (17) anakamata nafasi ya nne huku nyota wa Colombia, Radamel Falcao (17) akishika nafasi ya tano, kiungo Mohamed Aboutreika wa Al-Ahly ya Misri anashika nafasi sita (16) wakati Didier Drogba wa Ivory Coast akiwa nafasi ya tisa na mabao 12.
 
Washambuliaji wa Manchester United, Robin van Persie na Javier Hernandez wanashika nafasi ya 22 na 23 wakiwa wamefunga mabao 10 kila mmoja mwaka jana.
Tangu mwaka 1991, IFFHS imekuwa ikipiga hesabu na kutoa orodha ya wafungaji bora wa mwaka wa dunia kwa kuangalia mabao wanayofunga kuanzia Januari hadi Desemba 31.
Wafungaji hao wanapatikana kwa kuzingatia mabao waliyofunga kwenye michuano ya kufuzu kushiriki Fainali za Kombe la Dunia, michuano ya mabara kwa timu za taifa, Olimpiki, pamoja na mashindano ya klabu ya kimataifa.
Kama idadi ya mabao itakuwa sawa yule aliyefunga mabao mengi kwenye mechi za kimataifa anapanda juu.
                                CHANZO CHA HABARI  MWANANCHI
Powered by Blogger.