ad

ad

Yanga Waanza Mchakato Wa Mabadiliko

Katibu Mkuu wa Yanga,Boniface Mkwasa (Kushoto) akitoa ufafanuzi mbele ya waandishi wa habari kuhusu mchakato wa muundo mpya wa uendeshaji wa klabu yao katika kuleta mabadiliko.

MABOSI wa Yanga wameanza mchakato wa muundo mpya wa uendeshaji wa klabu yao katika kuleta mabadiliko.

Hiyo, ikiwa ni siku chache tangu watani wao wa jadi, Simba waikabidhi klabu yao kwa mwekezaji bilionea, Mohamed Dewji ‘Mo’.

Yanga imefikia maamuzi hayo, baada ya kikao cha Kamati ya Utendaji ya timu hiyo chini ya Kaimu Mwenyekiti, Clement Sanga kukutana juzi Jumatano.

Akizungumza, Katibu Mkuu wa timu hiyo, Boniface Mkwasa kwa mujibu katiba ya mwaka 2010 ibara ya 56 (3) iliyosajiliwa na msajili inawaruhusu wao kumpa mwekezaji klabu hiyo.

Mkwasa alisema, katiba hiyo inaridhia kumpa mwekezaji asilimia 49 mwekezaji huku 51 ikiwa inamilikiwa na wanachama wa klabu, hivyo hivi sasa wapo kwenye mchakato wa kumpa mwekezaji na kikubwa ni kuleta mabadiliko.

Aliongeza kuwa, kupitia katiba hiyo kamati hiyo imepitisha mchakato huo wa mabadiliko na tayari wameanza kuchagua watu watakaosimamia mpango huo kwa kuzingatia vigezo muhimu ambavyo ni lazima awe na taaluma ya sheria.

Aidha alisema, watu watakaosimamia mchakato watawapa kazi ya kutathimini mali za klabu ikiwemo zisizohamishika kama majengo yao ya Jangwani na lile lililokuwepo mtaa ta Mafia, Dar na zile zinazohamishika kama magari.

No comments

Powered by Blogger.