Lowassa aiteka ngome ya Dk Slaa
Mgombea wa Urais kupitia Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema),
Edward Lowassa, jana ameiteka ngome ya aliyekuwa Katibu Mkuu wa
Chadema, Dk. Wilbroad Slaa.
Jana, umati ulijitokeza kwenye uwanja wa Mbowe mjini Karatu kwa ajili ya kumlaki Lowassa.
Lowassa aliongozana na Mwenyekiti wa Chadema, Freeman Mbowe,
aliyekuwa muasisi wa CCM, Kingunge Kombale-mwiru, Waziri Mkuu mstaafu,
Frederick Sumaye, aliyekuwa mbunge wa Arumeru Magharibi, Goodluck
Ole-Medeye na mgombea wa Ubunge wa Monduli, Julius Karangaraiza.
Akizungumza na wananchi wa Karatu, Lowassa aliwataka wananchi wa
wilaya hiyo, kulinda kura hizo na wasihadaike na fedha zitakazotolewa.
“Watapitapita kuwapa pesa lakini msikubali, wakiwapa laki tano
waambieni hazitoshi...wakitoa milioni moja waambieni hazitoshi...”,
alisema.
Aidha, alisema akiingia madarakani atahakikisha walimu wanalipwa vizuri ili waweze kufanyakazi zao kwa ufanisi.
Hata hivyo, aliwashukuru maaskofu kwa kuonyesha maana ya uchaguzi
kwa kuwaruhusu waumini wao kwenda kupiga kura siku ya Jumapili.
MBOWE AMSHTAKI DK. SLAA
Mbowe alisema mara ya mwisho kusimama na kuzungumza na wananchi wa
Karatu ilikuwa miaka 20 iliyopita akiwa na aliyekuwa Katibu mkuu wa
chama hicho, Dk. Wilbroad Slaa.
“Leo nasimama hapa nikiwa peke yangu bila mndani wangu, rafiki
yangu, ndugu yangu na kaka yangu Dk. Slaa,”alisema na kuongeza:
“Sizungumzi kwa kuwa nina furaha bali nasikitika kwa kumpoteza mwenzetu
ambaye aliishia njiani ambaye hakutaka kuendelea na safari hii ya
kuwakomboa wananchi.”
Alisema ndani ya Chadema hakuna mkubwa kuliko Watanzania kwa sababu
chama hicho kilijengwa lakini si mali ya Chadema bali ni ya wananchi.
Alisema walizungumza na watu wa utafiti kutoka nje ambao waliwaambia
wakitaka kuiongoza Tanzania ni lazima waipasue CCM kwa sababu kuna mtu
atawasumbua.
“Tuliwauliza ni nani atakayetusumbua, wakatujibu ni Lowassa kwa
sababu anapendwa na kila Mtanzania,” alisema. Alisema wakiwa kwenye
mchakato wa kuipasua CCM, Dk. Slaa alipokea ujumbe kuwa Lowassa amekatwa
na chama chake.
“Dk. Slaa alinifuata na kuniambia kuwa Lowassa amekatwa na
tukashauriana kumfuata Lowassa ili awe mgombea wetu...lakini cha ajabu
Dk. Slaa aliporudi nyumbani, nyumba ikawaka moto,” alisema.
Alisema, Dk. Slaa akitaka kurudi Chadema watamsamehe na nafasi yake bado ipo.
“Tumemsamehe Dk. Slaa kama anataka kurudi nyumbani tutampokea kwani nafasi yake bado ipo,”alisema.
KINGUNGE
Naye, Kingunge alisema ameamua kuondoka kwenye chama chake kwa
sababu viongozi wa CCM wanakiongoza chama kama mali yao binafsi. “Siwezi
kuendelea kukaa ndani ya chama cha CCM kwa sababu siwezi kukubali
kuendelea kuona watu wanaivunja katiba ya chama.
“Kama kuna wanachama wa CCM ambao wanapenda maendeleo na wanaipenda nchi yao wajifikirie wenyewe ili waweze kuamua,” alisema.
Alisema CCM haiwezi kuwaletea mabadiliko Watanzania kwa sababu wameishiwa na pumzi.
SUMAYE
Alisema Tanzania haiwezi kuongozwa na Magufuli kwa sababu hashauriki wala hana huruma kwa Watanzania.
“Magufuli alishawahi kuwaambia watu wa Kigamboni wapige mbizi kwa sababu hawana pesa za kulipia kivuko...huyu mtu hana huruma.












Post a Comment