Taifa latikiswa •Bunge kuunda kamati teule, Bajeti Nishati yasitishwa.
SERIKALI imeapa kuwasaka waasisi wa vurugu za Mtwara ndani na
nje ya nchi ikisema kuwa waliohusika kupanga, kushawishi, kuandaa na
kutekeleza vurugu hizo hawataukwepa mkono wa sheria.
Kauli hiyo ya serikali ilitolewa jana bungeni na Waziri wa Mambo ya
Ndani ya Nchi, Emmanuel Nchimbi, akisema kuwa tofauti za Watanzania
lazima ziendelee kuzungumzwa kwa uwazi, kuheshimiana na kuzingatia
sheria na taratibu za nchi.
Nchimbi alisema vyombo vya dola vitaendelea kuimarisha amani na
utulivu katika eneo la Mtwara ili shughuli ziendelee kama kawaida.
“Tunalo taifa moja la Tanzania ambalo maliasili zake ni za Watanzania
wote, tabia inayoanza kujengeka ya kila eneo kutaka inufaike peke yake
na mali za eneo hilo italigawa taifa letu vipande vipande,” alisema.
Akieleza athari za vurugu hizo, Waziri Nchimbi alisema kuwa ofisi ya
mbunge wa Mtwara Mjini, Hasnain Murji (CCM), iliyoko Mikindani
iliharibiwa na kuibiwa vitu mbalimbali.
Nchimbi alisema kuwa ofisi ya mahakama ya mwanzo ya Mitengo ilichomwa
na kuteketea pamoja na nyaraka za ofisi huku ofisi ya CCM kata ya
Chikongola ikichomwa moto.
Aliongeza kuwa nyumba binasfi ya ofisa mtendaji kata ya Magomeni
ilichomwa moto, nyumba za askari polisi wanne zilivunjwa na kuibiwa vitu
mbalimbali.
“Nyumba ya mwandishi wa habari wa TBC, Kassim Mikongolo, imechomwa
moto na kuteketea; na ofisi ya kata ya Kichongola imeharibiwa na kuibiwa
vitu mablimbali. Thamani halisi ya mali zote zilizoungua na kuharibiwa
bado haijapatikana,” alisema.
Waziri Nchimbi alisema kuwa mtu mmoja Karim Shaibu alifariki katika
vurugu hizo na askari wawili walijeruhiwa kwa bomu la kishindo.
“Kutokana na usalama kuzorota, mkuu wa mkoa wa Mtwara kwa mujibu wa
sheria aliomba kwa Waziri wa Ulinzi kuongezewa nguvu kulinda raia wasio
na hatia na mali zao,” alisema.
Aliongeza kuwa waziri alikubali na kulielekeza Jeshi la Wananchi wa
Tanzania (JWTZ) liende mara moja na katika kutekeleza agizo hilo askari
32 wa jeshi hilo walianza safari kutoka Nachingwea kuelekea Mtwara.
Alisema kuwa walipofika njiani katika eneo la Kilimani Hewa, gari lao
lilipata ajali ambapo wanajeshi wanne walifariki na 20 kujeruhiwa.
“Wanajeshi hawa wamekufa na kujeruhiwa wakati wakiwa kazini kutekeleza
wajibu wa kuwalinda Watanzania wenzao. Damu yao haitamwagika bure,”
alisema.
Bunge laahirishwa
Kwa mara nyingine tena Spika wa Bunge, Anna Makinda, jana asubuhi
baada ya kauli hiyo ya serikali aliliahirisha Bunge hadi leo ili kutoa
nafasi kwa Kamati ya Uongozi kukamilisha kazi yake ya kuamua nini
kifanyike kufuatia vurugu hizo.
Pia Spika alisema kuwa mjadala wa hotuba ya bajeti umesitishwa hadi
hapo baadaye ili kuepusha kauli ambazo zinaweza kuchochea vurugu zaidi.
“Waheshimiwa wabunge tumeona kuendelea kujadili hapa hatujui kauli
zetu zinaweza kukoleza moto juu ya moto vipi, sasa Kamati ya Uongozi
tutakaa na kujadili kisha kuona hatua za kuchukua.
“Hivyo kesho tutaendelea na Wizara ya Afrika Mashariki, hii bajeti ya
Nishati na Madini tutaendelea nayo baadaye baada ya hali Mtwara
kutulia,” alisema.
Hata hivyo, chanzo chetu kilidokeza kuwa kamati hiyo ilimaliza kikao
chake kwa pendekezo la kuunda Kamati Teule itakayochunguza sakata zima
na kutoa mapendekezo.
Lakini baadhi ya wajumbe walipendekeza kuwa kamati hiyo isiende Mtwara
sasa hivi kufanya kazi hiyo kwani haitaweza kupata taarifa sahihi.
“Uamuzi wa ama kamati teule kuundwa au la umeachwa mikononi mwa Spika,
lakini kwa jinsi viongozi wetu wanavyopenda kufanya mambo kwa zima moto
wanaweza kuamua vinginevyo wakakimbilia kupeleka majeshi na hivyo
kusababisha balaa zaidi,” kilisema chanzo chetu.
Mbowe aibana serikali
Kionguzi wa Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni, Freeman Mbowe (CHADEMA),
alisema ni fikra potofu kudai kuwa mgogoro wa Mtwara unasababishwa na
wanasiasa.
Mbowe alisema kuwa wasababishaji wakubwa wa vurugu za Mtwara ni
serikali yenyewe ambayo haikujipanga kutatua jambo hilo mapema.
“Wakazi wa Mtwara ni jibu la tatizo na si chanzo cha tatizo, serikali
katika hili imeshindwa na imekuwa mshiriki mkubwa kwa njia moja au
nyingine, hivyo haiwezi kuwa mtatuzi wa tatizo hilo,” alisema.
Alifafanua kuwa ili ufumbuzi wa tatizo hilo uweze kupatikana ni
kushirikisha watu makini na taasisi ambazo zinaaminika kwa jamii ya wana
Mtwara,” alisema.
Pia alilaani nguvu kubwa inayotumiwa na serikali ya vyombo vya dola
kuwatawanya wananchi wa Mtwara akisema kufanya hivyo hakuwezi kusaidia
kutatua mgogoro na badala yake busara na hekima ya hali ya juu inatakiwa
kutumika.
Wabunge waponda
Baadhi ya wabunge waliozungumza katika viwanja vya
Bunge walimlaumu Rais Jakaya Kikwete wakisema amepuuzia mgogoro huo
tangu mapema.
Walisema kuwa serikali yake kupitia kwa mawaziri na viongozi wengine
wa kiserikali wamekuwa wakipotosha madai ya wananchi wa Mtwara na hivyo
kuonekana kama watu wasiotaka rasilimali za kwao zisinufaishe wengine.
“Tatizo la Rais wetu ni kutaka kumfurahisha kila mtu, jambo hili
serikali yake ndiyo imelipuuza kwa kuwadharau wananchi wa Mtwara. Sasa
huu ndiyo wakati wa yeye kuonyesha kuwa amani ya nchi inarejea,” alisema
mbunge mmoja.
Mbunge huyo wa CCM ambaye aliomba jina lake lihifadhiwe, alisema kuwa
malalamiko hayo waliyatoa hata kwenye kikao cha wabunge wa chama hicho
na Rais Kikwete.
Alisema walimweleza Rais kuwa amekuwa mpole sana kwa kutowakemea wanaojaribu kuhatarisha amani na usalama wa taifa.
Naye Mbunge wa Mwibara, Kangi Lugola (CCM), alisema Mtwara walipuuzwa
kwa kutokusikilizwa na kuwashanga viongozi kukimbilia kulalamika badala
ya kuchukua hatua.
“Tumeambiwa kuwa wanasiasa ndio wanachochea lakini kumbuka wanasiasa
ndio haohao wananchi…leo tunaambiwa yanaweza kuwa mataifa ya nje. Kwa
nini hatutafuti kiini mapema na kuchukua hatua kabla ya vurugu?”
alihoji.
Lugola alishauri kuwa hakuna sababu ya lazima kusafirisha gesi hiyo
kuja Dar es Salaam na badala yake mtambo unaweza kujengwa hukohuko
Mtwara ili gesi ikawa inafuatwa huko.
“Kwa nini dhahabu inayotolewa kwenye migodi kadhaa au samaki
wanaovuliwa Ziwa Victoria havipelekwi Dar es Salaam kwa ajili ya
kuchakatwa? Si mitambo imewekwa huko huko na wanaovitaka wanafuata
huko?” alihoji.
Mbunge wa Singida Mashariki, Tundu Lissu (CHADEMA), na James Mbatia
(NCCR-Mageuzi), walisema kuwa hatua inayochukuliwa na serikali ya
kutumia jeshi kuzima vurugu si suluhisho la kudumu.
“Huwezi kuzima moto halafu ukajivuna pasipo kudhibiti chanzo chake,
suluhu ya watu wa Mtwara ni mazungumzo, serikali inapaswa kukaa nao na
kuwaelewesha faida ya bomba inalotaka kulijenga,” alisema Lissu.
Mbatia naye alisema kuwa serikali imeshindwa kumaliza mgogoro huo,
hivyo lazima Bunge liisimamie serikali itemize wajibu wake.
Alisema Mtwara waliahidiwa viwanda miaka mingi lakini siku zinakwenda
hawaoni hatua inayofanyika kutimiza ahadi hiyo kama ilivyo kwenye mikoa
mingine.
Alisema kwa wakati huu kila taarifa si ya kupuuzwa kwani katika dunia
hii ya utandawazi wenye maslahi na gesi hiyo ni wengi na hivyo
inawezekana wakajipenyeza hata kuwagawa wananchi wa Mtwara.
Mnyika apinga
Mbunge wa Ubungo, John Mnyika (CHADEMA), amepinga hatua ya Waziri
Nchimbi kutoa kauli ya serikali wakati wa kipindi cha maswali na majibu
kwa Waziri Mkuu akisema ni kuvunja kanuni kwani kiongozi huyo wa
serikali alikuwepo.
“Pinda amekwepa kutoa taarifa kwa kuwa anajua kwamba aliahidi wakati
akijibu maswali kwenye mkutano uliopita wa Bunge kuwa ufumbuzi wa
mgogoro wa Mtwara umeshapatikana na kwamba tatizo lilikuwa ni uelewa
tu,” alisema.
Mnyika alisema kuwa kipindi cha maswali kwa Waziri Mkuu ni cha kwake
mwenyewe na kanuni ya 38(4) inaruhusu kama kuna jambo la kulitolea
taarifa afanye hivyo.

Post a Comment