ad

ad

Kesi ya Sugu: Mabishano makali yaibuka mahakamani juu ya ushahidi

Kesi inayomkabili Mbunge wa Mbeya Mjini (CHADEMA) Joseph Mbilinyi 'Sugu' na Katibu wa CHADEMA Kanda ya Nyassa, Emmanuel Masonga imeharishwa siku ya leo baada ya kutokea mabishano makali Mahakamani hapo ya kisheria kutokana na ushahidi uliyotolewa.

Uamuzi huo umetolewa na Hakimu Mkazi wa Mkoa wa Mbeya Michael Mteite, baada ya shahidi namba tano Afande Joramu Magova ambaye ni Mkuu wa Kitengo cha Tehama katika Ofisi ya Upelelezi Mkoa wa Mbeya kutoa ushahidi wake mbele ya Mahakama na kumtaka Hakimu kusikiliza sauti zilizokuwa zimehifadhiwa kwenye kinasa sauti. Hali ambayo ilipelekea kuibuka kwa mabishano ya kisheria baina ya Mawakili wa Jamhuri na wa upande wa utetezi ambapo upande wa Jamhuri walikuwa wanataka sauti zisikilizwe na upande wa utetezi ukipinga.

Kutokana na hali hiyo Hakimu Mkazi wa Mkoa wa Mbeya Michael Mteite amehairisha kesi hiyo mpaka siku ya kesho (Jumatano) ambapo atoa uamuzi wa juu ya hilo kama utasikilizwa ushahidi huo wa sauti mbele ya Mahakama au laa.

Mbunge huyo wa Mbeya mjini na Katibu wa CHADEMA Kanda ya Nyassa walishikiliwa na jeshi la polisi wakituhumiwa kutenda kosa la uchochezi katika mkutano wao wa hadhara ambao ulifanyika Disemba 31, 2017 jijini Mbeya ambapo jeshi la polisi linasema kuwa viongozi hao walizungumza maneno yenye kuleta chuki kati ya Serikali na wananchi

Chanzo: EATV

No comments

Powered by Blogger.