Binti wa Miaka 21 Atiwa Mbaroni kwa kuchoma moto nyumba sababu ikitajwa kuwa ni wivu wa kimapenzi
Jeshi
 la polisi mkoani Singida,linamshikilia mkulima mkazi wa Mitunduruni 
mjini hapa, Mariamu Juma (21), kwa tuhuma ya kuchoma nyumba moto na 
kuteketea pamoja na mali zote zilizokuwemo.
Kwa mujibu wa kamanda Jeshi la Polisi mkoa wa Singida, ACP Debora Magiligimba, kitendo hicho kimechangiwa na wivu wa kimapenzi.
Akizungumza
 na waandishi wa habari ofisini kwake, Kamanda Magiligimba,alisema kuwa 
tukio hilo limetokea Mei 30 mwaka huu saa 11.40 jioni, huko maeneo ya 
Mwenge tarafa ya Mungumaji Manispaa ya Singida.
Akifafanua,
 alisema kuwa siku ya tukio mtuhumiwa alienda kwenye nyumba aliyopanga 
mpenzi yake Benardo Mabula, ambayo inamilikiwa na Omari Hamisi (35) 
katika maeneo ya Mwenge mjini hapa.
“Uchunguzi
 wa awali wa Jeshi la Polisi  umebaini kuwa chanzo cha tukio hilo, ni 
wivu wa kimapenzi. Mtuhumiwa Mariamu alipoingia kwenye chumba cha rafiki
 yake wa kiume (Mabula),aliwasha moto kwa kiberiti kwa lengo la kuchoma 
vifaa vya mpenzi wake,” alisema na kuongeza;
“Lakini 
 moto huo ulisambaa vyumba vyote vya nyumba hiyo na kuteketeza kila 
kitu.Hadi sasa thamani ya nyumba na mali iliyoteketea, bado 
haijafahamika.”
Kamanda
 huyo alisema kuwa baada ya uchunguzi kukamilika, mtuhumiwa atafikishwa 
mahakamani kujibu tuhuma inayomkabili. Mpenzi wa mtuhumiwa 
Mariamu,amefanikiwa kutoroka na kukimbilia kusikojulikana.
“Jeshi
 la Polisi mkoani hapa,linatoa wito kwa wananchi wote hasa familia zenye
 migogoro ya ndoa,wafike ofisi zetu za dawati la jinsia na watoto 
zilizopo kila wilaya, ustawi wa jamii na viongozi wa dini, ili waweze 
kusikilizwa matatizo yao, badala ya kujichukulia sheria mkononi,” 
alisema Magiligimba.
Katika
 hatua nyingine, Kamanda huyo alisema vikongwe  wawili  wamefariki dunia
 papo hapo, baada ya kuangukiwa na ukuta wa nyumba iliyojengwa kwa 
tofali za tope na kuezekwa kwa bati.
Magiligimba
 alisema vikongwe hao na watu wengine, walikuwa kwenye nyumba hiyo, 
kushiriki mazishi ya Mwajuma Mwendo aliyefariki Mei, 28 na kuzikwa kesho
 yake.
Aliwataja
 vikongwe  hao kuwa ni Nzitu Mkumbo (80) mkulima kwa kijiji cha Mwangeza
 ambaye alivunjika miguu yote na mkono wa kushoto.Mwingine ni Kimwana 
Kingu (90) mkulima wa kijiji cha Mazangila, ambaye alivunjika mguu wa 
kulia na kujeruhiwa vibaya mguu wa kushoto. Vijiji hivyo vipo wilaya ya 
Mkalama. 
 Aliwataja
 waliojeruhiwa katika ajali hiyo ni Fatma Alli (70), Zena Ntoga (40), 
Kimwana Mohammed (70), Gyoli Kingu (45), Habiba Hussein (40) na Sophia 
Mashimba (50).
Alisema
 chanzo cha tukio hilo ni uchakavu wa nyumba hiyo iliyoanguka baada 
kupigwa na  upepo mkali na kusababisha ukuta wa ndani uliotenganisha 
chumba na sebule, kuanguka.
“Jeshi
 la polisi mkoa wa Singida,linatoa wito kwa wananchi wote wawe na 
utaratibu wa kukarabati nyumba zao mara kwa mara.Pia tunawashauri 
wapande miti kwa wingi kuzunguka maeneo ya makazi yao,” alisema kamanda 
Magiligimba.

Post a Comment