ad

ad

SAKATA LA POLISI KUMDAKA MSUVA PALE TAIFA HUKU MASHABIKI 'WAKIMRUKIA' CANNAVARO LILIKUWA HIVI



Sare ya bao 1-1 iliyopata Yanga dhidi ya African Lyon, jana ilikuwa chungu na kusababisha hali ya sintofahamu baada ya baadhi ya mashabiki wa Yanga kukasirishwa na matokeo hayo na kuzua varangati kiasi kwa wachezaji wa timu hiyo.
Matokeo hayo ya mechi hiyo ya Ligi Kuu Bara ambayo yanaifanya Yanga iendelee kubaki nafasi ya pili katika msimamo wa hiyo kwa kufikisha pointi 37 nyuma ya Simba yenye pointi 38, yaliwakasirisha baaadhi ya mashabiki walioamini kuwa wachezaji wao walifanya uzembe na ndiyo maana waliambulia pointi moja katika mchezo huo.
Nahodha wa Yanga, Nadir Haroub ‘Cannavaro’ na Simon Msuva katika nyakati tofauti walijikuta katika mazingira magumu baada ya mchezo huo uliofanyika kwenye Uwanja wa Uhuru jijini Dar.
MASHABIKI WAMVAA CANNAVARO
Baada ya mchezo huo mashabiki kadhaa wa Yanga wakionekana kuwa na hasira, walikuwa wakilalamika kuwa kitendo cha wachezaji kucheleweshewa mshahara wao wanaodai kimesababisha wacheze chini ya kiwango.
Kutokana na mashabiki hao kuonyesha hasira, ilibidi basi linalowabeba wachezaji wa Yanga liingie ndani ya uwanja kwa ajili ya kuwachukua lakini wengine wachache walielekea kwenye magari yao binafsi.
Wakati Cannavaro akitoka, ghafla alivamiwa na mashabiki waliokuwa wakimlaumu kwa matokeo hayo, baada ya muda uvumilivu ukamshinda na kujikuta akiwajibu kwa lugha kali, hali iliyosababisha mvutano na kutaka kupigana lakini daktari wa zamani wa Yanga, Juma Sufiani aliingilia kati na kumuondoa kisha kumpeleka kwenye gari lake.
Mashabiki hao walibaki wakitoa lugha kali huku wakilalamika wakati basi la wachezaji likitoka mlango wa nyuma na kuondoka huku mashabiki wengi wakiendelea kulisubiri upande wa mbele.
WACHEZAJI WATOA KAULI NZITO
Mchezaji mmoja wa Yanga (jina kapuni) akionekana kupandwa na hasira baada ya mchezo huo aliwajibu hovyo mashabiki wa timu yake waliokuwa wakilalamikia matokeo hayo kwa kusema: “Tumefanya kusudi na bado.”
Mwingine ambaye alianza katika kikosi cha kwanza cha jana, alisema bado hawajalipwa madai yao yaliyosababisha wagomee mazoezi wiki hii licha ya kuahidiwa kutimiziwa haki yao hiyo jana asubuhi.
MSUVA AKAMATWA
Wakati akitoka uwanjani hapo akiwa ndani ya gari lake aina ya Toyota Altezza, Msuva alisimama pembeni kidogo ya barabara, ghafla askari wa usalama barabarani walimfuata na kumwambia amesimama sehemu ambayo hatakiwi kuegesha gari.
Msuva akajitetea kuwa alikuwa akimsubiri mchezaji mwenzake, Ramadhani Kessy ambaye kweli alifika baada ya dakika kadhaa lakini askari hao hawakumuelewa, badala yake wakamtaka aende kituoni au alipe faini ya Sh 30,000.
Kuona hivyo, mashabiki wakaongezeka kwa wingi eneo hilo la tukio na kuwabembeleza askari hao lakini msimamo ulikuwa ni uleule, ndiyo wakalazimika kuchanga kiasi hicho cha fedha na kumlipia Msuva ndipo akaruhusiwa kuondoka huku akiwashukuru mashabiki hao.
MCHEZO ULIVYOKUWA
Baada ya kupata ushindi katika mechi iliyopita dhidi ya JKT Ruvu wa mabao 3-0, kocha mpya wa Yanga, George Lwandamina ameshindwa kuendeleza kasi yake ya ushindi.
Lyon ilianza kufunga kupitia kwa Venance Ludovick katika dakika ya 59, Yanga ilisawazisha katika dakika ya 74 mfungaji akiwa ni Amissi Tambwe aliyeunganisha kwa kichwa krosi ya Juma Abdul.
Tambwe atoa bao kwa mtoto

Akizungumza na gazeti hili, Tambwe aliyeshangilia kwa staili ya kunyonya kidole baada ya kufunga, alisema: “Bao nililofunga ni zawadi maalum kwa mwanangu (Amiyan) ambaye nimempata wiki hii baada ya mke wangu  (Raiyan) kujifungua.”

SOURCE: CHAMPIONI
Powered by Blogger.