ad

ad

KIFO CHA MTU ASIYE NA HATIA - 10 (MWISHO)

 
Prosper alitetemeshwa na swali la Alicia, alishindwa kuelewa ni jibu gani angempa mtoto wake, ingawa alielewa wazi ni kitu gani mtoto wake alitaka kufahamu! Ni yeye ndiye  alikuwa na wajibu wa matatizo yote ndani ya familia yake na ni yeye ndiye aliyeuingiza Ukimwi  ndani ya nyumba yake kwa sababu ya tabia ya kishoga aliyojifunza gerezani.
“Mwanangu Alicia!”
“Naam baba!”
“Ni mimi mwanangu ni mimi ninayekutesa!”
“Kwani ulifanya nini baba?”
“Ni mimi ninayekuua mwanangu!” Alisema Prosper na baadaye kuangua kilio.
“Ninahitaji kusamehewa sana Alicia na si wewe tu bali hata mke wangu anisamehe ninajua sote tutakufa kwa sababu ya uzembe wangu mimi!”
“Kwanini unasema hivyo baba?”
“Sikiliza Alicia, nilikutana na mama yako miaka mingi iliyopita tukiwa shuleni na tukapendana,lakini nilipata bahati mbaya ya kufungwa kwa kosa ambako sikulifanya, muda wote uliokuja kule nilikokuwa nikiishi nilikuwa gerezani  lakini hatukukuambia ukweli ni huko gerezani ndiko nilikoambukizwa Ukimwi ambao mimi niliupitisha hadi kwa mama yako na kutoka kwa mama yako ndiyo ulifika kwako nisamahe mwanangu!”
“Kwa hiyo mimi naumwa Ukimwi baba?Kwahiyo nitakufa?” Aliuliza Alicia huku akilia machozi.
“Huo ndio ukweli mwanangu si wewe tu utakayekufa bali mimi  pia na tutakufa sababu ya baba yako lakini hakuna sababu ya kumlaumu tumekwishachelewa hivyo  ni vyema kumsamehe kwani maji yakimwagika hayawezi kuzoleka, sawa  mwanangu Alicia?” Aliuliza Belinda akitegemea mtoto wake    angetoa msamaha lakini alishangaa kuona Alicia akiendelea kulia kwa uchungu na kuwalaumu wazazi wake kwa kila kitu.
“Siwezi kuwasamahe kwani sikustahili kufa kwa sababu ya makosa yenu! Ee Mungu kwanini uliruhusu jambo hili linitokee mimi?”  Alicia aliendelea kulia machozi! Maneno mengi aliyoyasema   hayakuwa ya mtoto wa umri wake!
“Nisamehe mwanangu!” Alisema Prosper huku akimbeba Alicia na kumweka miguuni pake.
“Kwanini nikusamehe baba?”
“Nisamehe  ni makosa yangu ndiyo yanayokutesa!” Aliendelea kusema Prosper.
Alicia aliendelea kulia na kuongea maneno ya kuwalaumu wazazi wake kwa kitendo walichokifanya   kusababisha yeye asiifaidi dunia na kuyafupisha maisha yake, aliwalaumu zaidi kwa kitendo cha kutomwambia ukweli  kwa kipindi kirefu na kutojali afya ake ili aishi maisha marefu zaidi.
“kwanini kama mlijua nilikuwa na Ukimwi hamkunifanyia kama daktari alivyoeleza, yaani kujali afya yangu ili niishi maisha marefu zaidi?”
“Tusamehe sana Alicia ni kwa sababu hatukutaka uujue ukweli huu!”
“Sasa imewasaidia kitu gani kunificha si ndio mneniua mapema zaidi wazazi wangu?” Alisema Alicia huku akijifuta machozi machoni pake.
Prosper na mke wake waliyajua makosa yao na  hapakuwa na njia nyingine yoyote zaidi ya kumwomba msamaha mtoto wao, waliendelea kumwomba awasamahe kwa   masaa matatu zaidi lakini Alicia hakujibu kitu zaidi ya kuendelea kulia, kila alipouangalia mwili wake ulivyokonda na kujaa vidonda alizidi kulia kwa uchungu na kuwatupia wazazi wake lawama.
“Basi nimewasamahe wazazi wangu ila yote namwachia Mungu  aliyeruhusu jambo hilo litokee yeye ndiye anayejua mwisho wangu!”
“Ahsante Alicia!” Prosper na mke wake walijikuta wakiitikia kwa pamoja na kumkumbatia mtoto wao, waliyajua makosa yao.
           ***************
Hali ya Alicia iliendelea kuwa mbaya kadri siku zilivyozidi kwenda, jambo hilo liliwaumiza  sana mioyo wazazi wake! Jamii ya wanafunzi katika shule aliyosoma walimtenga hawakutaka kucheza naye wala kusoma pamoja naye, alikaa peke yake katika  dawati mambo hayo yalimkosesha   raha kabisa na kusababisha achukie shule na kusimama masomo!
Wazazi wake walitumia karibu kila kitu walichopata  kumtibia mtoto wao lakini haikusaidia kitu hali yake ilizidi kuwa mbaya  hatimaye Alicia alikufa kwa kifua kikuu alichoogua siku za mwisho kabisa  za uhai wake, lilikuwa pigo kubwa mno kwa Prosper na mkewe Belinda! Kilikuwa kilio kikubwa mno kilichowatia simanzi  na moyo wa Prosper uliumiza zaidi sababu  siku zot alijiona yeye ndiye alikuwa muuaji wa familia yake.
            ************
Baada ya kifo cha  Alicia maisha ya Belinda na Prosper yalikuwa ni huzuni tupu, hawakuwa na kimbilio jingine zaidi ya kumwamini Kristo! Walijiunga na kanisa la Full Salvation Bible fellowship lililoko Mikocheni jijini Dar es Salaam, ambako waliamini wangepata  faraja.
Wakiwa ndani ya kanisa hilo matumaini yao yaliyokwishapotea yalirejea! Walikutana na waathirika wengine ndani ya kanisa na kwa pamoja waliamua kuanzisha chama cha waathirika wakristo kilichoitwa Christians affected with HIV&AIDS Solidarity (CAHAS).
Chama hiki kiliwakutanisha waathirika wote Wakristo  hata kutoka madhehebu mengine na kuwafanya wawe wamoja, Prosper ndiye alikuwa Mwenyekiti wa chama hicho kilichojishughulisha na Elimu na ushauri nasaha kwa wagonjwa na waathirika wa Ukimwi! Kilifanya mikutano ya Dini iliyofundisha watu juu ya gonjwa hilo hatari.
Pamoja na faraja na matumaini kurejea, siku zote Prosper na mkewe hawakumsahau mtoto wao Alicia, karibu kila kitu walichokiona ndani ya nyumba yao na hata barabarani kiliwakumbusha  mtoto wao,iliwatia uchungu sana kumpoteza mtoto wao mzuri! Kila siku iliyokwenda kwa Mungu hawakuacha kumwombea Alicia kwa Mungu ili apumzike kwa amani!
Mei 23 kila mwaka   waliazimisha sikukuu ya kuzaliwa kwa Alicia, kama kumbukumbu ya mtoto wao. Maisha yao yaliendelea vizuri na walizidi kunawiri   haikuwa   rahisi kuamini kuwa wote wawili  walikuwa waathirika na Ukimwi kwa jinsi walivyoonekana  wanene  wenye afya na siha njema! Lakini huo ndio ulikuwa ukweli wa mambo.
             ****************
Miaka mitano baadaye:
Mama wa kambo wa Belinda alikuwa katika hali mbaya kwa ugonjwa wa homa ya matumbo, homa hiyo iliutoboa kabisa utumbo wake  sababu ya kuchelewa kupata matibabu, hali ambayo madaktari waliita Intestinal Perforation, madaktari walisema kwa hali ilivyokuwa ilikuwa si rahisi kuokoa maisha yake  labda kubadilisha utumbo  na kuweka mwingine jambo ambalo ilikuwa si rahisi kuwezekana.
Pamoja na mabaya yote ambayo mama yake alimfanyia ni Belinda aliyeshughulikia  matibabu ya  mama huyo, hakuwa na mtu mwingine wa kumsaidia zaidi ya Belinda.
“There is nothing we can do! Your mom’s intestines are badly perforated! Unless intestinal transplant is done! Which is not easy here!”(Hakuna kinachoweza kufanyika  kwa sababu utumbo wa mama yako umetobolewa vibaya sana labda kuubadilisha  kabisa  jambo lisilowezekana kufanyika hapa) Daktari alimwambia Belinda.
“Where do you think that procedure can done, all we need  is to save my mom’s life!”( Wapi unafikiri hilo  linaweza kufanyika! Tunachohitaji  ni kuokoa maisha ya mama tu) Aliuliza Belinda.
“There is no place in Africa, but why do you want to spend your money for an impossible mission?”(Hakuna mahali hapa Afrika lakini kwanini unataka kutumia pesa yako kwa kufanya jambo lisilowezekana?) Daktari alimuuliza Belinda ni hapo ndipo alipogundua haikuwa rahisi kuokoa maisha ya mama yake wa kambo.
Mama yake alifariki siku tatu tu baadaye na kabla ya kifo chake mama huyo alimrithisha Belinda kisheria mali zote alizoachiwa na mume wake akazikwa na idadi kubwa ya watu wa jiji la Dar es Salaam.
           ****************
Kufuatia kurithishwa mali za mamilioni Belinda na Prosper wakawa miongoni mwa watu matajiri katika jiji la Dar es Salaam! Magari yote yaliyoendeshwa na marehemu mama wa  kambo  wa Belinda   yakawa mali yao! Majumba yote ya kifahari yakawa mali yao, watu wengi waliwaona wana maisha mazuri lakini kwa Belinda na Prosper mali haikuwa na maana tena kwa sababu maisha yao yalikuwa ukingoni.
Walichofanya na kilichowashangaza wengi ni uamuzi wao wa  kuanza kuuza mali zote walizoachiwa na kugawa pesa iliyopatikana kwa vituo vya watoto yatima nchini, waliendesha mnada kila sehemu kulikokuwa na nyumba  au mali za marehemu baba yao na pesa iliingizwa katika akaunti maalum ya kusaidia watoto yatima wa Ukimwi  iliyofunguliwa  katika benki ya CRDB!
Sifa zao zilienea nchi nzima  na hata kuvuka mipaka ya Tanzania, walialikwa kuhudhuria mikutano mbalimbali ya Ukimwi duniani! Uamuzi wao wa kutumia walichokuwa nacho kusaidia mayatima wa Ukimwi ulikuwa ni wa kishujaa!
Wafadhili wa shirika la umoja wa Kimataifa linalojishughulisha na Ukimwi, UNAIDS waliposikia habari juu ya juhudi zao   walisafiri hadi Tanzania na kufanya nao maongezi juu ya namna gani wangeweza  kuwasaidia, baada ya makubaliano walilazimika kuanzisha mfuko maalum waliouita PROBE FUNDS! Yaani mfuko wa Prosper na Belinda, Pro ikisimama badala ya Prosper na Be ikisimama badala ya Belinda pesa yote waliyokuwa nayo waliingiza katika mfuko huo.
UNAIDS ilingiza kiasi cha dola za Kimarekani milioni  tano katika mfuko huo na kuufanya mfuko huo kuwa na kiasi cha dola  za Kimarekani milioni  tano na nusu ambazo zilikuwa ni sawa na shilingi za Kitanzania bilioni  nne na nusu!Pesa hizo zote zilitumika kusaidia mayatima wa Ukimwi, vituo zaidi ya mia  vya kulea watoto yatima vilijengwa nchini Tanzania kwa kutumia pesa ya mfuko huo.
Prosper na mkewe hawakutumia hata senti tano kutoka katika mfuko huo, waliishi maisha ya kawaida hadi walipoanza kuugua na baadaye kufa wakiwa wamepishana miezi mitatu tu kati yao !Majina yao hadi leo hii yanaheshimika nchini Tanzania na mfuko wa  Probe bado unaendelea kusaidia waathirika na mayatima wa Ukimwi!
MWISHO.
Powered by Blogger.