WAKALA WA SHETANI - 02

MTUNZI: Ally Mbetu ‘Dr Ambe’
ILIPOISHIA:
Mathayo baada ya kumhudumia mtoto wake na mkewe ambaye aliweza kukaa mwenyewe, kazi akawa kumtazama mtoto aliyezaliwa wa aina gani. Uchunguzi ulionesha mtoto yule ni albino. Walijikuta wote wakikosa raha hasa ngw’ana Bupilipili ambaye aliamini ana mtihani mkubwa wa kumpoteza tena mtoto mwingine ambaye amekaa naye tumboni kwa kipindi kirefu halafu watu wamchukue na kwenda kumuua kiurahisi.
SASA ENDELEA...
“Unaona sasa mume wangu, ungemwita mama Sabina lazima siri hii ingetoka nje.”
“Sasa tutafanyaje na hali hii imetokea?”
“Dawa ni kumficha mtoto wetu ili wasijue nimejifungua.”
“Tutamfichaje? Pia mtu aliyejifungua anajulikana kwa tumbo kupungua na mtoto wetu tutamlea vipi usionekane kwa watu?” Mathayo aliona mtihani mgumu.
“Mume wangu nitaendelea kuweka nguo tumboni siku zote ili lionekane kubwa.”
“Tumbo sawa litaonekana kubwa, mtoto tutamweka wapi? Tukimficha ndani lazima atalia na kutoa sauti majirani watataka kujua ni mtoto wa aina gani. Na wakimuona hawatakubali kumuacha lazima watamuua, pia kutupiga faini ya ng’ombe watano huoni kama zizini kwetu ng’ombe watapungua?”
“Hilo nililijua toka mwanzo na nilijipanga kwa ajili ya hili,” ngw’ana Bupilipili alimtoa hofu mumewe aliyeonekana kuchanganyikiwa zaidi.
“Tutafanyaje mke wangu, huwezi kuamini hapa akili haifanyi kazi kabisa, siwezi kupoteza mtoto wa pili hivi hivi. Mke wangu sikubali nitaua mtu safari hii siwezi kukubali mtoto wangu auawe,” Mathayo alisema kwa uchungu kumuunga mkono mkewe.
“Nimepanga kitu kimoja kama nitajifungua albino.”
“Kipi hicho?” Mathayo aliuliza kwa shauku ya kujua mke wake amepanga nini.
“Usiku huu tutakwenda hadi kwenye mlima wa karibu na shamba letu, kuna pango nimeliandaa kwa ajili ya kumficha mtoto wetu.”
“Mke wangu unataka kuniambia usiku huu tutamwacha mtoto peke yake kisha turudi nyumbani?”
“Hapana, kila siku tutatoka alfajiri hadi kwenye pango hilo, kisha wewe utaingia shambani nami nitakuwa karibu na mtoto mpaka atakapokua kidogo, tutatoroka usiku kwa usiku na kwenda kijiji kingine.”
“Lakini mke wangu ni kijiji gani tutakachoweza kuishi na mtoto huyu bila matatizo?”
“Mume wangu hebu tufanya hili kwanza mengine yatafuata baadaye.”
Usiku uleule walimchukua mtoto wao na kutoka naye kiza kwa kiza. Japokuwa usiku ulikuwa mkubwa wenye kutisha, Ngw’ana Bupilipili alionesha ujasiri wa ajabu kwa kumuongoza mumewe hadi shambani kwao ambapo pembeni yake kulikuwa na kilima kidogo ambacho ndipo alipoandaa pango la kumtunzia mtoto wao.
Walitumia majani makavu kuyawasha moto ili kutengeneza tochi ya dharura kumulika sehemu ile. Mumewe alishangaa kukuta sehemu ile imetengenezwa vizuri sana.
“Mke wangu umetengeneza lini huku?”
“Toka nilipopata wazo la kujifungua tena mtoto albino basi nilijawa na mawazo ya kunusuru maisha ya mwanangu na kupata wazo la kupatengeneza huku.”
Walimlaza vizuri mtoto wao kisha Ngw’ana Bupilipili alijilaza pembeni ya mwanaye, naye Mathayo alilala pembeni kidogo ya mkewe, kwa vile muda ulikuwa bado usingizi uliwapitia.
Waliamshwa na sauti ya mtoto aliyekuwa akilia, Ngw’ana Bupilipili alishtuka usingizini na kukuta kumeanza kupambazuka, alimnyonyesha mtoto wake aliyeonekana ana njaa. Wakati huo mume wake alikuwa amekwisha amka na kutoka nje kuangalia hali ya usalama.
“Mke wangu wacha nirudi nyumbani nikawaandalieni chochote kitu.”
“Hakuna tatizo usisahau dawa zangu tumbo nalisikia kwa mbali.”
“Hakuna tatizo mke wangu.”
Mathayo kabla ya kuondoka alimtazama mkewe na kisha mtoto wake ambaye hakuwa na habari yeyote zaidi ya kuchezesha mikono na miguu baada ya kushiba na kufurahi kuja dunia salama, bila kujua hatari iliyo mbele yake ya kuonekana mkosi kwa jamii.
Bila kutegemea machozi yalimtoka kumwonea huruma mkewe ambaye aliamua kuishi maisha ya siyo yake kuhofia uhai wa mtoto wao.
Pia alimuonea huruma mtoto wao ambaye bado alikuwa hajapewa jina kutokana na misukosuko ya moyo wa kutaka kuokoa kwanza maisha yake baada ya wanakijiji kuona watoto maalbino ni mkosi kama wakiachwa kijiji kitapata balaa kubwa.
Japokuwa awali naye alikuwa ni mmoja wa watu walioamini albino ni mkosi, lakini mambo yalibadilika baada ya kutokewa yeye. Mwanzo naye alishiriki kuwaua watoto wa wenzake. Siku zote msiba wa mwenzio hauumi lakini msiba ikiwa kwako utajua uchungu wake. Mathayo baada ya mkewe kujifungua mtoto wa kwanza albino alikubali auawe lakini mkewe alisimama kidete asiuawe na kuwa tayari wafukuzwe kijijini.
Wakati wanahama kijiji walipovamiwa na vijana wa kijiji wenye jukumu kusaka na kutoa uchafu wa watoto wanaoonekana wanaleta mikosi kijijini. Mtoto albino alipouawa nyumba ilifanyiwa tambiko na kutengwa kwa muda wa wiki mbili.
Kilio cha mkewe baada ya kubeba ujauzito wa pili cha kuhofia uhai wa mtoto wake kilimfanya Mathayo naye abadili uamuzi na kuwa tayari kukisaliti kijiji pindi mkewe atakapo kifungua mtoto albino. Aliapa moyoni hatakubali kumtoa mtoto wake auawe tena.
Michirizi ya machozi iliendelea kumtoka huku miguu ikiwa mizito kunyanyuka. Mkewe alimwona na kunyanyuka alipokuwa amejilaza na mtoto na kumfuata mumewe. Alimkumbatia na kumbembeleza huku akimpigapiga mgongoni taratibu.
“Mume wangu hii ni mitihani aliyotupa Mungu tunatakiwa kupambana nayo, tunatakiwa tumtegemee yeye kwa kila kitu na kumtumai kwenye majaribu mazito kama haya. Hakika tutashinda japo kukua mwenetu itakuwa sawa kabisa na ngamia kupita kwenye tundu la shindano. Lakini tukimuamini yeye lolote kwake linawezekana,” Ngw’ana Bupilipili alimpa moyo mumewe.
“Ni kweli la..la..kini...” Mathayo hakumalizia kutokana na donge la uchungu kumkaba kooni huku machozi yakimdondokea mkewe.
“Hakuna cha lakini tumuachie Mungu ndiye aliyetupa kiumbe huyu, mbona kuna viumbe wasio na faida duniani wanaishi kwa furaha itakuwa mwanadamu. Mungu atamlinda mwanangu nina imani atakuwa tu na siku moja kutoa ushuhuda hata kama wazazi wake tumetangulia mbele ya haki,” ngw’ana Bupilipili alizidi kumpa moyo mumewe.
“Nashukuru mke wangu kunipa moyo.”
“Ni wajibu wangu, basi wahi ukaandae chochote kitu njaa naisikia imeanza kunichonyota.”
Mathayo aliondoka kwenye maficho na kurudi nyumbani kumuandalia mkewe chakula kutokana na njaa kali iliyokuwa imemshika hasa baada ya kujifungua hakuwa ameweka kitu tumboni. Alipofika nyumbani alimchemshia uji na viazi ambavyo vilikuwa vimebaki jana yake. Haraka haraka alianza kurudi shambani. Hakufika mbali mvua kubwa ilianza kunyesha.
Hakukubali kusimama alitembea nayo huku akilowa kila kona ya mwili. Alipofika pangoni alimkuta mkewe akiwa amemkumbatia mtoto wake ambaye maji yalikuwa yameanza kuingia ndani ya pango.
Wasingeweza kutokana nje kutokana na mvua kuwa kubwa iliyokuwa ikiendelea kunyesha. Mathayo alipofika aliingia mule pangoni alipokuwa mke wake na kiza kilianza kutanda huku baridi likizidi kuwa kali.
Mvua nayo ilikuwa kama imetumwa ilizidi kuongeza kasi ya kunyesha ukiambatana na upepo mkali. Maji yakizidi kuingia kwenye pango, kila dakika yalizidi kujaa na kuelekea mafutini huku Ng’ana Bupilipili akimkumbatia mwanaye na kuendelea kumuomba Mungu asitishe mvua ile kwani haikuonesha dalili zozote za kukatika mapema.
Maji nayo yalizidi kupanda juu yalielekea kiunoni mvua nayo ndiyo kama imechochewa kuni jinsi ilivyokuwa ikinyesha kwa kasi huku upepo ukizidi kupiga.
Walifikiria watoke nje ili wakimbilie kwenye makazi ambako palikuwa mbali, waliamini wasingefika mbali kwani wangeweza kuuawa hata na radi ambayo ilikuwa ikipiga kwa nguvu na upepo mkali.
Nje kulikuwa hapatamaniki kutokana na ukali wa mvua na upepo mkali uliokuwa ukipiga baadhi ya miti iling’oka. Ilikuwa mvua ambayo haikuwahi kupiga muda mrefu kijijini pale.
Pangoni maji nayo yalizidi kujaa na yalivuka kiunoni kuelekea kifuani. Ilibidi mtoto wamweke mabegani, hawakuacha kumuomba Mungu kila dakika ili kuwanusuru na janga lile zito ambalo lilikuwa lina kila dalili za kuchukua uhai wao.
Mvua nje iliendelea kunyesha na maji nayo kila dakika yalizidi kujaa mule pangoni. Yalivuka kifuani na kuanza kuelekea shingoni, Mathayo na mkewe waliamini kabisa hakukuwa na dalili zozote za kutoka salama. Ila Mathayo alikumbuka huenda mvua ile ni laana ya kumficha mtoto wao albino ambaye alifahamika kama mkosi.
Wazo lake alifikiria kumtupa yule mtoto ili waangalie itakuwaje. Aliona ampe mkewe naye atapokeaje wazo lake.
“Mke wangu kuhusiana na mvua hii nilikuwa na wazo.”
Wakati huo walikuwa wamekumbatiana huku mtoto wao wamembeba kichwani japokuwa walianza kuchoka kutokana na kuiweka mikono juu kwa muda mrefu.
“Wazo gani mume wangu? Siamini kama tutatoka salama muda si mrefu maji yatatufunika. Ona sasa hivi yanakimbilia kidevuni...Eeeh, Mungu sikiliza kilio chetu waja wako,” ngw’ana Bupilipili hakuacha kumuomba Mungu muda wote.
“Mke wangu nina wazo moja, japo nina imani huenda usiliafiki. Lakini huenda ndilo litakalo yaokoa maisha yetu.”
“Wazo lipi mume wangu?” alisema huku akiyapuliza maji yaliyotaka kuingia mdomoni.
“Mimi nafikiria kabisa mvua hii si bure huenda tumevunja sheria ya mila na desturi.”
“Kuvunja kivipi?”
“Ni wazi huyu mtoto ni mkosi na hii mvua ni hasira ya mizimu.”
“Sasa hiyo hasira zao sisi inatuhusu nini?”
“Huenda wameamua kututia adabu kwa kiburi tulichokionesha kwao.”
“Sasa wewe ulikuwa na wazo gani? Naona muda si mrefu maji yatatufunika hata mikono imeishiwa nguvu kwa ajili ya kumshikilia mtoto kwa muda mrefu.”
“Kwa nini tusimtupe huyu mtoto?”
“Mume wangu unasemaje?” kauli ile ilimshtua Ngwa’na Bupilipili.
“Tumtupe huyu mtoto ili kuyaokoa maisha yetu.”
“Tukiisha mtupa tupata nini?”
“Nina imani kabisa mvua itakoma na sisi kuokoka.”
“Mume wangu maisha yako ni bora kuliko ya mtoto wetu?”
“Hapana mke wangu siku zote vitu vya jadi si vya kuvipuuza, matokeo yake leo tunakufa tunajiona.”
“Mume wangu kwa taarifa yako mtoto wangu siwezi kumtupa kama tutakufa basi tutakufa wote na kama kupona ni pamoja na mtoto wetu.”
“Mke wangu unafanya mzaha, tutakufa huku tunajiona.”
“Mume wangu hata siku moja siwezi kuua mwanangu ni mimi ndiye ninaye ujua uchungu wake. Kama tutakufa sawa lakini tukipona naomba uachane na mimi nitajua jinsi gani ya kuishi na mwanangu.” Ng’ana Bupilipili alimjia juu mumewe.
“Mke wangu kwanini hutaki kuwa mwelewa, mtoto nini? Tutatafuta mwingine lakini hatuwezi kuwa na bomu ambalo linatulipukia tumelikumbatia.”
“Kwani tatizo nini? We toka niache peke yangu nife na mwanangu. Kama kufa nitaanza mimi mwanangu kutafuata baada ya kufa mimi mama yake.”
“Mmh, sawa nitafanyaje nawe umekuwa mbishi.”
“Siamini kumbe nawe ni walewale basi wafuate ili waje wamchukue mtoto wangu wakamuue kama mlivyo muua mwanangu wa kwanza.” Ng’ana Bupilipili alisema kwa uchungu huku machozi yakimtoka, maji ya pangoni alikuwa ya baridi na kiza kinene kilitanda mule ndani kutokana na mvua ambayo ilianza kupunguza kasi yake. Lakini wingu lilikuwa bado zito likiambatana na baridi kali.
Waliendelea kuwemo mule pangoni, mtoto wao alikuwa bado yupo juu huku mikono yao kuzidi kuchoka. Nje mvua ilikuwa imekoma hata maji kuingia pangoni yalikoma, lakini bado maji yalikuwa chini ya kidevu.
Kutoka ndani ya pango ilikuwa vigumu kwa vile hapakuwa na sehemu ya kushika pia giza la mule pangoni liliwafanya wasione njia ya kutokea nje.
Waliendelea kukumbatiana huku baridi la maji kilizidi kuwapiga, Ng’ana Bupilipili alianza kutetemeka kwa meno kugongana.
“Mume wangu nasikia baridi kali sana pia nahisi mtoto ataponyoka muda si mrefu, mikono imeishiwa nguvu kabisa.”
Itaendelea...
Post a Comment