JAMANI DADA MARTHA LOOO!-23
www.facebook.com/2jiachieILIPOISHIA:
“Mungu wangu, atakuwa nani amejitoa ufahamu mpaka kuamua kugonga geti langu?” alijihoji Roi akiwa anatafuta namna ya kutoka kwa mama Anna.
JIACHIE MWENYEWE SASA...
Roi alijitoa, akavaa bukta na kwenda sebuleni. Lakini akili ikamwambia kwamba amalizane na mama Anna kwanza, atoke kisha yeye amfungulie Martha wayaongee na kuyamaliza...
“Atanielewa tu,” alisema moyoni Roi.
Alirudi chumbani, kweli alimalizana na mama Anna na akamtoa huku mwanamke huyo akiamini kwamba, Roi hatamudu kukutana kimwili tena na Martha labda mpaka waende kwake au kama watalala hapohapo, basi usiku sana.
Wakati Roi anamtoa mama Anna, alimuahidi kwamba, atampa pesa kwa ajili ya kupanga chumba Sinza kama walivyokubaliana.
“Poa baby,” alikubali mama Anna akiwa anatoka geti la uani ambalo lipo ubavuni mwa nyumba hiyo na kutokomea upande wa pili kwa nyuma.
Roi alirudi chumbani na kumpigia simu Martha.
Martha akiwa bado dukani baada ya kugonga sana geti, alishangaa kuona simu ya Roi, akaipokea haraka sana huku akisema moyoni...
“Utadhani alikufa sasa amefufuka. Ngoja nimsikilize. Si ajabu anajua mimi nipo nyumbani, hajui kama nipo getini kwake...”
“Haloo...”alipokea Martha...
“Ee, nilikuwa sebuleni, simu ilikuwa kwenye chaja chumbani. Si unajua sijabeba chaja kuja nayo huko...”
“Roi,” aliita Martha...
“Sema...”
“Una uhakika upo sebuleni?”
“Kha! Sasa nipo wapi kama si sebuleni? Au wewe upo sebuleni kwangu?”
“Mimi nipo nje kwako hapa. Na nimeambiwa mengi sana kuhusu wewe.”
“Mengi kama?”
“Wewe unajijua. Unajua uko wapi na nani! Kama kweli upo sebuleni toka unifungulie geti.”
“Poa,” alijibu Roi na kukata simu huku moyoni akisema...
“Haya ndiyo mambo nisiyoyataka. Anaanzaje kunikontroo wakati anajua mimi si mume wake?”
Martha, alikwenda getini na kupiga kambi hapo akisubiri kufunguliwa. Yeye alijua Roi hawezi kufungua na kama atafungua kweli basi atakuwa ameongozana na mama Anna.
Alishangaa geti limefunguliwa, Roi akiwa ndani ya bukta tu, tena akionesha hana wasiwasi wowote ule...
“Unajua nikiwa hapa nyumbani sipendagi kuacha geti wazi. Si unajua naishi mwenyewe?” alisema Roi akimbusu Martha ambaye alikuwa mbali sana kimawazo...
“Ina maana maneno ya muuza duka si ya kweli?” alijiuliza Martha akiwa hajui akubali au akatae.
Walizama mpaka sebuleni, Roi akakaa hapo kisha akamwambia Martha kama amefika kufanya usafi, aanze na chumbani.
Martha alisimama, akaenda chumbani. Lakini akashika mlango wa chumba cha kwanza, akaufungua, hakuona mtu, akashika mlango wa chumba cha pili, hakuona mtu, akaenda jikoni, hola. Akaenda stoo, hakuna kitu, akaenda chooni na bafuni hakukuwa na dalili ya kuwepo mtu...
“Mh! Basi yule kijana ni mwongo mkubwa. Afadhali hata ningemwona mwanamke, hata kama si mama Anna kuliko kutokuwa na mtu yeyote yule,” alisema moyoni Martha akiingia chumbani.
Sebuleni, Roi alikuwa kwenye kompyuta mpakato akibofyabofya huku akijivunia ushindi wake kwa mama Anna.
Martha alifanya usafi sehemu mbalimbali za nyumba hiyo hadi akafika sebuleni, kisha uani.
Alipofika uani, kwa mara ya kwanza alibaini kuwepo kwa mlango mdogo ambao mtu anaweza kutoka nje. Lakini ulikuwa umetiwa kufuli...
“Aa...aaaaa! mama Anna alikuwepo, ametokea mlango huu. Sasa nimejua,” alisema moyoni Martha huku hasira za wivu zikimpanda kama mwanamke.
Ili aujue ukweli alimfuata Roi sebuleni na kumwambia ampe funguo za mlango huo ili akatupe taka nje...
Kwa kujikaza sana, Martha alisema...
“Baby, naomba funguo za mlango wa uani. Nataka kutupa takataka.”
Roi naye alijua kimenuka au kitanuka, kwamba Martha atajua nini kiliendelea...
“Ooh! Baby, ule mlango tangu nimehamia nyumba hii haujawahi kufunguliwa na wala sijawahi kuona funguo yake. Pia kwa sababu ni uchochoroni sijawahi kutaka kuufungua,” alisema Roi kwa macho makavu kabisa.
Martha alikubaliana na utetezi wa Roi, moyo wake ukarejea katika hali yake ya kawaida.
***
Mama Anna alipotoka hapo, moja kwa moja alikwenda nyumbani na kuwasimulia wale mashoga zake, wapangaji wenzake kilichojiri nyumbani kwa Roi. Walicheka sana na kumshauri...
“Wewe usiwe mjinga. Pesa za kupanga za nini? Usipokee. Unachotakiwa kufanya wewe ni kung’ang’ania kuishi kule kwake. Mwambie wewe utakuwa unaishi kule yeye na Martha waishi hapa. Kwa hiyo akitoka kazini anakufuata kule. Mnajirusha halafu midamida anakuja huku,” alisema mmoja wa wanawake hao.
Mama Anna alikubaliana na ushauri huo kwani kwake aliuona kama ni wa kuweza kumfikuisha kwenye ndoa kabisa na kumpiku Martha.
***
Martha na Roi waliwasili nyumbani hapo, usiku wa saa tatu. Waliwakuta wapangaji wapo nje bado wakipiga domo licha ya kibaridi cha mbali.
Macho ya Martha yalitua kwenye sura ya mama Anna, akakasirika kwa mbali. Kilichomshtua zaidi Martha na gauni alilovaa mama Anna muda huo ndiyo lilelile ambalo aliambiwa na muuza duka kwamba, mwanamke aliyeingia na Roi ndani alikuwa amevaa...
“Inawezekana kweli mama Anna alikuwa amekwenda kula kwa Roi lakini labda hakukaa sana akatoka ila yule kijana wa dukani hakumwona ndiyo maana alijua bado yupo,” alisema moyoni Martha...
“Jamani za leo?” alisalimia Roi akiwa nyuma ya Martha wakiingia ndani...
“Nzuri tu za kwako shemeji?”
“Salama za kazi shemeji?”
“Salama za kazi honey,” alijibu mama Anna kwa sauti ya chini...
Je, nini kilitokea? Tukutane siku ya Jumanne wiki Ijayo hapa hapa
Share! share kutumiwa sehemu inayofuata kabla ya Jumanne!
Post a Comment