ad

ad

WANAOSUBIRI KUTOKA, KUINGIA OLD TRAFFORD HAWA HAPA

ZIMEBAKI siku chache tu kabla ya dirisha la usajili wa wachezaji katika majira ya baridi kuanza barani Ulaya.



Wakati klabu zinajiandaa kuingia sokoni mwezi ujao kusaka nyota wa kuongeza nguvu kwenye vikosi vyao, kuna baadhi ya wachezaji wa Manchester United hawajui hatima zao.
Kuna wasiwasi juu ya makinda wa klabu hiyo, Tyler Blackett, Reece James, Jesse Lingard, Paddy McNair na Andreas Pereira juu ya uwezekano wa kuendelea kubaki Old Trafford hasa kutokana na mikataba yao kubakiza miezi sita kufikia tamati.
 

Makinda wote hao watano mikataba yao inamalizika mwisho wa msimu na kama kutakuwa hakuna mpango wa kuwaongezea mikataba mipya, huenda Man United ikachukua uamuzi wa kuwapiga bei kwenye dirisha lijalo la uhamisho wa wachezaji kuliko kusubiri mwisho wa msimu na kuwashuhudia wakiondoka bila ya kuambulia kitu kama ilivyotokea kwa kiungo Paul Pogba.

Kwa siku za karibuni, kocha mkuu wa kikosi hicho, Louis van Gaal amekuwa akiwatumia makinda Blackett, Paddy McNair katika safu yake ya ulinzi baada ya kusumbuliwa na majeruhi wengi na Mdachi huyo anaweza akawapa ulaji mpya makinda hao.
Lingard pia alimwonyesha kiwango kizuri Van Gaal wakati alipoichezea timu hiyo kwenye mechi za kujiandaa na msimu mpya nchini Marekani kabla ya kupata majeraha yaliyomweka nje ya uwanja kwa sasa.

Van Gaal aliwapa nafasi makinda wote hao kuonyesha viwango vyao na kama wanastahili kuendelea kubaki kwenye hesabu za klabu hiyo ambayo imepania kujijenga upya na kurudisha makali yake.
Pereira ana umri wa miaka 18 tu na amekuwa mchezaji muhimu katika kikosi cha wachezaji wa akiba wa klabu hiyo ya Old Trafford.
Wakati dirisha hilo la usajili wa wachezaji likiwa limebakiza siku chache kuanza, kuna orodha ya wachezaji kadhaa watafunguliwa milango ya kutoka kwenye kikosi cha Man United na kuwapisha wengine wanaotajwa kutua klabuni hapo kwenye uhamisho huo wa Januari.
Wanaoondoka
Anderson
Kiungo huyo Mbrazili ameshindwa kuonyesha makali yake yaliyomfanya apate nafasi ya kusajiliwa na timu hiyo akitokea Ureno.

Anderson alicheza kwa kiwango kizuri msimu mmoja tu na baada ya kuvunjika mguu ameshindwa kurejea kwenye ubora wake na kuwashawishi makocha wa Man United.
Staa huyo alijikuta akitolewa kwa mkopo msimu uliopita wakati alipopelekwa Fiorentina, Man United ilipokuwa chini ya Kocha David Moyes.
Msimu huu alirudi Old Trafford na kukutana na kocha mpya, Louis van Gaal na Anderson ameshindwa kumshawishi Mdachi huyo na kuendelea kusugua benchi akiwa hajaonja utamu wowote wa kucheza kwenye Ligi Kuu England kwa msimu huu.
Ripoti za karibuni zinaweka wazi kwamba Man United ipo tayari kusikiliza ofa ya mchezaji huyo kama atatakiwa na klabu yoyote i na kuna uwezekano mkubwa akafungasha virago vyake usajili ujao.

Adnan Januzaj
Mmoja wa makinda wanaotajwa kuwa na kipaji kikubwa cha mchezo wa soka. Adnan Januzaj alipata nafasi na kuonyesha uwezo wake wakati Man United ilipokuwa chini ya Moyes.
Kocha Van Gaal alijaribu kumpa nafasi mchezaji huyo wa kimataifa wa Ubelgiji kabla ya kuonekana kwamba hawezi kuendana na mfumo wake licha ya kwamba majeraha yalichangia kumfanya asugue benchi kwa sasa.
Kutokana na hilo, Man United bado inahitaji huduma ya mchezaji huyo na ilichopanga ni kumtoa kwa mkopo katika usajili ujao ili akaongeze ukomavu kabla ya kurejea kugombea namba katika kikosi hicho cha Old Trafford.
Anders Lindegaard
Kipa huyo raia wa Denmark mambo yake hayapo vizuri klabuni hapo. Kitu kibaya kwa Lindergaard ni kwamba kipa namba moja, David De Gea amekuwa akiongezeka kiwango kila kukicha na kutishia kabisa uwezekano wa kipa huyo ambaye ni namba mbili kwa sasa kupata nafasi.
Kocha Van Gaal pia anaonekana kuwa hana mpango na Lindergaard na kufikiria kufanya usajili mpya kwenye nafasi ya kipa kitu ambacho kinamfanya staa huyo wa Denmark kusaka timu nyingine ya kujiunga nayo wakati dirisha lijalo la usajili litakapofunguliwa.
Watakaotua

Kevin Strootman, AS Roma
Kiungo huyo Mdachi amekuwa kwenye rada za Van Gaal kwa muda mrefu na hilo linachochea uwezekano wa kujiunga na miamba hiyo ya Old Trafford mwezi ujao.
Strootman ni kiungo mwenye nguvu na uwezo wa kucheza uwanja mzima, goli hadi goli na kwenye hilo Van Gaal anashawishika zaidi kumsajili kuliko Sergio Busquets.
Strootman anaweza kurudisha makali ya kiungo ya kikosi cha Man United ambayo yamepungua uwezo wake kwa miaka ya karibuni tangu alipoondoka Roy Keane. Kuna uwezekano mkubwa akajiunga na miamba hiyo ya Ligi Kuu England mwezi ujao.
Mats Hummels, Borussia Dortmund
Beki huyo Mjerumani kwa msimu huu hana raha kabisa kwenye klabu yake Borussia Dortmund kutokana na kuboronga kwenye Ligi Kuu Ujerumani.
Kwenye fainali za Kombe la Dunia 2014 zilizofanyika Brazil, Hummels alicheza kwa ubora mkubwa na kuisaidia Ujerumani kubeba ubingwa huo, lakini aliporejea katika klabu yake mambo yamekuwa mabaya na Dortmund kwa sasa inakamata nafasi ya pili kutoka mwisho katika msimamo wa Bundesliga.
Kocha Van Gaal anahitaji kumaliza tatizo kwenye safu yake ya ulinzi na anamtambua Hummels kuwa ni chaguo lake la kwanza katika nafasi hiyo ya ulinzi na atahakikisha anainasa saini kwenye uhamisho ujao.
Sergio Busquets, Barcelona
Mambo yamegeuka katika kikosi cha Barcelona kutokana na kuwekwa kando mara kadhaa kwenye kikosi cha kwanza cha timu hiyo ya Nou Camp.
Kutokana na hilo, kiungo huyo wa kati ameamua kufungua milango ya kutaka kuhama na Old Trafford panatajwa kuwa ni mahali atakapokwenda kutua wakati wa dirisha la usajili ujao litakapofunguliwa mapema mwezi ujao.
Van Gaal akifanikiwa kuinasa saini yake atakuwa amefanya usajili wa maana kwa kumnasa kiungo mwenye uwezo wa kufanya kazi ya kukaba kuwalinda mabeki na pia kupiga pasi za maana zitakazoifanya miamba hiyo ya Old Trafford kuwa na nafasi kubwa ya kutawala katika sehemu ya kiungo.
 Victor Valdes, huru

Kwa sasa kipa huyo Mhispaniola hana timu baada ya kuondoka Barcelona mwishoni mwa msimu uliopita. Baada ya kukaa nje ya uwanja kwa muda akiuguza majeraha yake, Valdes amepona na kurejea uwanjani aliomba nafasi ya kufanya mazoezi Man United na anatajwa kwamba atajiunga na miamba hiyo ya Ligi Kuu England mwezi ujao.

Kocha Van Gaal anamtazama Valdes kuwa ni kipa atakayeweza kumfanya De Gea kupandisha kiwango chake zaidi kutokana na hofu ya kupoteza namba yake kwenye kikosi hicho.

Ron Vlaar, Aston Villa

Kocha Van Gaal anasaka beki wa kati kwa nguvu zote. Kwenye orodha ya mabeki anaowataka wametajwa wengi, lakini Mdachi Vlaar ni mmoja wao.

Van Gaal anafahamu vizuri namna ya kumtumia Vlaar baada ya kuwa naye pamoja kwenye fainali za Kombe la Dunia 2014 zilizofanyika nchini Brazil ambapo Uholanzi ilimaliza nafasi ya tatu.

Vlaar anaweza kupatikana kirahisi kutokana na mkataba wake klabuni Aston Villa kufikia tamati mwishoni mwa msimu huu.

No comments

Powered by Blogger.