BABA KIUMBE WA AJABU - 06
MTUNZI: ALLY MBETU
Endelea kulike: www.facebook.com/2jiachie
Tembelea: www.2jiachie.com
“Masalu unajua nakupenda sana kuliko watoto wangu wote.”
“Najua baba.”
“Hebu niambie unataka nini nikufanyie ili ujue napenda sana.”
“Cha kwanza kunipa nafasi ya kurudia masomo niliyoanguka katika mtihani wangu ili nifanye vizuri, bado nina hamu ya kuendelea kusoma.”
“Tofauti na hilo?”
“Siwezi kusema kwa sasa mpaka nitakapofanya mtihani wangu wa marudio.”
“Masalu, kusoma si muhimu sana kwako, kama pesa zipo nitakufungulia mradi wako ili uendeleze maisha yako.”
“Lakini...”
“Masalu hakuna haja ya kubishana, naomba ujiandae kuna duka moja nimelifungua na kuanza kazi wewe ndiye msimamizi mkubwa.“
Nilijikuta nakosa cha kuzungumza na kukubaliana na baba japo nafsi yangu ilitaka kusoma ili nimkomboe mama yangu. Nilijua kukubali mradi ule japo utakuwa chini yangu bado utakuwa wa nguvu za kishirikina kwa kuhofia huenda siku za mbele baada ya kuoa na kupata mtoto akatolewa kafara.
Baba alinitolea hati za kumiliki duka lile lenye jina langu na kunionesha sehemu ya kusaini. Nilisaini na kuniahidi kunifanyia mambo makubwa kuliko ndugu zangu wote. Baada ya kutoka pale aliniingiza kwenye gari lake na kunipeleka mjini Barabara ya Pamba kwenye duka langu.
Nililikuta duka lipo wazi na watu wakiendelea na mauzo ya vitu, lilikuwa duka kubwa la kuuza vitu vya jumla na rejareja. Tulipofika dada mmoja ambaye alikuwa akinifahamu aliniuliza:
“Leo Masalu ndiyo umeamua kuja?”
“Alikuwa anamalizia masomo,” baba alijibu.
“Karibu bosi.”
“Asante.”
Nilijibu huku nikiingia dukani na kwenda kukaa kwenye kiti changu kilichoandaliwa kwa ajili ya kukalia niwapo kazini. Baada ya kukagua duka lililokuwa likilingana na maduka ya ndugu zangu, baba aliondoka na kuniacha nisimamie duka langu.
Alinipitia jioni na kunirudisha nyumbani, nilipofika nyumbani nilimueleza mama kuwa nimepewa duka na baba. Ajabu mama badala ya kufurahi alitokwa na machozi, kwa vile tulikuwa peke yetu nilimuuliza:
“Mama unalilia nini?”
“Mmh, najua hukufurahi na unaweza usifurahi.”
“Kwa nini mama?”
“Ni vigumu kunielewa kwa sasa lakini tumuombe Mungu aepushe mbali.”
“Mama mbona sikuelewi?”
“Suala la shule limeishia wapi?”
“Baba amekataa na kusema tayari ameishanifungulia duka, na leo ndiyo nimekabidhiwa rasmi.”
“Mmh! Haya”
“Kwani kuna nini?”
“Hakuna ubaya.”
“Mama kuna kitu hutaki kuniambia.”
“Hakuna kitu kikubwa zaidi ya kukatika kwa ndoto yako ya kusoma.”
“Mama nitasoma tu.”
“Kwa duka lako, si unawaona ndugu zako walivyo bize na maduka yao hata muda wa kunikumbuka hawana.”
“Mama nitajipanga, siku hizi kuna masomo ya jioni.”
Siku zilikatika, biashara nayo ilizidi kushika kasi, hata mwili wangu ulibadilika na kuonekana mtu mzima kutokana na kunenepa, hata sauti yangu ilibadilika. Lakini ilikuwa tofauti na wenzangu, mimi nilibakia nyumbani na mama pamoja na mfanyakazi mmoja, niliamua kumpumzisha mama kazi za shamba, lakini mama aling’ang’ania kwa kusema kama akiacha kwenda shamba atafukuzwa na baba.
Nilipomuuliza baba naye alinijia juu na kunionya nisiingilie mambo yake, sikuwa na jinsi, nilimuacha mama aendelee kulima huku nikitumia vijana kumsaidia mama, ambaye alifanya kazi ndogondogo. Kingine ambacho sikukubaliana na baba ni kuhusu mavazi ya mama yaliyokuwa yamechoka.
Hapo sikukubali hata kidogo na nilikuwa tayari kwa lolote.
“Masalu unataka tubishane?” baba alinikaripia.
“Kwa hili baba sikubaliani nawe hata kidogo.”
“Umeanza kuvimba kichwa kwa vipesa unavyopata?”
“Si kuvimba kichwa, nipo sahihi, kama mali zako chukua lakini nimechoka kuiona hali hii mpaka lini?”
Sikuogopa chochote cha baba mpaka tulipokubaliana kumnunulia mama nguo mpya, pamoja na mzozano huo bado baba hakuonekana kukasirika sana. Mama alibadilika na kuanza kuvaa vitenge vya gharama, hata kandambili alivaa mpya.
Ndugu zangu walipokuja nyumbani hawakuamini kumkuta mama yetu kapendeza. Walipomuuliza aliwaeleza ni kwa ajili yangu, walinifuata kutaka kujua nimewezaje kumbadili baba kukubali mama kuvaa nguo mpya. Niliwaeleza ni msimamo hakuna kitu kingine, maisha yaliendelea.
Katika vitu ambavyo baba alinionya ni kutembea na wanawake, nilikumbuka kauli za dada Monika kuwa alianza kuelezwa asijihusishe na wanaume na mwisho alipata kidonda cha kichawi.
Nilimkubalia kumridhisha tu, lakini niliendelea kuwa na uhusiano na binti mmoja ambaye ndiye tuliyepanga kuoana siku za mbeleni. Siku zote mambo yangu nilikuwa nayafanya kwa siri kubwa bila baba kujua kwa kuamini sina uhusiano wa kimapenzi na mwanamke.
****
Siku moja nikiwa nimelala niliota kitu kama nyoka, lakini sikukielewa vizuri kikiniuma kwenye mguu wa kulia kwa ndani. Nilishtuka lakini hakukuwa na kitu chochote, niliendelea kulala. Kesho yake nilikwenda dukani kama kawaida na kuendelea na shughuli zangu.
Wiki moja baadaye nilianza kusikia muwasho sehemu niliyoota nimeumwa na kitu kama nyoka. Nilimueleza mama asubuhi baada ya kujikuna mpaka kukaleta weusi sehemu iliyokuwa ikiniwasha. Mama alishtuka, jambo lililonitisha.
”Mama mbona umeshtuka?”
“Baba yako alikueleza nini?”
“Kuhusu nini?”
“Huo muwasho wako?”
“Hata, sijazungumza lolote.”
“ Mmh!” Mama aliguna.
“Unaguna nini?” nilimuuliza.
“Hapana.”
“Mbona kama unanitisha, unakuwa hauna tofauti na wa dada Monika?”
“Ni kweli.”
“Unataka kuniambia ndiyo huu?”
“Ndiyo.”
“Mungu wangu nimekwisha.”
“Wala hujaisha, ukifuata masharti yake hauna tatizo.”
“Kwa hiyo na mimi nitakuwa na kidonda kama dada Monika?”
“Ndiyo lakini hakiumi.”
“Na nikikosea nitakufa kama dada Monika?”
“Monika kafa na yake.”
“Mamaa, juzi tulizungumza nini, leo unanibadilikia?” Nilimuona mama akitaka kuficha mambo.
“Masalu nakuomba suala hili muulize baba yako na usimueleze kuwa tumezungumza.”
“Sawa mama.”
Niliachana na mama huku mwili wote ukininyong’ea kwa kujua niliyoelezwa na dada Monika yametimia.
Siku ile hata hamu ya kwenda kwenye duka langu sikuwa nayo, kwa kuamini nilikuwa nimeishaharibika. Nilishinda ndani huku nikilia lakini mama alitumia muda wake kunibembeleza kuwa sijaharibika kama ninavyo fikiria.
“Masalu usilie mwanangu.”
“Mama kwa nini mnanitendea unyama kama huu kosa langu nini?”
“Huna kosa mwanangu, kidonda hiki humfuata yule aliyeteuliwa na mizimu.”
“Wataniteua vipi wakati mimi sitaki?”
“Huwezi kukataa.”
“Mama nina malengo yangu wewe unajua.”
“Ni kweli, lakini hakuna wa kumzuia baba yako uamuzi wake.”
“Mama na mimi nitakufa kama dada Monika?”
“Kwa nini?”
”Siwezi kufuata masharti ni magumu.”
“Si magumu ukizingatia.”
“Siwezi mama siwezi...,” nilikatwa kauli na sauti ya baba aliyekuwa akimwita mama. Nilimuona mama akishtuka na kuanza kutetemeka na kijasho chembamba kilimvuja.
“Mama vipi?”
“Naomba usimwambie baba yako niliyokueleza, ataniua.”
“Siwezi kumwambia.”
“Ng’wana Manoni.”
“Lama,” mama aliitikia huku akitoka chumbani kwangu.
“Vipi mbona unatoka chumbani kwa mtoto?”
“Hajisikii vizuri.”
“Na shamba hujaenda?”
“Baba Mihayo nimwache Masalu anaumwa niende shamba?”
“Kwani anaumwa sana?”
“Toka asubuhi analia tu.”
“Kafanya nini?”
“Mmh, nenda ndani ukamuone.”
“Masalu,” baba aliniita.
“Naam baba.”
“Eti kuna nini?”
“Kuna vitu ambavyo sielewi.”
“Vitu gani?” Baba alisema huku akiingia ndani.
Alipoingia ndani alinikuta nimeshikilia mguu.
“Kuna nini?”
“Baba sehemu hii inaniwasha sana kufikia hatua ya kunikosesha raha.”
“Hebu nione,” nilimuonesha baba, baada ya kuona alisema:
“Kumbe hiki?”
“Ndiyo baba.”
“Sasa tatizo nini?”
“Kinaniwasha.”
“Usikikune kitapoa chenyewe.”
“Hapana baba bora niende hospitali.”
“Masalu usiende hospitali, ugonjwa juu si wa kawaida.”
“Wa nini?”
“Utajua tu baadaye, lakini chonde usiende hospitali.”
“Au ndiyo kama wa dada Monika?”
“Eti?” Kauli yangu ilimshtua baba na kunitazama mara mbili kama ndiyo siku yangu ya kwanza kuniona.
“Eti umesemaje?”
“Baba mbona umeshtuka hivyo?”
“Sijakuelewa, hebu rudia swali lako.”
“Nauliza, kisiwe kidonda kama cha dada Monika.”
“Mama yako ndiyo kwakwambia? Leo atanitambua,” baba alikuja juu.
“Baba badala ya kunijibu swali langu unakimbilia kutaka kumpiga mama au ndiyo umemuona gunia lako la mazoezi,” nilizidi kumchanganya baba na maneno yangu ambayo hakufikiria hata siku moja nitayatamka.
“Masalu mbona unanikosea heshima?”
“Sijakukosea heshima ila nataka kujua ukweli wa muwasho huu kwa vile nilibashiliwa kipindi kirefu.”
“Na nani?”
“Na dada Monika”
“Alikubashiria nini?”
“Alinieleza kuwa kifo chake kimetokana na kukikataa kidonda hiki, na ulichomuahidi ndicho kilichotokea.”
“Muongo, unamsingizia Monika wakati uongo wote kakupa mama yako.”
“Baba utamuonea mama bure, mama hajanieleza chochote zaidi ya kunifanya mtoto mdogo mambo ninayoyajua.”
“Mambo gani?”
“Kuhusu chanzo cha utajiri kidonda cha dada Monika mpaka kifo chake kilisababishwa nini na utabiri wake kidonda kikitoka kwake kinakuja kwangu.”
“Mmh,” baba aliguna, kisha alinitazama kwa muda na kuangalia juu kabla ya kushusha tena pumzi.
“Masalu.”
“Naam.”
“Niambie ukweli mama yako kakuambia nini juu ya huu muwasho?”
“Kaniambia ni muwasho wa kawaida, utapoa wenyewe.”
“Hakukuambia kitu kingine?”
“Hajaniambia, ndiyo maana nilijua ananidanganya, dada Monika alinipa siri nyingi, zingine hata mama hajui na bahati mbaya wakati anakufa nilikuwa mbali lakini kuna mengi mazito alitaka kunipa juu ya familia yetu.”
“Monika alikuambia nini?”
“Alinieleza jinsi kidonda chake kilivyoanza kama muwasho na mwisho kilikuwa kidonda kisichouma zaidi ya kutoka maji na kukatazwa asiyafute.”
“Mmh, pamoja na uongo wake nakuomba usimuamini ni mfitini yule.”
“Baba unataka kunihakikishia kidonda hiki sio kama cha dada Monika?”
“Nimekueleza usimfuate Monika ni muongo.”
“Kama muongo naomba na mimi uniondolee masharti ya kuwa na mke.”
“Masalu, umri wako bado.”
“Baba mimi si mdogo, ukweli ni kwamba huu muwasho mwisho wake ni kidonda ambacho kitaingiza pesa kwa njia ya kumwagika maji. Baada ya dada Monika kuyashindwa masharti yako uliamua kumuua na mimi nahofia utaniua.”
“Narudia tena kukueleza Monika ni muongo.”
“Baba nasema kama ndicho kidonda hiki basi nami nitakufa kama dada Monika.”
“Masalu kuna sababu ya kuzungumza kwa kituo.”
“Sawa baba lakini kaa ukijua kama muwasho huu mwisho wake ni kidonda cha utajiri sikitaki nakuomba unirudishe shuleni.”
“Nikurudishe shuleni fedha za shule utazipata wapi?”
“Kwani lazima nipate kidonda ili nisome?”
“Utasoma, lakini kumbuka fedha zinatafutwa na njia zake pesa zipo nyingi.”
“Moja wapo ni kidonda changu?”
“Masalu tutazungumza, hebu vaa kuna mali mpya nimeituma dukani mwako twende ukaiangalie.”
ITAENDELEASIKU YAKESHOOOOOOOOOOO

Post a Comment