ad

ad

BABA KIUMBE WA AJABU - 05


MTUNZI: ALLY MBETU
Endelea kulike: www.facebook.com/2jiachie
Tembelea: www.2jiachie.com

Mama anateseka dada Mihayo anamhonga bwana wa pembeni gari, Masalu inauma lakini sina uwezo. Kama kidonda hiki angekuwa nacho mtu mwingine na mimi kuwa na uwezo wa dada Mihayo hata kwa kutoa kafara ya mtoto mama yangu angeishi kama malaika.
Lakini sina uwezo, hata hiki kidogo ninachokipata nikimpelekea mama hatakitumia zaidi ya kugeuzwa ndondocha na baba.”                                                             
Kila nilipoyakumbuka maneno ya dada nilijikuta nikitokwa na machozi. Nilikumbuka neno moja ambalo dada Monika alinieleza nilifanyie kazi, aliniambia:
“Masalu, mchunguze mama muda mwingi akiwa peke yake mkono huwa shavuni, na kama utamfuatilia kwa muda baada ya kutoa mkono shavuni hutikisa kichwa na kufuta machozi. Katika maisha yetu toka tupate utajiri wa kishirikina furaha ya mama imetoweka, kutabasamu kumekuwa kama ajali lakini kulia kumekuwa kitu cha kawaida.
Mara nyingi mama amekuwa kila akiwa peke yake kanga huwa mkononi ili kufuta machozi. Vitu vile nilivifanyia kazi na kumueleza dada Monika yote aliyonieleza ni kweli. Aliniuliza swali lingine:
“Masalu umeshawahi kumuona mama akivaa nguo mpya?”
“Hapana,” nilimjibu.
“Hebu jifikirie mama yetu ni wa kuvaa nguo zilizoachwa na wanaye?”
“Nilikuwa sijui.”
“Kama hujui, hata macho yako hayaoni? Masalu sasa hivi wewe si mtoto unaona vitu ambavyo baadaye vinataka majibu kwa kile ulichokiona.”
“Huwezi kuamini dada nilikuwa kama nimefungwa akili, unachonieleza sasa hivi ndiyo kama kwangu kunapambazuka baada ya kukaa gizani kwa muda mrefu. Kama usingenieleza haya ningekufa kibudu.”
Niliamini kabisa kama dada Monika kweli amekufa, basi alikuwa amekufa na mengi moyoni sawa na samaki mwenye mengi ya kuzungumza lakini kila alipofumbua mdomo maji yalimjaa mdomoni. Kama alivyonieleza shemeji kabla ya kufa kutokana na maelezo yake mengi angenieleza mengi mazito.
                                                        ****
Tulipofika shambani mama hakuonesha kama anataka kulima, aliniweka chini ya mti huku akionekana mwingi wa mawazo. Baada ya ukimya mfupi mama aliniita jina langu.
“Masalu.”
“Naam mama.”
“Najua umesikia mengi juu ya maisha yetu, lakini hakuna ukweli kwa yote uliyosikia nakuomba uwapuuze, sawa baba.”
“Lakini mama mbona yote niliyoelezwa yana ukweli.”
“Ukweli upi?
”Mama kwanza naanza na wewe, toka nipate akili sijawahi kukuona ukifurahi, kila siku mtu wa masikitiko na kutokwa na machozi.”
“Ha! Masalu umejuaje?”
“Mama dada Monika kanieleza mambo mengi sana ambayo niliyafanyia kazi na kuupata ukweli juu yako.”
“Ukweli gani?”
“Kuhusu muda mwingi kuweka mkono shavuni na kutokwa na machozi, nilikufuatilia bila wewe kujijua na kuupata ukweli, pia uvaaji wako wa nguo mama toka nipate akili sijakuona ukivaa nguo mpya au nzuri, pia mama hebu angalia ndala zako. Kwa maisha tunayoishi wewe si wa kuvaa ndala za kufunga na waya.”
Niliposema vile mama alijiangalia kama hakujua alichokivaa wakati wa kutoka nyumbani.
“Mama najua yote haya yanatokea kwa ajili ya nini.”
“Kwa ajili gani?”
“Haya ni mateso anayokupa baba, baada ya kutengwa na ndugu zako, na chanzo cha yote ni yeye. Kutokuwa na ukaribu na familia yako, katumia ni fimbo ya kukuadhibia. Hivi mama hata wanao wengine wanajijali wao na kukusahau , bila wewe wangeijuaje dunia?
“Mama maisha haya unayoishi siyo mazuri, nilisikia eti baba alikutishia maisha kama utataka mambo makubwa. Haya ndiyo aliyoyakataa dada Monika kidonda akitunze yeye wengine wale maisha mazuri. Matokeo yake mnaamua kumuua na kuificha maiti yake.”
“Masalu nani kaificha maiti ya Monika?”
“Ipo wapi?”
“Masalu swali gani hilo, kila anayekufa si huzikwa?”
“Mbona mtoto wa dada Mihayo hakuzikwa?”
“Masalu una uhakika gani?”
“Dada Monika hakunificha yote nisemayo ni yeye aliyeniambia ni mengi sana nayajua kuliko mtu mwingine.”
“Masalu yote usemayo ni kweli, nakuomba usimwambie mtu yoyote habari hizi.”
“Kama ni kweli naomba kuanzia leo kazi ya kulima aachiwe mtu mwingine, uvae nguo nzuri ili ulingane na utajiri wa familia yetu.”
“Masalu hilo haliwezekani.”
“Kwa nini?”
“Baba  yako ataniua, naomba mwanangu yote unayoyaona yaache kama yalivyo, na ukizidi kumchokonoa anaweza kukuua.”
“Kama alivyomuua dada Monika?”
“Usiseme hivyo Masalu.”
“Mama tunafichana nini? Hivi utajiri ndiyo unaotufanya tukose huruma kwa wenzetu?”
“Masalu nakuomba usichimbe sana.”
“Hapana mama, huwezi kujua sasa hivi tunaonekana vipi mbele ya macho ya watu, kwa taarifa yako inasemekana Monika hajazikwa amewekwa ndani kwa imani za kishirikina.”
“Nani kasema?”
“Aliyekuwa akikaa na dada Monika ndiye anayeeneza habari hizi.”
“Yeye kajuaje?”
“Mama ina maana ninapozungumza na wewe unakuwa wapi? Nilikueleza kuwa kabla ya kufa dada Monika alimpa siri kubwa ya maisha yetu na sababu ya kifo chake. Pia alimueleza kuwa alikuwa na siri nzito ambayo asingemwambia mtu zaidi yangu mimi.”
 “Mmh, sasa huyo kijana kinamhusu nini kututangaza vibaya?”
“Kinachomuuma ni kumuulia mtoto wake asiye na hatia.”
“Hivi baba yako akijua kuwa ndiye anayetutangaza vibaya kwa watu kutakuwa na usalama kweli?”
“Atamfanya nini?”
“Masalu wee acha baba yako hana dogo, anaweza hata kumkata kichwa.”
“Akimuua atapata faida gani? Si ndiyo atakuwa anaongeza chuki kwa watu?”
“Masalu mwanangu, kwa umri wako hata nikueleza kitu hutanielewa, nakuomba kila ulilosikia liache lilivyo, wewe bado mtoto mdogo litakuchanganya.”
“Sawa nimekuelewa, ila naomba ukweli wa jambo moja.”
“Jambo gani?”
”Kuhusu ukweli wa dada Monika.”
“Ukweli upi?”
”Ni kweli amekufa?”
“Ndiyo.”
“Amezikwa wapi?”
“Mmh! Si makaburini.”
“Makaburini gani?”
“Kwa kweli siwezi kujua makaburi gani sikwenda kuzika.”
“Mama kuna makaburi tofauti na tuliyoyazoea?”
“Hakuna.”
“Na misiba yote huanzia kanisani kisha kupelekwa kuzikwa?”
“Ndiyo.”
“Sasa msiba wa dada Monika mliupeleka kanisa gani?”
“Masalu hata ukijua itakusaidia nini?  Aliyekufa amekufa huwezi kumfufua.”
“Hata kama siwezi kumfufua, dada Monika ndiye kipenzi changu, kaburi lake kwangu ni kielelezo cha kumuona kipenzi changu.”
“Masalu nakuomba suala hilo uachane nalo.”
“Yote nitaachana nayo si la dada Monika.”
“Masalu ukitaka kujua mengi utakosana na baba yako.”
“Kwa hiyo ukweli dada Monika maiti yake haikuzikwa?”
“Masalu nakuomba mwanangu chondechonde achana na hayo ili maisha yako yawe salama.”
“Kwa hiyo nikitaka kujua baba ataniua?”
“Hawezi kukuua ila utakuwa matatizoni.”
“Mmh! Sawa mama,” nilikubali kwa shingo upande kutokana na kuonekana kumuweka mama katika wakati mgumu.
Sikutaka kumsumbua sana mama yangu kutokana na maelezo ya dada Monika, kila nilipomtazama nilimuonea huruma. Nilimuahidi mama toka moyoni mwangu sitaulizia lolote kuhusiana na dada Monika wala kitu chochote kuhusiana na familia yetu.
Kauli yangu ilimfurahisha mama na kuonekana hawezi kuamini nilichokisema.
“Kweli Masalu.”
“Kweli mama, nakupenda sana mama yangu.”
“Asante Masalu, nakuomba kila unachokijua huenda hata mimi mama yako sivijui kwa vile baba yako alimpenda sana Monika hata siri zingine sizijui ambazo alikueleza wewe na pengine kabla ya kufa angekueleza,” maskini mama yangu alisema huku akitokwa na machozi, kitu kilichozidi kuniumiza nami machozi yalianza kunitoka kwa mbali.
“Nimekuelewa mama yangu, nimekuelewa sina budi kukusikiliza.”
“Asante Masalu, siku zote niliamini wewe na Monika ndiyo watoto wangu wanaonijali, endelea kunijali mwanangu wewe ndiye tegemeo langu, soma unikomboe.”
“Nitafanya hivyo mama yangu, nakuahidi kuwa kimbilio lako.”
“Asante mwanangu.”
Baada ya mazungumzo marefu tulirudi nyumbani, lakini  bado aliniacha na maswali lukuki moyoni mwangu, nilijikuta nakubaliana na shemeji, bwana wa Monika kuwa mwili wa dada umefichwa ndani pamoja na mtoto wa dada Mihayo.
                                                SIKU TATU BAADAYE
Siku tatu baadaye nilipata taarifa za kusikitisha za kifo cha utata cha shemeji aliyekuwa bwana wa Monika. Taarifa zilizonitisha na kuamini mazungumzo yangu na mama juu ya taarifa zinazosambazwa na shemeji zilimfikia baba na kuamua kufanya umaruhuni wake.
Ndugu walisema aliporudi nyumbani alianza kusema anasumbuliwa na kichwa huku akisema kama akifa atakuwa ni baba. Na usiku alipiga kelele akilitaja jina la baba, kitu kilichozidi kuaminisha kwamba anahusika moja kwa moja ili kumkomoa baada ya kusikia akitutangazia sifa mbaya familia yetu.
Kifo kile kiliongeza sifa mbaya kufikia hatua familia ya aliyekuwa mpenzi wa marehemu dada Monika kuja kutushambulia kwa maneno ya kutuita wachawi. Siku hiyo nilikuwepo, mama wa marehemu alikuja nyumbani na kuanza kutoa shutuma nzito kwa sauti ya juu huku watu wakisikiliza.”
“Mmeniulia mwanangu kwa imani zenu za kichawi ili muwe matajiri, kumuua mtoto wa Mihayo hamkuridhika mmemuua Monika na kumficha ndani bado tu mmeona haitoshi mmemuua mwanangu. Nawaambia damu ya mwanangu haiendi bure.”
Taarifa zile zilipelekwa kwa baba ambaye aliita polisi na kumchukua yule mama na kumpeleka kituoni. Kwa kweli kilichoendelea sikujua zaidi ya kumsikia baba akitamba atamuonesha. Pamoja na yule mama kupelekwa polisi familia yetu ilitawaliwa na sifa mbaya ambazo wengi walizisikia na kuzisambaza kwa watu kuwa maisha yetu yametawaliwa na utajiri wa kishirikina ambao ulikuwa ukipitia kwenye kidonda cha marehemu dada.
Nilijikuta nikiishi maisha ya kukosa amani, hata tembea yangu ilikuwa ya mashaka kwa kuhofia maneno ya watu. Siku zilikatika walisema mchana, usiku wakalala. Walizungumza sana mwisho wakanyamaza na kusahaulika na maisha yakaendelea.
Katika maisha yetu hakuna kilichobadilika, nilimaliza kidato cha nne kwa kupata matokeo mabaya. Niliamini kufanya vibaya kulitokana na migongano ya mawazo iliyotokana na kuchanganywa na mambo yote yaliyotokea yakihusu familia yetu, na taarifa nilizopewa na dada Monika juu ya kifo chake na matukio mengi ya kishirikina yaliyoilenga familia yetu.
Wazo la kurudia mtihani wa kidato cha nne, lilipingwa na baba na kusema atanipatia shughuli nyingine. Roho iliniuma kwani ndoto zangu zilikuwa kusoma kwa bidii ili siku moja nimkomboe mama kwenye mateso ya kuwekwa kifungoni na baba.
Miezi sita baada ya matokeo mabaya ya kidato cha nne, baba alionesha mapenzi makubwa kwangu tofauti na zamani. Alifikia hatua ya kuzunguka nami kila kona kwenye shughuli zake. Siku nyingine alinipa pesa za matumizi ambazo alinieleza ninunue kitu chochote nikitakacho.
Kwa akili za kitoto nilianza kubadilika na kuyaona yote niliyoelezwa juu ya ukatili wa baba ni uongo. Baba alikuwa mtu mzuri kwa kuninunulia nguo za thamani, nilionekana kweli mtoto wa mtu mwenye pesa tofauti na mwanzo nilivyokuwa nasoma shule.
Baba siku zote alinisifia kuwa mimi ndiye mtoto anipendaye kuliko wote, kauli zile za baba zilinifanya nisahau hata wazo la kumuuliza juu ya dada Monika. Siku moja tulikuwa tumekaa kwenye moja ya hoteli ya baba huku akiniruhusu kula nikitakacho, baada ya chakula baba alinichukua na kuingia naye kwenye ofisi yake iliyokuwa ndani ya hoteli ile ambayo sikuwahi kuingia siku za nyuma.
Baada ya kuingia ofisini baba aliendelea kunimwagia sifa.
“Masalu unajua nakupenda sana kuliko watoto wangu wote.”
“Najua baba.”
“Hebu niambie unataka nini nikufanyie ili ujue napenda sana.”
“Cha kwanza kunipa nafasi ya kurudia masomo niliyoanguka katika mtihani wangu ili nifanye vizuri, bado nina hamu ya kuendelea kusoma.”
“Tofauti na hilo?”
“Siwezi kusema kwa sasa mpaka nitakapofanya mtihani wangu wa marudio.”
“Masalu, kusoma si muhimu sana kwako, kama pesa zipo nitakufungulia mradi wako ili uendeleze maisha yako.”
“Lakini...”
ITAENDELEA SIKU YAKESHOOOOOO

No comments

Powered by Blogger.