ad

ad

BABA KIUMBE WA AJABU - 04

  
MTUNZI: ALLY MBETU
Endelea kulike: www.facebook.com/2jiachie
Tembelea: www.2jiachie.com
“Masalu unataka kuniambia hukuwa na habari Monika amekufa au ulitaka kunitega akili?”
“Shemu, huwezi kuamini kila dakika nimekuwa nikichanganyikiwa juu ya taarifa za msiba wa dada Monika. Kweli niliuona mwili ukiteremshwa kwenye gari. Lakini tokea hapo sikuweza kujua nini kilichoendelea mpaka leo hii.”
“Ulipouliza walikujibu nini?”
“Sijauliza bali nilifanya upelelezi wangu, kila kona nilifika lakini sikupata kuona chochote.”
“Ulichunguza nini?”
“Sehemu za makaburi au kupata taarifa kama hajafa yupo wapi?”
“Una uhakika Monika hakuzikwa?”
“Nina uhakika.”
SONGA NAYOOOOO
“Basi kuna sehemu wamemuweka, isiwe naye wamemuweka kwenye hicho chumba  na kumpaka mafuta?”
“Mmh! Sijui.”
“Unaweza kuingia?”
“Mmh! Nitajitahidi kuhakikisha napata ukweli.”
“Basi utakachokipata usikose kunijulisha.”
“Nakuahidi kukuletea kila kitu.”
“Haya shemu kwaheri.”
“Ya kuonana.”
Niliagana na shemu na kurudi zangu nyumbani, nilizidi kuchanganyikiwa na maneno ya pande mbili juu ya ukweli juu ya kifo cha dada Monika. Moyoni niliapa nikipata muda lazima mama ataniambia ukweli.
Siku zilikatika bila kujua taarifa za uhakika kuhusiana na habari tata juu ya kifo cha dada Monika ni kweli amekufa? Kitu ambacho moyo wangu haukukubaliana nacho. Uvumilivu ulinishinda, siku moja nilimfuata mama shambani kutaka kujua ukweli wa dada Monika. Kama kawaida yangu nilidanganya naumwa.                                                         
*****
Baada ya kuondoka na kuniacha nyumbani na mfanyakazi, majira saa nne asubuhi nilikwenda hadi shamba. Nilimkuta mama akipiga jembe kama hana akili nzuri. Moyoni nilimuonea huruma jinsi alivyohenyeka japo tuna pesa, kila dakika niliyakumbuka maneno ya dada Monika kuwa maisha yetu yanaongozwa na ushirikina.
Nilimwita mama ambaye alishtuka kuniona, niliamini kabisa alijiandaa kutokana na kumuuliza maswali mazito siku ya kwanza.
“Wee Masalu mbona huku si unaumwa?”
“Kidogo nimepata nafuu.”
“Haya ulikuwa unasemaje?”
“Kuna kitu mama kinanisumbua kila siku naomba msaada wako kwani naweza kuwa chizi.”
“Wee mwana mbona una mambo kuna nini tena?”
Mama alisema huku akiweka jembe pembeni na kunifuata nilipokuwa nimesimama.
“Masalu  kuna  nini tena?” Mama aliniuliza huku akifuta jasho kwenye paji la uso kwa mkono.
“Mama toka kifo cha dada Monika kuna mambo yamekuwa yakinichanganya na kunifanya kila siku nisijielewe.”
“Masalu mambo gani tena mwanangu kila siku huishi vioja?”
“Kuhusu dada Monika.”
“Monika kafanya nini tena?”
“Mama ni kweli dada Monika amefariki?”
”Masalu wewe si mtoto mdogo sasa, kila mtu anajua Monika amefariki wewe ukiwemo.”
“Mamaa, kama dada Monika amefariki mbona sikuona mazishi wala kaburi lake.”
“Masalu uyaone hayo ili yakusaidie nini?”
“Mama unajua majirani wanatusema vibaya toka taarifa za kifo cha dada Monika.”
“Nani aliwaambia Monika amekufa?”
“Mamaa, kwani kifo cha dada Monika kilikuwa cha siri?”
“Hata kama sio cha siri sio lazima wajue.”
“Hivi mama watu wakiniuliza dada Monika yupo wapi mimi niwajibu nini?”
“Wanyamazie usiwajibu chochote.”
“Lakini mama, kumbe hata yule shemeji aliyekuwa anakaa na dada Monika mlimfukuza asihudhurie mazishi?”
“Ahudhurie ametoa kiasi gani cha pesa kwa dada yako, zaidi ya kutuchanganya kifamilia?”
“Lakini mama tuachane na hayo, kaburi la babu na bibi nalifahamu, kaburi la kaka mkubwa nalifahamu. Makaburi yote yanayotuhusu nayafahamu na kila mwisho wa mwaka huenda kuyazuru familia yote na pia huenda kila mwezi kusafisha na kuyaweka katika hali ya usafi. Lakini kaburi la dada Monika lipo wapi, japo sikuhudhuria mazishi yake?”
“Masalu, wee mtoto mdogo hujui lolote, elewa kuwa dada yako Monika amefariki.”
“Mama, bado hayajaniingia akilini.”
“Masalu hebu niondokee, nilifikiri jambo la maana kumbe ni upumbavu,” mama alisema huku akijiandaa kurudi shambani.
“Mama unaniona mtoto lakini mambo yetu yote yapo hadharani.”
“Mambo gani?” Mama alishtuka na kunigeukia ili kutaka kujua.
“Dada Monika alinieleza mengi kuhusiana kifo chake alichotishiwa na baba kwa ajili ya kukikataa kidonda na kunitisha kidonda kile kitahamia kwangu.”
“Masalu nikueleze mara ngapi kuwa dada yako Monika alikuwa muongo aliyetaka aonekane alichokifanya ni sahihi cha ukosefu wa adabu?”
“Lakini mama mbona mengi aliyonieleza yanatokea? Uongo wake ni nini?”
“Kama nini?”
“Kuhusu wewe kuteseka na kilimo wakati familia ina uwezo mkubwa?”
”Kulima si kujitesa bali kujipa mazoezi.
“Mama, juzi uligombana na baba akikulazimisha uje shamba wakati ulikuwa hujisikii vizuri hata juzi uliniambia hukulala kutokana na maumivu ya mgongo. Mama naona umejisahau pale uliponiambia kuwa baba atakuua kwa vitu vya kulazimishana, bado tu unasema mazoezi. Mama unaweza kuona mnafanya siri lakini kila kitu kipo wazi.
“Unaweza kuona watu wapo kimya, lakini kuna maneno mengi sana juu ya kifo cha dada Monika, hakina tofauti na kifo cha mtoto wa dada Mihayo.”
“Masalu! Hakina tofauti ya nini?”
“Wanasema hata mtoto wa dada Mihayo alipokufa hakuzikwa.”
“Hakuzikwa alifanywa nini?” Maskini mama aliniuliza huku macho yakimtoka pima na kijasho chembamba kilimvuja.
“Eti wanasema kile chumba ambacho hakifunguliwi ndani kuna maiti ya mtoto ambayo huwa mnaipaka mafuta kila siku ndicho chanzo cha dada Mihayo kuwa na utajiri mkubwa kuliko wenzake.”
“Wee mtoto, haya yote umeyasikia wapi?” Mama alishtuka.
“Shemeji aliniambia kuwa kabla dada hajakata roho alimueleza mambo mengi juu ya ushirikina wa familia yetu kutumia kidonda chake kujipatia utajiri na hata alipotoka nyumbani kukataa kuendelea na kidonda ilisababisha kifo chake.”
“Masalu! Alimueleza kuwa kwenye chumba hicho kuna maiti ya mtoto?”
“Ndiyo, tena alimueleza kuwa watu waliokuwa wakiipaka maiti ile mafuta ni wewe baba na yeye dada Monika.”
“Mungu wangu, kayasema hayo Monika?”
“Na wasiwasi mwingine wanasema maiti ya dada Monika huenda nayo haikuzikwa imefichwa kwenye chumba kile cha siri.”
“Ooh... Mungu wangu ...Ooh moyo wangu,” mama alisema huku akishikilia kifua na kuanguka chini. Nilipojaribu kumuamsha hakuamka, nilipiga kelele kwa majirani wa shamba la pili. Sauti yangu iliwakusanya watu ambao walifika na kumpa huduma ya kwanza mama aliyekuwa amepoteza fahamu.
Alipopata fahamu aliwaomba wampe msaada wa kumrudisha nyumbani, jirani yetu mama Kusekwa alimsindikiza mama hadi nyumbani. Tulipofika alituacha na yeye kurudi shambani. Nilijawa na wasiwasi huku nikijilaumu kwa kumueleza mama mambo ambayo niliyaona mazito.
Nikiwa pembeni ya mama aliyekuwa bado amejilaza kwenye zulia huku akipuliziwa na upepo wa feni aliniita:
“Masalu.”
“Naam mama.”
“Kuna mtu aliuliza sababu ya kuanguka kwangu?”
“Ndiyo mama.”
“Uliwajibu nini?”
“Niliwaeleza kuwa ulianguka ghafla.”
“Hawakukuhoji zaidi?”
“Hawakunihoji zaidi ya kukupa huduma ya haraka.”
“Ooh, afadhali.”
“Unajisikiaje kwa sasa?” Nilimuuliza mama kwa huruma.
“Mmh, sijambo kidogo ila nakuomba tuliyozungumza yote usimwambie mtu.”
“Sawa mama.”
Nilimkubalia ili tu kuiacha siku ile ipite pia kutokana na hali yake, lakini bado sikupata jibu la dada Monika amekufa kweli, japo shemeji alinihakikishia amekufa. Na kama amekufa amezikwa wapi au ndiyo yaleyale niliyoelezwa kuwa mwili wake umefichwa ndani.
Moyoni nilibakia njia panda kutaka kujua ukweli kuhusu dada Monika, nilipanga kama mama atashindwa kunieleza basi nitamvaa baba na ukali wake ili nijue amekufa au mzima na kama amekufa amezikwa wapi.
Sikutaka kuliulizia jambo lile haraka kutokana na hali ya mama, niliamua kukaa kimya, lakini moyoni sikuwa na raha kutaka kujua ukweli wa kifo cha dada Monika. Siku moja asubuhi kabla ya kwenda shule mama alinifuata chumbani kwangu na kunieleza nisiende shule kuna sehemu anataka kunituma.
Nilibadilisha nguo zangu za shule na kuvaa za nyumbani, wakati huo alikuwa akijiandaa kwenda shambani. Lakini siku ile hakuwahi kama ilivyo kawaida yake. Tuliondoka nyumbani pamoja kuelekea shambani, baada ya muda wa chai, kutoka  nyumbani mpaka shambani ni mwendo wa dakika 45. Tulikwenda huku tukizungumza, mama aliniulizia habari za shule, nilimuelezea maendeleo yangu japo hakuwahi hata siku moja kushika madaftari yangu kuyaangalia.
Katika kumbukumbu zangu nilielezwa kuwa mama aliishia darasa la sita baada ya kupewa ujauzito na baba kisha kumtorosha. Taarifa hizo alinipa marehemu ambaye sina uhakika kama kweli amekufa au maiti yake imefungiwa katika chumba kisichofunguliwa.
Dada Monika alinieleza kuwa mama yetu alitengwa na familia yake baada ya kubebeshwa ujauzito na baba na kutoroshwa. Kitendo kile ndicho kilichofanya mama aishi maisha ya peke yake bila ndugu, ndugu yake mkubwa alikuwa baba kitu kilichofanya amnyanyase kwa kujua hana pa kwenda.
Sababu ile ndiyo iliyomfanya mama aishi kama mtumwa kwa vile kila alipofanya kosa baba alimtishia kumfukuza. Kwa kweli kitendo cha baba nilikiona cha kikatili sana, kila dakika nilijikuta nikimchukia baba kwa roho mbaya ya kuitesa familia yake kwa ajili ya mali.
Niliamini  mateso ya muda mrefu na shuluba zote, baada ya kupata utajiri wa kushirikina, basi alitakiwa mama atulie na kufaidi matunda ya uchawi wao. Lakini imekuwa tofauti mama kila kukicha amekuwa mtu wa kusurubika. Kilichonishangaza ni ndugu zangu kushindwa kumsimamia mama na kumpunguzia mateso ya kulima na kupasua kuni. Kila nilipomtazama mama yangu roho iliniuma na kujiapiza kama Mungu atanisaidia kupata kazi na kuwa na maisha mazuri basi nitamuondoa kwa baba.
Moyoni nilijiapiza kutokubali kuishi maisha machafu ya ndugu zangu ya kutoa familia zao kwa ajili ya kafara ya hatari na kujiona kama wataishi milele. Nilijiuliza dada Mihayo atamwambia nini mwanaye mbele ya Mungu, aliyemtoa kafara kwa ajili ya utajiri na baadaye kuendelea kumtesa kwa kumlaza kwenye chumba?
                                                             ****
Kuna kitu alinieleza dada Monika juu ya mama na kuniomba nimchunguze, nakumbuka siku hiyo alinieleza:
“Masalu, mama yetu anaishi maisha ya mateso makubwa sana, baba ni shetani asiyefaa mbele ya jamii. Nataka nikueleze kitu kimoja ambacho mimi wananikataza. Kwa taarifa yako nilikatazwa kulala na mwanaume lakini baba ana mwanamke kamjengea nyumba ya gharofa moja.”
Dada Monika aliendelea kunieleza jinsi watu wanavyotumia pesa huku mama akiteseka, alinieleza:
“Mdogo wangu familia yetu yote tutateketea kwa moto wa kiama, hebu ona maisha ya mama yanalingana na utajiri tulionao? Hata kama kuyumba hatuwezi kuishiwa kiasi cha kutisha, sawa na tembo kuugua maralia hawezi kukonda kama mbwa.
“Masalu, sema tu mama mbishi, nilimueleza mapema tuondoke pamoja ili aepukane na maisha ya mateso, lakini mama kama amerogwa na baba haelewi hasikii. Hivi kweli mama yetu ni wakuvaa kandambili za kufunga na kamba?” Nakumbuka siku hiyo dada Monika alizungumza huku akibubujikwa machozi.
Mama anateseka dada Mihayo anamhonga bwana wa pembeni gari, Masalu inauma lakini sina uwezo. Kama kidonda hiki angekuwa nacho mtu mwingine na mimi kuwa na uwezo wa dada Mihayo hata kwa kutoa kafara ya mtoto mama yangu angeishi kama malaika.
Lakini sina uwezo, hata hiki kidogo ninachokipata nikimpelekea mama hatakitumia zaidi ya kugeuzwa ndondocha na baba.”                                                  
ITAENDELEA SIKU YA KESHOOOOOOOOOOOO

No comments

Powered by Blogger.