ad

ad

MASSACRE (MAUAJI YA HALAIKI) SEHEMU 03


   “Upo wapi Benedict? Mbona sikuoni hapa nje?” Sauti ya upande wa pili ilisikika ikiuliza.

   “Wewe nani?” Benedict aliuliza.

   “Mkuu wa polisi kitengo cha upelelezi”

   Benedict hakutaka kuongea kitu chochote kile, akakata simu, akainuka kitandani na kuanza kuelekea nje. Alipofika nje, akaanza kuangalia katika kila upande. Macho yake yakatua katika uso wa mwanaume mmoja aliyekuwa na ndevu nyingi ambaye alimuonyeshea ishara ya kumuita. Benedict akaanza kupiga hatua kumfuata mwaname yule.

   “Hebu tusogee pembeni kidogo” Mwanaume yule alimwambia Benedict na kuanza kusogea pembeni. Hata kabla mzee yule hakuongea chochote, akatoa kitambulisho chake na kumuonyeshea Benedict.

   “Uchunguzi wenu umeishia wapi?” Benedict aliuliza.

   “Kwamba baba yako hakujinyonga”

   “Unasemaje?”

   “Huo ndio ukweli. Hakujinyonga bali alinyongwa”

   “Umejuaje?”
   “Tulipima alama za vidole katika kamba ile, na vile vile tulikuta alama za kiganja katika shavu lake hali iliyoonyesha kwamba alipigwa kibao kabla ya kunyongwa” 
   “Sawa. Kwa hiyo mmeamua nini?”
   “Kumtafuta muuaji. Jambo hilo libaki kuwa lako tu, usimpe taarifa dada yako wala mama yako katika kipindi hiki. Wape taarifa baada ya mwezi mzima kupita” Mkuu yule wa polisi alimwambia.
   Benedict akaonekana kuchanganyikiwa, maneno ambayo aliongea mzee yule ndio ambayo yalionekana kumchanganya zaidi. Alimwangalia mzee yule mara mbili mbili huku akionekana kutokuamini kile ambacho alikuwa ameambiwa. Hasira zikazidi kumpanda zaidi juu ya kanisa la Praise And Worship kwa kuona kwamba kanisa lile pia lilikuwa limehusika katika mauaji ya baba yake.
   Unyonge ukaongezeka zaidi moyoni mwake, kiu ya kumtafuta muuaji ikaonekana kumkamata. Maswali mengi juu ya muuaji huyo yakaanza kumiminika kichwani mwake, mbele yake akaona giza, tumaini ndani ya moyo wake likaonekana kupotea.
   “Ni kanisa. Kanisa linamjua muuaji” Benedict alijisemea kwa hasira.
****
   Mchungaji Mwakipesile hakuonekana kuridhika japokuwa mchungaji Matimya alikuwa amevuliwa cheo cha uchungaji na kusimamishwa kazi ya Utumishi wa Mungu. Hakutaka mzee Matimya abaki ndani ya dunia hii kwani kama angemuacha basi ni lazima ingetokea siku ambayo angekuja kufahamu njama zote alizozifanya na hivyo kumuingiza katika matatizo.
   Mchungaji Mwakipesile hakutaka kutulia, akaiweka pembeni kazi yake ya Utumishi wa Mungu aliyokuwa nayo na kujiingiza katika mambo ambayo yalikuwa kinyume na kazi yake. Akaamua kuwafuata vijana ambao akaamini kwamba wangeweza kumfanyia kazi yake kama alivyotaka kufanyiwa. Mchungaji Mwakipesile hakutaka kuendelea kubaki Morogoro, kitu alichokifanya ni kuanza safari ya kuelekea Dar es Salaam kwa kutumia gari lake.
   “Unahitaji nini mzee?” Kijana mmoja aliyejazia mwili alimuuliza mchungaji Mwakipesile.
   “Nahitaji kuonana na kiongozi wenu”
   “Unamfahamu au?”
   “Hapana” Mchungaji Mwakipesile alijibu.
   Hapo hapo akaambiwa ateremke kutoka ndani ya gari lake. Vijana watatu wakatokea mahali hapo kutoka katika sehemu ambayo hakuifahamu na kuanza kumpekua. Walitumia dakika tano kumpekua yeye pamoja na gari lake, walipomaliza wakaanza kumwangalia usoni.
   “Wewe ni polisi?” Kijana mmoja aliuliza.
   “Hapana”
   “Unahitaji nini?”
   “Nataka kuonana na mkuu wenu” Mchungaji Mwakipesile aliwaambia.
   Hapo hapo akafungwa kitambaa usoni na kisha kupakizwa ndani ya gari nyingine na safari ya kuelekea asipopafahamu kuanza. Muda wote mchungaji Mwakipesile alikuwa akitetemeka kwa woga. Imani aliyokuwa nayo juu ya vijana wale ikaanza kupotea, kitu alichokifanya katika kipindi hicho ni kutulia ili kuona ni mahali gani ambapo angefikishwa.
   Safari ilitumia dakika kumi huku kitamba kikiendelea kuwa usoni mwa Mchungaji Mwakipesile. Mara baada ya dakika chache gari likasimama nje ya jengo moja ambapo geti likafunguliwa na gari kuingizwa ndani. Mchungaji Mwakipesile akateremshwa na moja kwa moja kupelekwa ndani ya nyumba hiyo. Kitambaa kile alichokuwa amefungwa usoni kikafunguliwa na kuamrishwa kukaa kochini.
   Macho ya mchungaji Mwakipesile hayakutulia sehemu moja, yalikuwa yakiangalia kila kona sebuleni pale ambapo alikuwa ameachwa peke yake. Wala hazikupita dakika nyingi, mzee mmoja mnene akafika mahali hapo na kutulia katika kochi jingine huku mkoni akiwa na chupa ya kinywaji cha Heineken.
   “Nasikia unanihitaji” Mzee yule alimwambia mchungaji Mwakipesile.
   “Ndio”
   “Una shida gani?”
   Mchungaji Matimya akaanza kuelezea shida zake huku mzee yule akiwa kimya kumsikiliza. Mchungaji alitumia dakika tano kuelekezea kila kitu ambacho alitaka kifayike kwa wakati huo. Mara baada ya kumaliza maelezo yake, mzee yule akachukua kinywaji chake kile na kupiga funda moja.
   “Una kiasi gani?” Mzee yule alimuuliza.
   “Milioni mbili” Mchungaji alijibu lililomfanya mzee yule kuanza kucheka.
   “Unataka tumuue mtu au kuku?” Mzee yule aliuliza.
   Tayari muonekano wa mzee yule ukaonekana kuwa tofauti na jinsi alivyokuwa kabla, ndita zikaanza kuonekana usoni mwake hali ambayo ilimuongezea wasiwasi mchungaji. Mchungaji Mwakipesile akashindwa kutoa jibu, alibaki akimwangalia usoni mzee yule kana kwamba hakulisikia lile swali aliloulizwa.
   “Acha utani na kazi yetu” Mzee yule alimwambia.
   “Milioni tatu” Mchungaji Mwakipesile alimwambia.
   “Nimekwambia acha utani”
   “Milioni nne. Naomba unisaidie”
   “Utani wako umezidi”
   “Milioni tano. Please, naomba unisaidie”
   “Sawa. Nitafanya hivyo kwa kiasi hicho kwa sababu tu umeniomba” Mzee yule alimwambia Mchungaji Mwakipesile.
   Mchungaji akaanza kutoa maelekezo kama njia ambazo zingewezesha kupatikana kwa mzee Matimya. Akatoa picha yake na yule mzee kuanza kuiangalia kwa makini. Alieleza kila kitu ambacho kilionekana kuwa muhimu kuhitajika na watu hao.
   “Utafurahia kifo gani?” Mzee yule alimuuliza.
   “Chochote kile ili mladi aonekane amejiua” Mchungaji Mwakipesile alijibu.
****
   Saa kumi na mbili, vijana watatu walikuwa wamelipaki gari lao dogo mita hamsini kutoka katika geti la nyumba ya mzee Matimya iliyokuwa Mwenge. Vijana wale hawakutoka nje ya gari lao, waliendelea kumsubiri mzee Matimya ambapo lengo lao lilikuwa moja tu, kumuua. Waliendelea kusubiri zaidi na zaidi lakini wala mzee Matimya hakutoka ndani.
   Mara baada ya kuona kwamba wamesubiri muda mrefu pasipo mzee Matimya kutoka ndani ya nyumba yake, kijana mmoja kati yao akachukua simu yake na kupiga namba ya mzee Matimya ambayo walikuwa wamepewa na mchungaji Mwakipesile. Simu ikaanza kuita, iliendelea kuita kwa sekunde chache, ikapokelewa.
   “Mungu wangu! Umerudi lini kutoka Marekani?” Sauti ya mzee Matimya ilisikika ikiuliza mara baada ya maongezi mengine.
   Maongezi kati ya mchungaji Matimya na kijana yule aliyejiita Zolaya yaliendelea zaidi na zaidi. Vijana wale wengine wala hawakuongea kitu chochote kile, walibaki kimya wakimsikiliza Zolaya. Maongezi hayo yalichukua dakika mbili nzima, simu ikakatwa, uso wa Zolaya ukajaa tabasamu hali ambayo iliwaonyeshea matumaini fulani.
   “Vipi?” The Killer aliuliza.
   “Anatoka. Jiandaeni, wekeni silaha zenu vizuri” Zolaya aliwaambia.
   Hawakutaka kusubiri chochote kile, silaha zikawekwa tayari. Kila mtu akabaki kimya huku macho yakiwa getini kwa mzee Matimya. Zilipita dakika tano, geti likafunguliwana gari aina ya Vitara kutoka. Wakayapeleka macho yao ndani ya gari lile, hakukuwa na mtu yeyote zaidi ya mzee Matimya. Walipoona kuwa mzee Matimya ameanza safari ya kuelekea uwanja wa ndege, hapo hapo Zolaya akawasha gari na kuanza kumfuatilia mzee Matimya.
   Hawakutaka kuwa karibu na gari la mzee Matimya, waliacha umbali wa hatua thelathini kati yao. Mara baada ya gari la mzee Matimya kuchukua barabara ya Sam Nujoma, nao wakachukua barabara hiyo na kuanza kuelekea Mwenge kituoni.
   “Unafikiri atatumia njia gani kwenda uwanja wa ndege?” The Killer aliuliza.
   “Labda atakwenda kuingilia pale Sayansi. Njia ya kule Ubungo hakutaka kuitumia kwa sababu ya foleni” Zolaya alijibu.
   “Kwa hiyo tufanye nini?”
   “Kama kutakuwa na foleni kidogo pale Sayansi itakayomfanya kusimama. Shukeni na mkamuingilie. Hakikisheni mnampa amri ya kuelekea Mbezi, hasa katika msitu wa Pande” Zolaya aliwaambia.
   “Sawa”
   Bado waliendelea kumfuatilia zaidi na zaidi huku wakiwa wametenganishwa na magari mawili kati yao. Mzee Matimya akakata kona na kuchukua barabara ya Ally Hassan Mwinyi. Kila mmoja garini alikuwa na shauku ya kutaka kufanya kile ambacho walikuwa wameagizwa. Kama walivyotaka ndivyo ilivyokuwa, walipofika Sayansi, magari yakasimama kutokana na foleni iliyokuwa mahali hapo.
   “Fanyeni haraka. Mfuateni, mtekeni na kuanza kuelekea Mbezi” Zolaya aliwaambia.
   Kwa haraka sana bila kupoteza muda, The Killer na Zinja wakateremka na kuanza kulifuata gari alilokuwa mzee Matimya.Walipolifikia, wakaingiza mikono yao katika madirisha yale ambayo hayakuwa yamefungwa vioo na kisha kutoa loki za milango ile. Mzee Matimya akapigwa na mshtuko mara baada ya kuona vijana wawili wakiingia ndani ya gari lake.
   “Mbona mnaingia nd….?” Mzee Matimya aliuliza lakini hata kabla hajamalizia swali lake, The Killer akatoa bunduki yake iliyokuwa kiunoni.
   Mara baada ya mzee Matimya kuiona bunduki ile, hapo hapo akatulia, mapigo yake ya moyo yakaanza kumdunda kwa kasi kubwa huku woga ukianza kumuingia. Hakutakiwa kuongea kitu chochote kile katika kipindi hicho. Kitu walichokifanya ni kumuamuru mzee Matimya kutoka katika usukani na kuelekea katika kiti cha nyuma huku Zinja akishikilia usukani na safari ya kuelekea Mbezi kuanza.
   Walitumia dakika sabini kutoka Kijitonyama mpaka Mbezi Mwisho huku Zolaya akiwafuatilia kwa nyuma. Hawakutaka kuishia Mbezi Mwisho, kitu kilichowapelekea kuendelea mbele. Kutokana na kasi ambayo walikuwa wakiitumia, walichukua dakika tano mpaka kufika katika msitu wa Pande.
   “Hapa hapa panatosha” The Killer alimwambia Zinja.
   Wote wakateremka kutoka ndani ya gari, wakamshusha mzee Matimya na kuanza kusogea nae katika sehemu iliyokuwa na miti mingi zaidi. Zolaya akafika mahali hapo, akateremka huku mkononi akiwa na kamba ngumu na kisha kuanza kuwasogelea.
   Kutokana na giza nene lilikuwa mahali hapo, wakawasha tochi zao na kuanza kuelekea mbele zaidi. Mzee Matimya bado alikuwa akitetemeka, moyoni alikuwa akiendelea kusali kwa kumtaka Mungu amnusuru na kumlinda na chochote ambacho kilitakiwa kufanyika. Hali haikuonekana kuwa na usalama wa hali yoyote ile kwa mzee Matimya, kadri walivyozidi kusonga mbela na ndivyo ambavyo woga ulivyozidi kumshika zaidi.
   “Panatosha” Zolaya aliwaambia huku akiwa amemaliza kufunga kamba katika mtindo wa kitanzi.
   “Jamani vipi tena?” Mzee Matimya aliuliza mara baada ya kuona akivalishwa shingoni kamba ile ambayo Zolaya alikuwa amekwishaifunga mtini. Hakukuwa na mtu aliyejibu chochote zaidi ya Zolaya kumpiga kofi moja shavuni ambalo lilimfanya kulewa.
   Kutokana na ubishi ambao alikuwa akiuleta mzee Matimya, iliwachukua nusu saa mpaka kukiingiza kichwa chake katika tundu la kamba na kumnyonga huko porini. Hakukuwa na mtu aliyeonyesha roho yoyote ya huzuni, kila mtu alikiona kitendo kile kuwa cha maana kwake. Huo ndio ukawa mwisho wa maisha ya mzee Matimya.
   Kazi yake kubwa ya kumtumikia Mungu katika kipindi kilichopita ikabaki kuwa kama historia. Alinyongwa porini siku hiyo baada ya wiki mbili ndani ya skendo yake ya kutaka kubaka ambayo ilikuwa imevuma sana nchini Tanzania. Zolaya alipohakikisha kwamba mzee Matimya amefariki, akaondoka pamoja na wenzake huku wakiuacha mwili ule mtini.
*****
   Kadri siku zilivyozidi kwenda mbele na ndivyo ambavyo hasira za Benedict juu ya kanisa la Praise and Worship lililoko Mwenge zilivyozidi kuongezeka. Hakuonekana kumpenda mtu yeyote ndani ya kanisa lile, kila mtu kwake alionekana kuwa adui wake. Kila alipokuwa akielekea kanisani pamoja na mama yake, Bi Meriana na Angelina, Benedict hakutaka kuongea na mtu yeyote kanisani hapo.
   Moyo wake aliuona kuwa kanisa lilihusika na kifo cha baba yake, mzee Matimya. Kila kitu ambacho kilikuwa kikifanyika kanisani kama mahubiri ya Neno la Mungu kilionekana kuwa kama unafiki. Mauaji ndicho kitu ambacho kilikuwa kimeutawala moyo wake katika kipindi hicho, hakutaka kuliacha kanisa hivi hivi, alitamani kuliangamiza kanisa.
   Ibada ya mwisho ya Jumapili ya mwisho katika mwaka huo ndio ambayo ilikuwa ikiendelea ndani ya kanisa hilo. Kila mtu alionekana kuwa uso ulioonyesha furaha. Wanakwaya walikuwa wakiimba kwa furaha, yaani kila kitu katika kipindi hicho kilikuwa kikifanyika katika hali ya furaha. Watu wote walikuwa wakiimba kwa furaha kwani zilikuwa zimebakia siku mbili kabla ya kumaliza kwa mwaka huo wa 2007.
   “Funguo ziko wapi?” Sauti ya shemasi ilisikika ikiuliza.
   Kila mtu aliyekuwa amekaa katika viti vya nyuma kanisani pale aligeuka na kuwaangalia mashemasi ambao walikuwa wakizitafuta funguo ambazo zilikuwa mlangoni katika kipindi kichache kilichopita. Ingawa ibada ilikuwa ikiendelea huku mchungaji mpya wa kanisa hilo, Munisi akiendelea kuhubiri, mashemasi hawakuwa wakisikiliza mahubiri hayo zaidi ya kuendelea kuzitafuta funguo za milango ya kanisa.
   “Kwani zilikuwa wapi?” Shemasi mwingine aliuliza.
   ”Zilikuwa hapa. Tena muda mchache uliopita”
   “Hebu angalia chini ya viti, labda kuna mtoto alizichukua”
   Hapo hapo Shemasi mmoja akaanza kuangalia angalia chini ya viti lakini funguo wala hazikuonekana. Tayari wasiwasi ukaanza kuwaingia, akili zao zikaanza kuchanganyikiwa. Hawakujua ni nani ambaye alizichukua funguo zile kutoka katika msumali uliochomekwa ukutani, wakazidi kuangalia katika kila sehemu huku mchungaji Munisi akiendelea kuhubiri.
   “Zile kule”
   “Ziko wapi?”
   “Kazishika yule mtoto” Shemasi alijibu.
   Kwa haraka haraka akaanza kupiga hatua kumfuata mtoto yule aliyezishika funguo zile ambazo alikuwa nazo, mtoto yule ambaye alikuwa pembeni mwa Benedict. Mara baada ya kumfikia mtoto yule, shemasi akazichukua funguo zile.
   “Mmechelewa sana” Benedict alijisemea moyoni huku akionekana kuwa katika utulivu mkubwa kumsikiliza mchungaji.
   Mara baada ya ibada kumalizika, moja kwa moja Benedict akaanza kupiga hatua kuelekea nje ya kanisa lile huku furaha ikiongezeka maradufu moyoni mwake. Kitendo cha kuzipata funguo za milango ya kanisa lile kilionekana kumfurahisha kupita kiasi. Hakutaka kuliona kanisa likiendelea kumtumikia Mungu kwani kitendo kile kilionekana kuwa kama unafiki mbele ya macho yake.
   Mara baada ya kufika Kariakoo, akateremka na kuanza kuelekea katika kibanda ambacho kilikuwa na tangazo la kuchongesha funguo. Alipokifikia, akamuita mchonga funguo ambaye mara moja akafika mahali hapo. Akachukua kipande cha sabuni ambacho kilikuwa na alama tatu za funguo na kisha kumgawia.
   “Elfu moja kila moja”
   “Sawa” Benedict alisema na kisha kumgawia noti ya shilingi elfu kumi mchongaji yule.
   “Rudi saa kumi, kila kitu kitakuwa tayari”
   “Hakuna tatizo” Benedict alisema na kisha kuondoka mahali hapo.

****
   Masaa manne yalikuwa yamebaki kabla ya kuuingia mwaka ambao ulikuwa ukiitwa ‘Mwaka wa Baraka’, mwaka wa 2008. Kila mtu alionekana kuwa na furaha, waumini mbalimbali wa dini ya kikristo wakaanza kujiandaa tayari kwa kuanza safari ya kuelekea makanisani mwao. Vijana mitaani wakaziweka ngoma zao vizuri huku mafataki ya aina mbalimbali yakiwa yamewekwa vizuri.
   Japokuwa waumini wa Kikristo walikuwa wakitaka mwaka uingie na kuwakuta wakifanya maombi ya kumshukuru Mungu kanisani lakini hali ilionekana kuwa tofauti kwa watu wengine. Walevi walitamani mwaka uingie huku wakiwa na vinywaji midomoni mwao, kwa wale ambao walikuwa wazinzi, walitamani mwaka uingie na kuwakuta wakifanya ngono na watu wawapendao.
   Benedict hakutulia, muda wote alikuwa akifikiria kufanya mauaji. Huruma ilitoweka moyoni mwake, hasira kali na roho ya kulipa kisasi ndio ambayo ilikuwa imeutawala moyo wake kwa wakati huo. Mara kwa mara macho yake yalikuwa yakiiangalia saa yake, dakika zilionekana kwenda taratibu tofauti na siku nyingine.
   “Jiandae twende kwenye mkesha kanisani” Bi Meriana alimwambia Benedict.
   Mishipa ya fahamu ya Benedict ikawa kama imezibuka, kitendo cha mama yake na dada yake, Angelina kwenda kanisani kingeweza kumzuia katika kufanya kile ambacho alitaka kukianya. Akili yake ikafanya kazi ya haraka haraka, akainuka na kuanza kuelekea chumbani kwake. Akaiangalia saa yake ya ukutani, masaa mawili ndio ambayo yalikuwa yamebaki kabla ya kuingia mwaka mpya wa 2008.
   Hakutaka kuendelea kukaa chumbani, hapo hapo akainuka na kuanza kuelekea sebuleni. Alichokifanya ni kuchomoa funguo za kuingilia mlango wa sebuleni na mlango wa nyuma. Akatoka nje na kisha kuifunga milango yote kwa nje. Hakutaka kubaki mahali hapo, akaingia garini na kisha kuanza kuelekea kanisani huku akiwa na funguo za kanisa lile ambazo alikuwa amezichonga Kariakoo.
   Hakutaka kuelekea kanisani moja kwa moja, akaanza kuelekea Sinza huku lengo lake likiwa ni kutaka kupata madumu ambayo angefanya nayo kazi. Mara baada ya kuliona duka la jumla maeneo ya Sinza Makaburini, hapo hapo akasimamisha gari, akateremka na kuanza kupiga hatua kulifuata duka lile.
   “Nahitaji madumu matatu ya lita ishirini” Benedict alimwambia muuzaji mara baada ya salamu.
   “Yenye mafuta?”
   “Hapana. Matupu”
   “Elfu tatu moja”
   Benedict akaingiza mkono mfukoni na kutoa kiasi cha fedha ambacho kilikuwa kinatosha kwa madumu yote hayo matatu. Mara baada ya kumgawia muuzaji kiasi kile cha fedha, akapewa madumu ambayo akayapakiza ndani ya gari na kuondoka katika eneo hilo.
   Safari ya kuelekea katika kituo cha mafuta ikaanza. Akili yake ilikuwa ikicheza na muda tu, dakika tisini ambazo zilikuwa zimebaki kabla ya mwaka mpya kuingia zikaonekana kumtosha kabisa kwa kufanya kile ambacho alipanga kukifanya. Mara baada ya kufika katika eneo la kituo cha mafuta, akayatoa madumu yale na kuanza kujaziwa mafuta aina ya petroli. Yalipojaa yote, akalipa fedha na kisha kuyapakiza garini na kuondoka eneo hilo kuelekea kanisani.
   Kadri muda ulivyozidi kwenda mbele na ndivyo ambavyo hasira zake juu ya kanisa lile zilivyozidi kukaba kiasi ambacho kiliyafanya machozi kutiririka mashavuni mwake. Kila wakati ambao picha ya marehemu baba yake ilivyokuwa ikimjia kichwani na ndivyo ambavyo hasira juu ya kanisa lile ilivyozidi kumpanda. Hakulipenda kanisa, alilichukia kanisa hilo, mbaya zaidi alimchukia kila mtu kaisani mule.
   Ibada ilikuwa ikiendelea kanisani, idadi kubwa ya washirika zaidi ya mia mbili hamsini ilikuwa ndani ya kanisa hilo. Nyimbo mbalimbali za dini zilikuwa zikiendelea huku watu wakiimba kwa furaha. Benedict akayapeleka macho yake katika saa yake ya mkononi, dakika arobaini na tano ndizo ambazo zilikuwa zimebaki kabla ya mwaka mpya kuingia. Benedict hakutaka kuteremka kutoka garini, aliendelea kubaki mule mule huku macho yake yakiendelea kuangalia mishale ya saa yake.
   “Mnahitajika kanisani” Shemasi Mjuni alimwambia Benedict huku akigongagonga katika kioo cha mlango wa mbele wa gari lile. Benedict akashtuka kutoka katika lindi la mawazo, akayapeleka macho yake katika kioo cha saa yake ya mkononi, dakika tano ndizo ambazo zilikuwa zimebakia kabla ya kuingia kwa mwaka mpya.
   Benedict hakutaka kuteremka japokuwa alikuwa amesikia kwamba washirika wote walikuwa wakihitajika kaisani, washirika ambao walikuwa nje ya kanisa wakaanza kuingia kanisani. Ndani ya dakika mbili tu, hakukuwa na mtu yeyote nje ya kanisa zaidi ya Benedict ambaye alikuwa ndani ya gari.
   “Tunataka kuukaribisha mwaka kwa maombi ya shukrani” Sauti ya mchungaji Munisi ilisikika na mashemasi kuanza kufunga milango. Kitendo kile kilionekana kuwa kama kosa, kwani kwa haraka haraka, Benedict akateremka kutoka garini na kuanza kuufuata mlango mkuu wa kuingilia kanisani mule. Akaanza kuchungulia ndani kwa kupitia katika vitundu vya ufunguo kitasani, hakukuonekana kuwa na ufunguo wowote kwa ndani. Benedict akauchukua ufunguo wake ambao aliuchongesha kwa fundi na kisha kuuingiza katika tundu lile na kisha kuufunga mlango ule.
   Akaanza kupiga hatua kuelekea katika milango mingine midogo, napo huko akafunga milango ile kwa funguo alizokuwa nazo. Hakutaka kuzitoa funguo zile katika vitasa, aliziacha pale pale ili kama watu waliokuwa kanisani watakapojaribu kuziingiza funguo zao basi zisiweze kuingia.
   Kwa wakati huo Benedict alionekana kuwa na haraka kupita kawaida. Akaanza kurudi garini ambapo akachukua dumu moja lililokuwa na mafuta ya petroli na kisha kuanza kuyamwaga mafuta yale kupitia katika nafasi ndogo chini ya mlango.

 Unataka niwe nakutumia CHOMEZO watu 200 wa kwanza kulike PAGE YA 2JIACHIE Mtatumiwa imbox chomezo LIKE PAGE YETU HAPA ==>www.facebook.com/2jiachie

ITAENDELEA KESHO HAPA HAPA

No comments

Powered by Blogger.