Mashine za TRA majanga eneo la Kariakoo jijini Dar es Salaam
WAFANYABIASHARA wa maduka eneo la Kariakoo jijini Dar es Salaam
wametangaza mgomo kwa muda usiojulikana hadi pale serikali itakapofanyia
mabadiliko njia mpya za ukusanyaji kodi zilizotangazwa na Mamlaka ya
Mapato Nchini (TRA), za kutumia mashine za kielektroniki (EFD).
Akizungumza jana jijini Dar es Salaam mshauri wa
Jumuiya ya Wafanyabiashara wa Kariakoo, Johnson Minja, alisema kuwa
walikuwa wakitafuta mawasiliano ya Waziri wa Viwanda na Biashara Dk.
Abdallah Kigoda kuweza kukaa meza moja ili kutafuta njia bora ya muafaka
wa ukusanyaji kodi kwa njia nyingine badala ya kutumia mashine hizo.
Minja alisema kuwa njia iliyotumiwa na TRA ya kutumia mashine hizo
imeonekana kuwa mwiba kwa wafanyabiashara wengi wa eneo hilo kutokana na
wengi wao kukosa uwezo wa kununua mashine hizo.
Alisema kuwa serikali imekuwa ikiwabana zaidi wamiliki wa maduka
pekee huku wafanyabiashara ndogo ndogo (Machinga) wakiachwa na kuendelea
na biashara pasipo kulipa kodi.
Mshauri huyo alisema kuwa hawailaumu TRA kwa kuwa jambo hilo ni la
kisera na viongozi ndiyo watekelezaji ila aliiomba serikali kuwasikiliza
na kukutana na wafanyabiashara hao ili kujadiliana kuhusiana na
matumizi ya mashine hizo.
“Tatizo hilo lisingefikia hapo kwa kuwa tumekuwa tukiandika barua
tangu Septemba mwaka huu na kuzipeleka kwa Waziri wa Viwanda na Biashara
ili tukae meza ya majadiliano lakini hatukufanikiwa kuonana naye
kutokana na kubanwa na kazi,” alisema.

Post a Comment