Rupia Banda akamatwa tena na kushtakiwa Zambia
Rais wa zamani wa Zambia, Rupia Banda amekamatwa tena mapema leo
na kufikishwa mahakamani kwa tuhuma ya kuiba malori 9 ya serikali wakati
alipokuwa ofisini.
Malori hayo yalitolewa kama msaada kwa serikali na shirika moja la ujenzi ambalo lilisaidia kujenga uwanja wa michezo wa Ndola.
Upande wa Mashtaka umesema kiongozi huyo wa zamani alikataa kukabidhi
malori hayo kwa serikali na badala yake akayapeleka nyumbani kwake.
Banda mwenye umri wa miaka 76 ameachiliwa kwa dhamana na mahakama
imeamuru hati yake ya kusafiria itwaliwe.
Hii ni katika hali ambayo, kiongozi huyo bado anakabiliwa na mashtaka
mengine ya utumiaji mbaya wa madaraka. Machi 25 rais huyo wa zamani wa
Zambia alipandishwa kizimbani kujibu tuhuma za ulaji rushwa ambapo korti
iliahirisha kesi hiyo hadi baadaye mwezi ujao.

Post a Comment