ad

ad

Nauli hizi bila nyongeza ya mshahara ni sawa?

NAWAAPIA sasa mtajiju. Wakati ule mliwacheka wenzenu wa Kigamboni walipoambiwa kama hawajui kuogelea imekula kwao siyo eh?

Sasa mtashangaa wale wanaotoka Songea kuja Bongo Dar es Salaam kama nao watapiga mbizi kama kijana wangu Magufuli alivyowataka watu wa Kigamboni wafanye walipolalamika maji yamezidi unga kwenye kivuko cha Feri.

Narudia tena huko simo msije mkaninukuu vibaya watu wangu. Nani angependa kung’olewa meno bila ganzi? Huko simo kabisa.
Sasa si mmesikia hili sekeseke la nauli mpya? Kwa mtaji huu wapo watu wataamua kuomba waache wenyewe kazi kwa hiari kwa manufaa ya miili yao.
Ni wangapi watamudu kutembea kwa miguu toka Mbagala hadi Sitesenta kusaka mia? Na ukiamua kukwea motokaa basi ujue kazi yako unaifanya ili upate nauli ya kwenda na kurudi kazini.

Wacha tu nikubaliane na wale wanaosema kama kweli uchumi wa taifa letu umekua basi ni namba kwenye makaratasi tu lakini sio kwenye waleti zetu sisi wavuja jasho.
Wacha niweke pozi kidogo hapa kabla sijajitoa mzima mzima. Ila kwa mtaji huu lazima tutajiju.

Hivi mlipoongeza hizo nauli mna mpango gani na mishahara yetu? Mbona tulidhani mngeanza kuongeza mishahara ndipo mje kwenye hilo la nauli?
Au kwa mahesabu yenu mwaona gharama zimekwenda juu kwa wamiliki wa motokaa tu siyo eh? Niambie wamiliki wao wakikutana na kukoroma mnawasikiliza, niambieni  sisi wafanyakazi wengine tufanye nini?

Tukigoma si mnakimbilia pale Mahakama ya Kazi na kupata stopu oda upesi upesi? Tumeliona hilo kwa walimu na madaktari, mnadhani tuna cha kujiuliza wakati huu?
Kula yenyewe ni shida sasa na nauli ya kwenda kutafuta hicho kibaba nayo mshaifanya iwe ishu watu wangu. Ila jambo moja ninalofahamu ni kwamba aliyeshiba hamjui mwenye njaa ng’o!

Sasa kama mmepandisha hizo nauli, mmejaribu pia kuangalia ubora na usalama wa huo usafiri? Najua wakubwa hamjui adha za usafiri wa umma hasa daladala. Nauliza mmejipanga baada ya kuwapa wamiliki kapu la kuchuma sasa nao wajue wana wajibu kwa walipa nauli?

Hatuwezi kula mlo mmoja kwa siku ili tupate vijisenti vya kudandia daladala  halafu bado ukiingiga huko ukutane na kero. Yale mambo ya levo siti yalikufa siku Mwaibula alipowaachia Sumatra usukani siyo eh?
Hilo huwa hamlioni jamani? Kwamba gari ya watu ishirini inabeba watu arobaini kwenu hilo sio tatizo kabisa naona.

Na gari hilo linakutana na wale manesi wa barabarani wala hakuna kinachotokea, utadhani ni haki ya kikatiba kujaza gari hadi watu wakose pa kukanyaga. Wacha tu nijitoe kimya kimya nikipiga mluzi wangu.  Nasema huko simo kabisa.

Na kwenye magari mnayosema ya kwenda mikoani kwani hamjui kuna mengine yanakuwa na abiria watu na abiria mifugo humo humo utadhani kwenu mtu si afya? Tembeeni mjionee.
Kuna mikoa kusafiri na  gari huku mbuzi na kuku wakiwa sehemu ya abiria wala sio jambo la kushangaza kwao. Nyie mmeshupalia nauli tu siyo eh?
Au hamjui kuna mabasi yanapakia mabati na mazagazaga mengine humo humo na abiria? 

Hamjawahi kujiuliza kwa nini ajali zetu vifio vinakuwa vingi?
Endeleeni tu maana naona Afrika mmeamua sheria zimewekwa ili zivunjwe, mnashtuka tu maafa yakitokea. Ukibisha hili nitakupa mfano wa wanaojenga maghorofa kupitiliza idadi iliyo kwenye  vibali vyao.

Mnadhani ghorofa isipoanguka kuna atakayemchukulia hatua? Na hapo bado wanishangaa nikisema yaelekea huku kwetu sheria zimewekwa ili zivunjwe?
Wacha tu ninyamaze maana machozi yangu mtoto wa mama yako karibu sana.
Ukiacha haya ya kujaza abiria na kupakia mifugo au bidhaa nyingine hatari kwa usalama bado hamjui kwamba wapo madereva wengi wanaendesha hasa daladala wakiwa wamevuta sigara kubwa?

Msiniulize mimi sigara kubwa ila namaanisha ile sigara isiyokuwa ya kawaida ambayo kaka’angu Ndugai ana wasiwasi kuna wabunge wanaichoma kisawasawa!
Huko simo nisije kuambiwa ninawakejeli wahishimiwa sana wanaoendelea kupata   zile posho za kukaa kitako huko wanakokuita makao makuu ya nchi. Mimi wacha nikae kimya lakini nijitoe mwanawani.

Kiukweli kabisa ukiona namna hawa waendesha  daladala  au kule kwetu kwa wakina Kibaki na Uhuru na Raila tunaita Matatuu wanavyoendesha bila kuhofia ajali utapinga kabisa hawavuti sigara kubwa?

Kwenye hili mmejipanga vipi isije ikawa  kazi yenu ni kuruhusu mifuko ya wamiliki itune kwa unono wa nauli, lakini walipaji uhai wao mmeamua kuuweka rehani?
Na hata kwenye haya magari ya safari ndefu kuna wambea wanasema madereva wengi hupenda kutafuna miraa. Nasema haya nimeyasikia kwa wambea msije kuniambia nitoe ushahidi hiyo ni tipu tu nimewapa mfanye wenyewe upelelezi kama ni trafiki au Sumatra huko simo kabisaaaa!

Hata baada ya kupandisha nauli bado mnasema elimu ni bure? Si mmesema mtoto atalipa nusu ya mtu mzima ambayo nauli ya chini kabisa kwa tripu moja ni shilingi mia mbili?
Hivi nyie mnajua umaskini wa watu wetu au vitambi vinawazuia msione mbele? Nauliza kwa dhati kabisa kwa kiwango hiki ni watoto wangapi hasa kwenye miji mikubwa wataweza kwenda na kurudi shule?

Itaanza hadithi ya kwenda kwa miguu wanafika wamechoka halafu wakimaliza shule na kufeli mnaunda tume! Hivi maskini sasa hivi ana raha gani tena ndugu yangu?
Na ole wenu mseme wavizie lifti.  Siwaambii kitakachotokea hadi muende kwanza mkasimuliwe hadithi za Sodoma na Gomora.
Kwa dunia ya leo nani anathubutu kumwacha mwanae apewe lifti na hii mibaba ambayo hujui nani ni nani?  Hamjui siku hizi kuna mijitu inaonekana kwa nje ina heshima zao na wengine hawakosi nyumba za ibada kumbe ni mibazazi isiyokuwa na utu?

Kama hujanielewa shauri yako ila mwenyewe najiondokea taratibu bila kutia neno.
Hili niliseme taratibu tena kimya kimya. Kuna porojo eti imeundwa kamati kuchunguza nauli mpya. Nasema kama hii ni kweli basi Watanzania tutafute aliyetuloga.
Tulipoanzisha Sumatra tulikuwa tumevuta ile nanihii au tumekunywa pombe haramu?  Narudia tena wacha tu niombe kusiwepo na hiyo tume au kamati au kamisheni maana nitakuwa siwaelewi.

Zamani walikuwa wakisema kufa hatufi ila cha moto tutakiona, sasa kwa mtaji huu nina wasiwasi kama tutamudu kubakia kuona hicho cha moto.
Wajanja washajaza nafasi zote za kula kwa mikono miwili sasa wanatuchekishia tu  wakisubiri muda ufike waje tena  watudanganye tuendelee kudanganyika kama kawaida yetu wao waendelee kula kama kawaida yao.
Narudia tena kwa sauti kubwa simo tena simo kwenye hayo yote.
Powered by Blogger.