Ukatili wa kijinsia sokoni wazidi kuwatesa wanawake
ASASI zinazotetea ukatili wa kijinsia, zimeshauriwa kutoa elimu
kuhusiana na unyanyasaji kwa wanawake wengi zaidi sehemu za masoko ili
kupunguza tatizo hilo kwa wajasiriamali hao.
Wakizungumza kwa nyakati tofauti wakati wa kufungwa kwa mafunzo yaliyokuwa yanatolewa na asasi ya Equality for Growth (EfG) kuhusiana na kupinga ukatili kwa wanawake sokoni, kinamama hao walisema vitendo hivyo vimekithiri katika masoko.
Mwenyekiti wa Umoja wa Wanawake katika soko la
Kigogo Sambusa, Mariam Rashid alisema kutolewa kwa mafunzo hayo sokoni
kutachangia wanawake kujitambua na kutambua haki zao.
“Kabla ya mafunzo kutolewa tulikuwa tukinyanyasika sana, lakini hivi sasa wanaume sokoni hapa wamebadilika na kuacha kutumia lugha za matusi,”alisema Mariam.
Naye Mwenyekiti wa Umoja wa Wanawake katika soko
la Feri, Hamida Hindi alisema wanaume sokoni hapo walikuwa na tabia ya
kuwadhalilisha kijinsia kwa kuwashikashika sehemu za miili yao bila
ridhaa yao.
Alisema baadhi ya wanaume walikuwa wakikopa
chakula lakini malipo ilikuwa shida, lakini mafunzo hayo yamewajengea
ujasiri wanawake kudai fedha zao na hata kukataa mambo ya udhalilishaji.
Mtathmini Mradi wa EfG, Samora Julius alisema waliamua kuendesha mafunzo hayo katika masoko manne ya Halmashauri ya Ilala Dar es Salaam,ili kuweza kuondoa unyanyasaji huo.
Alisema mradi huo ambao umeyanufaisha masoko ya
Ilala, Kigogo Sambusa, Buguruni na Kibasila,yamesaidia kuwafanya
wanawake kujitambua katika shughuli zao.
“Tuliwafundisha jinsi ya kujiwekea akiba katika biashara zao,jambo ambalo limewasadia kwa kiasi kikubwa” alisema Julius.
Alisema hivi sasa wanawake katika masoko hayo
wameweza kuanzisha vikundi vya kuweka na kukopa,ambavyo wamekuwa
wakivitumia kusaidiana pale wanapokwama katika shughuli zao.

Post a Comment