ad

ad

Ubuyu Ulionyooka! Wolper Ndani ya Penzi Jipyaaa

Staa wa Bongo Muvi, Jacqueline Wolper Massawe na mpenzi wake mpya Brown.

Ubuyu ambao upo mezani leo ni wa staa wa Bongo Muvi, Jacqueline Wolper Massawe ambaye kwa sasa yupo kwenye penzi jipya la mwanamitindo aliyetajwa kwa jina moja la Brown.
Ubuyu huu unakujia ikiwa ni miezi michache tangu Wolper amwagane na msanii Rajab Abdulhan ‘Harmonize’.


TUJIUNGE NA CHANZO
Kwa mujibu wa mleta ubuyu wetu, mara baada ya Wolper kumwaga manyanga rasmi kwa Harmonize, aliamua kutafuta kipozo cha moyo wake na kuweka msongo pembeni kisha kumdaka Brown ili kumsahaulisha yaliyopita.
Chanzo hicho kilizidi kumwaga mchele kwenye kuku wengi kuwa, Wolper anaonekana kufa na kuoza kwa kijana huyo mtanashati ambaye naye, kama ilivyokuwa kwa Harmonize, ni mdogo kiumri ukimlinganisha na mrembo huyo.

Wolper na Brown
MAHABA NIUE SASA
Ilisemekana kwamba, muda mwingi Wolper amekuwa akionekana na jamaa huyo wakioneshana mahaba niue katika kila kona ili kuthibitisha kwamba ni kweli hayupo tena na Harmonize kwa sababu kuna baadhi ya watu walikuwa hawaamini kama kweli amemwagana naye.

“Kwa sasa anaonekana ndiyo amefika kwa Brown. Yaani haambiwi kitu kwa huyo kijana na hivi sasa mara nyingi wako wote kama kumbikumbi.
“Hii ndiyo ‘kapo’ mpya mjini na ukibahatika kumuona Wolper, lazima umuone Brown maana sasa hivi wamekuwa kama kumbikumbi,” kilinyetisha chanzo hicho kwa sharti la kutotajwa ili kisionekane kimbeya.

WIKIENDA SIYO LA MCHEZOMCHEZO
Kama kawaida, Wikienda siyo la mchezomchezo maana baada ya kuunyaka ubuyu huo, ukiwa bado hata hujafunguliwa kwenye pakti yake, lilifanya jitihada ya kumsaka Wolper ili zijulikane mbivu na mbichi ambapo mambo yalikuwa hivi;
Wikienda: Mambo vipi Wolper?
Wolper: Poa tu, kulikoni kuniibukia asubuhiasubuhi?

 
Brown wakiwa amepozi. 


Wikienda: Kuna ubuyu kuwa, kwa sasa umejiweka kimapenzi kwa mwanamitindo Brown, je, hii ishu ikoje?
Wolper: (kicheko) siyo kujiweka bwana, ukisema hivyo itakuwa labda mtu anajiegesha then (halafu), anaondoka, kwangu haiko hivyo.

Wikienda: Kwa hiyo ni kweli Brown ndiye mpenzi wako kwa sasa?
Wolper: Ndiyo. Kwani kuna sababu gani ya kuficha? Awali hakuna mtu aliyejua lakini kwa sasa tuna muda kama miezi miwili, naona watu ndiyo wanajua sasa hivi.
Wikienda: Je, kweli kwamba unafanya hivyo kumkomoa Harmonize kwa vile inasemekana naye ana mwanamke mjamzito wa Kizungu?

Wolper: Aaah! Wapi! Ili iweje sasa? Kila mtu ana maisha yake jamani.
Wikienda: Je, huyo Brown ni nani au ana wasifu gani?
Wolper: Ndiyo kwanza watu wanaanza kumfahamu, wasijali watamjua tu.

Wikienda: Inasemekana umemzidi umri kama ilivyokuwa kwa Harmonize, je, ni kweli unapenda vijana wadogo?
Wolper: Nani kasema mdogo? Hebu watu waniache nitulize mawazo miye!

TUMGEUKIE BROWN
Kutoka kwa Wolper, Wikienda lilimsaka Brown ili kupata mzani wa ubuyu huo kuhusiana na kujiweka kwa staa huyo mwenye jina kubwa Bongo.

Wikienda: Habari Brown, inasemekana sasa hivi wewe ndiye unapoza roho ya Wolper, je, umejipangaje kuwa na mrembo kama Wolper?

Brown: Kwani kuna shida gani? Nijuavyo mapenzi hayanaga hivyo vitu, ninachojua mimi, ninampenda sana na yeye ananipenda sana.

NENO LA MHARIRI
Kama kweli Wolper ameamua kujituliza kwa Brown, ni vyema akafanya uamuzi sahihi wa kujiridhisha kuwa anampenda kutoka moyoni ili kuepuka kuhesabiwa wanaume aliotoka nao na kuleta picha mbaya kwenye jamii inayomzunguka.

Ubuyu: Imelda Mtema | IJUMAA WIKIENDA | Dar



No comments

Powered by Blogger.