ad

ad

Jay amkumbuka mama yake ukumbini

Baada ya kufunga ndoa katika kanisa la St. Joseph jijini Dar es salaam na mpenzi wake wa muda mrefu, Mbunge wa Mikumi na Mkongwe wa hip hop bongo Joseph Haule 'Prof Jay' amesema ingawa ametimiza ndoto yake, anasikitika mama yake hajaweza kushuhudia.
Prof Jay na mkewe Grace wakionyesha vyeti vyao baada ya kufunga ndoa.
"Namshukuru Mungu kufikia siku ya leo ni ndoto niliyokuwa nayo muda mrefu. Hii ni siku ya kipekee sana kwangu. Ningependa sana mama yangu awe shuhuda wa tukio hili lakini nasikitika bahati mbaya alitangulia mbele ya haki miaka minne iliyopita, naomba tuzidi kumuombea apumzike kwa amani" alisema Prof Jay
Aidha Prof Jay aliongeza kwamba furaha aliyonayo ni kukamilisha ndoto zake kwa mpenzi wake huo ambaye tayari walibahatika kupata mtoto wa kike na bado wakaendelea kudumu pamoja kwenye mahusiano.
"Nimedumu na Grace kwa muda mrefu sasa namshukuru Mungu kwa hii siku kutimia maana nilikuwa naiota kila siku. Hata wimbo wa Kamili Gado ulikuwa maalumu kwake.....Mke wangu ni mrembo sana yupo Kamili gado...." Prof Jay.
Mh. Joseph Mbilinyi ' Sugu' (kushoto) akiwa na maharusi
Kwa upande wa wahudhuriaji Mbunge wa Hai na kiongozi wa Kambi rasmi ya upinzani bungeni, Freeman Mbowe alitoa pongezi kwa Prof Jay huku akimuuita ni mbunge mjanja.
"Sisi tunakupongeza kwa hatua nzuri uliyochukua, tunakutakia maisha mema wewe na familia yako. Lakini unaona Wabunge wa vyama vyote wako hapa ni kwa sababu wanakuthamini kwa kuwa na wewe unaheshima sana unyeyekevu japokuwa wewe ni mbunge mjanja sana. Tunakutakia mafanikio katika Siasa yako, biashara na sanaa" Mh. Mbowe.
Mjumbe wa kamati kuu Chadema na Waziri Mkuu mstaafu Edward Lowassa akipunga Mkono ukumbini kwenye harusi ya Prof Jay.
Prof Jay aliungana katika tafrija ya kusherehekea kuuaga ukapera jana usiku katika ukumbi wa Mlimani City pamoja na Wabunge wenzake, Viongozi wa CHADEMA, Wasanii mbalimbali, ndugu jamaa na marafiki pamoja na mashabiki zake.
Uongozi wa EATV LTD unampongeza Mh Joseph Haule kwa kupiga hatua nyingine katika maisha yake.

No comments

Powered by Blogger.