ad

ad

Singidani (A Story From My Heart) - 2



MARA kadhaa watu walikuwa wakimwangalia na kumnyooshea vidole wakisemezana ndani ya ukumbi huo. Wengine walimfuata na kumsalimia huku wengine wakitaka hata kupiga naye picha tu.
Kwa msichana huyu ni tofauti. Hana muda naye kabisa. Pengine silaha ya kwanza haikuwa na nguvu au msichana yule si mpenzi wa filamu kwa hiyo hamfahamu.
Labda!
Bado alikuwa na silaha nyingine. Mavazi ya gharama aliyokuwa amevaa yalikuwa ni silaha kwa msichana yeyote wa mjini. Chris alikuwa amependeza sana. Alivaa kawaida tu, lakini alipendeza vilivyo.
Silaha hiyo nayo imeshindikana!
Chris akabaki akimsindikiza kwa macho mpaka alipoishilia. Akaanza kupiga hatua za taratibu kurudi alipokuwa amekaa awali. Lengo likiwa ni kuendelea na mawazo yake yaleyale!
***
Macho ya Chris ni kama yalizingirwa na ukungu. Akaamua kuyapekecha kidogo ili kuuondoa ili aweze kuangalia vizuri. Kweli kabisa...alichokiona ni sahihi.
Ni yule msichana alikuwa anacheza na kundi la vijana watano. Wale vijana walikuwa wamemzunguka, yeye akawa katikati yao. Kuna wakati, walianza kuingia katikati mmojammoja na kucheza na yule mrembo kwa zamu.
Lilikuwa onesho la bure lililovutia ambalo lilisababisha wengine waache kucheza, wabaki kuwaangalia wao. Chris akafura!
“Yaani wale watoto ndiyo wanaweza kushindana na mimi? Haiwezekani. Mimi ni mtoto wa mjini...” akawaza Chris akiinuka kusogea karibu na lile duara la vijana watano wakicheza na msichana yule mrembo!
Yule anayeusumbua moyo wake.
Mtikisiko wa moyo ulimvaa Chris. Hasira zikamkaba rohoni. Aliumizwa na msichana yule mrembo ambaye alikataa hata kumsalimia tu wakati tayari alikuwa ameshaufanya moyo wake mateka. Hasira zake sasa zilihamia kwa wale vijana.
Chris akajikaza na kusimama kisha akasogea karibu na wale vijana. Akatoa macho. Hata yeye alijishangaa ni kwa nini alikuwa na hasira kiasi kile.
Yule msichana hakuwahi kumfahamu kabla na hakuwa mpenzi wake. Kwa nini achanganyikiwe? Labda ni mapenzi, lakini kwa nini awakasirikie watu wengine ambao hawafahamu?
Alikiri moyoni mwake kwamba alifanya makosa.
“Nakosea sasa...nadhani huu umaarufu wangu unataka kunidanganya. Natakiwa kuwa mpole kwanza...” akawaza.
Kitu alichogundua kwa haraka ni kwamba alitakiwa kupata liwazo kidogo. Ingekuwa rahisi zaidi kuliwazwa na msichana yule lakini kwa sababu anajifanya anamkataa, Chris alikuwa na kitulizo kingine.
Alichepuka haraka hadi kwenye kaunta ndogo ya pembeni katika ukumbi ule. Akamvaa msichana aliyekuwa akihudumia.
“Nataka toti tatu za Grant’s haraka tafadhali,” akasema Chris akiweka noti moja ya elfu kumi mezani.
“Kaka Chris hata salamu?” yule mrembo akamwambia.
Chris akageuza uso, akakutana na msichana mrembo, mweupe, mrefu, mwenye macho makubwa ya kung’ara. Alijilaumu sana.
“Wakati mwingine unaweza kupoteza cast hivihivi...huyu msichana anafaa kuigiza,” akawaza akitabasamu.
“Habari yako dada yangu?”
“Salama, sasa mambo si hayo? Kwani ulivyonisalimia umekufa?”
Chris akacheka.
“Wewe utakuwa unatoka katika makabila mawili tu ya hapa Singida, kama siyo Mnyaturu utakuwa Mnyisanzu.”
“Mh! Wewe umejuaje? Mimi Mnyaturu.”
“Umeona sasa! Nilisema tu, nimefurahi kuwa mtabiri mzuri,” alisema Chris huku akiondoka zake.
Anarudi kulekule! Msichana hana jipya kwake, anamtaka yule ya mwanzo. Kadiri muda unavyozidi kwenda anazidi kuwaza tofauti. Si kwamba alimtaka msichana yule kwa usiku mmoja tu; aliwaza ndoa kabisa.
Ilikuwa mapema sana kwake kuanza kuwaza mambo makubwa kama yale lakini ndicho kilichokuwa kichwani mwake. Potelea mbali, hata kama akigombana na baba yake mzee Shila, bora aishi na yule mrembo!
“Nimeshajua cha kufanya!” akajisemea Chris akipiga funda moja dogo, akachanganya na mate, akameza.
Itaendelea wiki ijayo.

Powered by Blogger.