ad

ad

Msuva: Baba baki na Simba

Mfungaji bora wa msimu uliopita wa Ligi Kuu Bara na mshambuliaji ya Yanga, Simon Msuva.

MFUNGAJI bora wa msimu uliopita wa Ligi Kuu Bara, Simon Msuva, amemwambia baba yake mzazi, Happygod Msuva, amuache na Yanga yake na yeye abaki na Simba yake.
Kauli hiyo ameitoa ikiwa ni siku chache tangu baba yake atangaze kumzuia mwanaye kuongeza mkataba mwingine Yanga mara huo alionao utakapomalizika ili aende Simba au akacheze soka la kulipwa.
Kiungo huyo, hivi karibuni alitangazwa kuwa mchezaji bora wa msimu uliopita, huku akifanikiwa kutwaa tuzo ya ufungaji bora kwa kupachika mabao 17 akifuatiwa na mshambuliaji wa Yanga Mrundi, Amissi Tambwe.
Akizungumza na Championi Jumatano, Msuva alisema kuwa kikubwa baba yake anatakiwa kutambua soka kwake anachukulia kama ajira inayoendesha maisha yake ya kila siku.
Msuva alisema, baba yake anachukulia soka kama burudani kwake kutokana na kuwepo na mapenzi na Simba. Lakini amesisitiza yeye hachezi soka kwa ajili ya kumfurahisha baba yake, hivyo ni vyema akafahamu hilo.
“Ujue mara nyingi nimekuwa nikimzuia baba yangu kuongea na waandishi kwa kuhofia kuongea tofauti kwa hofu ya kunigombanisha na viongozi, pia mashabiki wa Yanga.
“Watu wengi wanajua kama baba yangu ni Simba, hivyo anavyoongea tofauti kuhusiana na mimi na timu yangu ya Yanga, mimi ndiye ninayeathirika kwa kukosa uaminifu kwa mashabiki.
“Hivyo, nikwambie tu mimi sina mpango kwa hivi sasa wa kuondoka Yanga na ninaomba nimwambie kuwa, yeye abaki na Simba yake na mimi aniache na Yanga yangu.
“Kwa sababu mimi bado ni mchezaji halali wa Yanga mwenye mkataba wa mwaka mmoja ambao unatarajiwa kumalizia Juni, mwakani ni vyema akalifahamu hilo,” alisema Msuva.

No comments

Powered by Blogger.