ad

ad

TOROJO BAMIA (Winga teleza) - 05





“Nina imani elfu inakutosha, una jingine?” Suzy alinyoosha mkono kumpa Shuku lakini hakupokea kitendo kilichomuuzi Suzy na kumkazia macho kumuuliza.
“Kuna mtu kakutuma? Haya niambie.”
“Sivyo hivyo Suzy.”
“Sasa unashida gani Shuku? Unajua kuna sehemu nawahi kuna ofa.”
“Nashida na wewe,” Shuku alijikakamua.
“Mimi?” Suzy alishtuka na kujishika kifuani.
“Eeh.”
“Shida gani?”
“Unajua Suzy nateseka kila nikuonapo.”
“Mmh! Makubwa, jamani mbona mapya, Shuku mimi nikutese wewe? Nimegeuka mchawi nakuchukua usiku na kukugeuza fisi?”
“Hapana Suzy kimapenzi.”
“Unamaanisha unanitaka niwe mpenzi wako?”
“Ndi..ndi..yo Suzy.”
“Muone huna hata haya hata kuzungumza huwezi unajua kabisa mimi si saizi yako. Shuku umenidharau kiasi gani kunisimamisha na kunieleza ujinga wako?” Suzy alikuja juu na kupaza sauti iliyosikika umbali mrefu.
“Si..si..hivyo..Su..su zy...na..na kupenda.”
“Shuku mbona unataka kunitia nuksi huko niendako mambo yangu yaende ndivyo sivyo.”
“Lakini Suzy mpenzi hayapo hivyo nami nina haki ya kuyasema mateso yangu kwako.”
“Hebu niangalie,” Suzy alisema kwa sauti huku akijigeuza mbele ya Shuku kitu kilichomfanya Shuku ajute kumsimamisha mbele za watu na kujiona kama kavuliwa nguo. Alitamani kukimbilia kuepuka aibu ile lakini miguu ilikuwa mizito alibakia kasimama kama sanamu.
“Jamani mimi ni hadhi ya Shuku?” aliwauliza mashoga zake kwa sauti ya juu waliokuwa mbali kidogo na yeye.
“Ha! Ndicho alichokusimamishia?” waliuliza.
“Eti jamani mbona leo kajua kunitia nuksi, najiona kama nimekutana na paka mweusi.”
Yalikuwa maneno yaliyomdhalilisha Shuku na kujiona kama kajipaka kinyesi, Shuku akiwa ndani ya gari aliyawaza yale yaliyomfanya awaogope wanawake wazuri  kama ukoma. Alijiuliza siku ile yule demu na shoga zake waliomtoa nishai wakimuona yupo vile watasemaje.
Alikwenda kupiga picha na  kuzipeleka kwa mkuu wa usalama barabarani, kisha alirudi uswazi kwake kulipa kodi ya nyumba. Alipokaribia nyumba aliyokuwa akiishi alifungulia muziki kwa sauti ya juu na kuwafanya wote kuliangalia lile gari.
Alilifunua na kuwafanya wote waliokuwa wamekaa akiwemo Suzy kulishangaa lile gari lilionekana la ajabu mtaani,alilipaki pembeni ya nyumba anayoishi.
Alitulia kidogo kabla hajateremka kuwaacha watu washangae kwa muda kisha alilifunga na kutulia tena kabla ya kuteremka huku kila mmoja akimtumbulia macho. Suzy na kampani yake walijiuliza zungu la unga limetoka wapi. Baada ya kutembea kuelekea ndani wote walishtuka kumuona Shuku.
“Suzy yule si Shuku?”
“Hapana Shuku awe vile labda ndugu yake.”
“Hapana ni Shuku.”
“Makubwa mbona tutakoma, gari na pamba kali katoa wapi?”
“Najua?”
“Mmh! Inawezekana alinitongoza akijua mimi ni hadhi yake, maskini sikujua,” Suzy alijikuta akijilaumu kumkataa Shuku.
“Dharau zako shoga, lakini bado una nafasi, sasa zamu yako  kujipendekeza kwake,” shoga yake alimshauri.
“Naona aibu.”
“Aibu ya nini wakati ni jambo la kawaida bila kuwa kauzu mjini hatukai.”
Wakati wakijadiliana na hali ya Shuku, ndani walimpokea kwa mshtuko.
“Jamani hodi,” Shuku aliingia kwa mama mwenye nyumba.
“Ha! Shuku?” alishtuka kumuona alivyolipuka.
“Ndiyo mimi mama.”
“Ha! Mwanangu siamini!”
“Amini mama ni mimi.”
“Karibu mwanangu.”
“Asante, sasa mama mi si mkaaji kile chumba alichohama mtu jana kina mtu?”
“Hakina baba.”
“Sasa mama, sasa hivi nitalipia miaka miwili na deni ulilokuwa ukinidai.”
“Hakuna tatizo baba, tena utakuwa amenisaidi maana hali ilikuwa tata.”
“Ila chumba changu kitakuwa na vitu vyangu nami nitakuja siku moja moja, lakini sasa hivi nina maisha mengine kabisa.”
“Jamani Shuku sasa hivi unaishi wapi?”
“Utajua muda si mrefu mama.”
Shuku alimuhesabia fedha ya miaka miwili na deni kisha alimpa elfu ishirini ya soda.
“Asante mwanangu, Mungu akuzidishie huku uliko.”
“Atuzidishie wote, ila baada ya muda nitakuja kubadili vitu vya ndani, na hii fedha atampa salmini amihamishie vitu vyangu.”
Shuku baada ya kulipia pango miaka miwili aliagana na mama mwenye nyumba na kuelekea kwenye gari lake. Wakati anatoka aliwakuta wale wanawake wakisumbiri kwa hamu wamuone kwa mara nyingine, Shuku aliyelipuka pamba za nguvu na kamba nzito shingoni, chini alikuwa na raba kali. Kwa jinsi alivyokuwa hakukuwa na mwanamke yeyote anayeweza kusimamishwa na Shuku akakataa.
Kabla ya kutoka nje alivaa miwani ili aweze kuwasanifu waliombele yake, alipofika mbele ya gari lake aliwatazama wale wasichana macho yalivyowatoka kama wameona meli barabarani, Shuku alichekea moyoni. Kabla ya kuondoka walitokea washkaji zake waliokuwa wakirudi toka kwenye mihangaiko, kwanza walimpita bila kumjua alipowaita ndipo waliposhtuka na kushangazwa na maajabu ya dunia.
“Shuku ni wewe?”
“Ni mimi ndugu zangu.”
“Mbona kama njozi ni asubuhi tulikuwa pamoja ajabu sasa hivi umekuwa kama mtu wa hadithini?”
“Ni historia ndefu ila tutazungumza wiki endi.”
“Sasa tuachie basi mshiko, yaani baada ya kuachana asubuhi siku ya leo imekuwa na gundu tupu.”
“Poa wangu,” Shuku aliingiza mkono mfukoni na kutoa fedha alizozihesabu kwa kuzionesha ili wale wasichana waone na kuhesabu elfu therasini na kumpa kila mmoja elfu kumi kisha aliwaaga rafiki zake.
“Sasa washikaji ngoja nirudi nikapumzike, nilikuja kulipia chumba changu pia nilipitia kwa mkuu wa trafiki kwa ajili ya leseni si mnajua sina gamba sitaki nikitembea na gari nipate usumbufu.”
“Mmh! Hatukuwezi, sasa ndo upo anga zipi?”
“Mtajua tu washikaji zangu nikija jumapili mtaelewa.”
Baada ya kusema vile aliingia kwenye gari, kabla ya kuondoka alilifunua gari na kuwafanya rafiki zake wapige kelele za mshangao.
“Wawooo, si mchezo mwana una kitu cha nguvu mwaka huu wanga lazima wazime zao.”
“Poa washkaji baadaye,” Shuku alisema huku akiwasha gari aondoke. Wakati Shuku akiagana na rafiki zake ili aondoke zake Suzy na shoga zake walikuwa kwenye kigagaziko kikubwa wafanye nini ili kumnasa Shuku.
“Sasa jamani nitafanyaje na Shuku ndio anaondoka?” ITAENDELEA KESHO HAPAHAPA

KAMA ULIKOSA SEHEMU ZA NYUMA SOMAHAPA

1.SOMA SEHEU YA KWANZA >>>www.2jiachie.com/2014/06/torojo-bamia-winga-teleza-01.html
2. SEHEU YA 2: >>www.2jiachie.com/2014/06/torojo-bamia-winga-teleza-02.html
3. SEHEU YA 3: >>www.2jiachie.com/2014/06/torojo-bamia-winga-teleza-03.html

No comments

Powered by Blogger.