BEYOND LOVE- (ZAIDI YA MAPENZI) SEHEMU YA 40 MPAKA YA 41
Beyond Love- 40
Kama mapenzi ni raha, basi
kwa Mariam hayakuwa na maana yoyote, kwani siku zote yameendelea kuwa msumari
wa moto katika maisha yake. Kila anapokaribia kupata faraja, lazima kuna kitu
kinaingia na kuharibu furaha hiyo. Mariam anakuwa mtu wa kulia kila siku.
Machozi hayakauki machoni mwake. Yote hayo yanasababishwa na mwanaume mmoja tu,
Tom, ambaye hathamini wala kuheshimu penzi lake.
Anapata mateso makubwa,
kusimangwa, kufukuzwa nyumbani na mengine mengi. Jambo linalosababisha aamue
kukimbia mji na kwenda kwa bibi yake anayeishi Matombo, Morogoro. Akiwa huko
anaanza maisha mapya na kufanikiwa kumsahau kabisa hadi pale alipoona gazeti
mjini alipotumwa na bibi yake.
Matatizo yakafumuka! Akaanguka
na kupoteza fahamu ambapo kijana Ramsey ndiye aliyejitolea kumsaidia hadi
alipopata nafuu akasafiri naye hadi Dar es Salaam na kwenda kumwangalia Tom
aliyekuwa amelazwa.
Mariam anakuwa tayari
kugombana na wazazi wake kwa ajili ya Tom, anaamua kuishi hotelini na Ramsey
ambaye baadaye anamtaka kimapenzi jambo lililopingwa vikali na Mariam. Hata
hivyo baadaye anamkubalia, lakini hakuwa tayari kufanya naye mapenzi, kitu
kilichomuudhi sana Ramsey aliyeamua kumuacha na kurudi zake Morogoro.
Mariam akaamua kujiua, lakini
kabla ya hajafanya hivyo anajikuta akijisikia mwenye dhambi sana kujitoa uhai
wake. Akaamua kuahirisha, hapo ndipo alipoona umuhimu wa kwenda kwa wazazi wake
ambao walimpokea kwa mikono miwili.
Akiwa nyumbani kwa wazazi
wake, anapanga safari ya uongo ya kwenda kwa rafiki yake Clara, lakini ukweli
ni kwamba alikuwa anakwenda Muhimbili. Huo ukawa ndiyo utaratibu wake wa kila
siku, hadi siku apoamua kusema ukweli mbele ya mama yake.
Mzozo mkubwa unaibuka lakini
mwisho wake, Mariam anaamua kurudi nyumbani kwake Mbezi, anakuta nyumba chafu
sana yenye mpangilio mbovu, anaweka vitu sawa na kufanya usafi kisha anaanza
maisha upya huku jambo kubwa linalokuwa mbele yake likiwa ni kumhudumia Tom.
Miaka minne badaye, Tom
anazinduka mbele ya Mariam, anamfukuza akimwambia aondoke kwani Mayasa akifika
ingekuwa ugomvi! Kwa kifupi Tom amekupoteza kumbukumbu kabisa, lakini baadaye
anapata picha kwamba alivamiwa na majambazi usiku akiwa anarudi nyumbani.
Tom anapooza kuanzia shingoni
hadi miguuni, taarifa ambazo Mariam alipewa! Mariam hamwelezi Tom ukweli juu ya
kifo cha mama yake. Kila anapomuuliza, anajaribu kumficha! Lilikuwa jambo gumu
sana kumweleza Tom kwamba mama yake alifariki dunia, tena alizikwa na
Halmashauri ya Jiji. Je, nini kitatokea? SONGA NAYO....
Hakukuwa na kitu kingine chenye thamani katika
maisha ya Tom kama mama yake, hapakuwa na mtu muhimu zaidi maishani mwake kama
mama yake! Kwa Tom, mama yake alikuwa kila kitu. Alikuwa uhai wake, furaha
yake, kila kitu chake. Kumuona mama yake akiwa hai tu, ilitosha kabisa kumfanya
mwenye furaha siku zote.
Sasa
mama yake hayupo tena duniani, mbaya zaidi hajui na wala hana taarifa zozote
juu ya kutokuwepo kwa mama yake duniani. Pamoja na kutokujua hilo, moyo wake
ulikuwa mzito kuliko kawaida, alihisi kama ganzi fulani ikizunguka moyoni
mwake, alihisi kitu.
Tom
akayatoa macho yake katika hali ambayo hata Mariam mwenyewe alishindwa kuelewa
kilichokuwa akilini mwake. Midomo yake ikaanza kutingishika.
“Mariam!”
“Nakusikiliza
mpenzi wangu!”
“Unanipenda?”
“Hata
moyo wako unalitambua hilo!”
“Utakuwa
tayari kuniacha niendelee kuumia?”
“Hapana!”
“Unaweza
kumdanganya mpenzi wako?”
“Hapana!”
“Nahitaji
kujua ukweli, mama yangu yupo wapi?!” Tom alisema akiwa hana chembe ya furaha
usoni mwake.
“Unamaana
gani?”
“Nataka
kujua mama yangu alipo!”
“Ngoja
nikuambie ukweli mpenzi wangu, jana nilienda nyumbani nikiwa na furaha sana,
nilitamani sana kukutana na mama ili nimweleze kuhusu hali yako, lakini
nilipofika nyumbani sikumkuta mama, aliacha maagizo kwamba anakwenda nyumbani
Musoma, lakini majuzi alikuwa akinieleza nia yake ya kuanza kukushughulikia
kienyeji, nadhani atakuwa huko,” Mariam akasema maneno hayo akiwa macho makavu.
Haikuwa
rahisi kupingana naye, hasa kutokana na jinsi alivyokuwa akizungumza kwa
kujiamini huku macho yake akiwa ameyatuliza usoni mwa Tom ambaye alianza
kuamini maneno ya Mariam.
“Sawa
mpenzi wangu, kama ni kweli, lakini kama ni uongo ni wazi kwamba hunipendi!”
“Nakupenda
mpenzi wangu!”
“Lakini
kuna kitu nahisi!”
“Ondoa
hisia nyingine zozote nje ya penzi lako la kweli kwangu mpenzi wangu!”
“Ok!”
Tom akajibu.
Jambo
hilo likaisha wakiwa na maelewano kwa pamoja, Mariam akambusu Tom midomoni
mwake, macho yake yalikuwa yanazungumza jambo, lakini bado akaongezea kwa
kinywa chake.
“Nakupenda
sana Tom!”
“Nakupenda
pia Mariam wangu!”
******
Tom
aliendelea kukaa hospitalini kwa mwezi mzima zaidi huku hali yake ikiendelea
vizuri lakini hakuweza kuinuka kitandani. Marim alikuwa msaada pekee kwa Tom,
lakini siku zote hakumweleza ukweli wa kifo cha mama yake.
Hiyo
iliendelea kuwa siri iliyopo katikati ya moyo wake. Baada ya miezi miwili, Tom
aliruhusiwa kurudi nyumbani kwa sharti la kupelekwa Kliniki kila baada ya mwezi
mmoja kwa ajili ya kuangalia upya maendeleo ya afya yake.
Hilo
ndilo lililofanyika, maisha hayakuwa mazuri nyumbani kwao kwani hawakuwa na
uwezo kifedha wala vitega uchumi vya kuwaingizia kipato. Siku moja usiku wakati
wa chakula cha usiku, Mariam alimweleza mumewe wazo alilokuwa nalo juu ya
maisha yao.
Waliishi
kwa upendo na Tom hakumkumbuka tena Mayasa, alimfananisha na shetani ambaye
aliharibu maisha yake, kwake Mariam akawa ndiye kila kitu. Maisha yale magumu
hayakumfurahisha kabisa Mariam, alitakiwa kufanya jambo moja muhimu sana ili
kuyafanya maisha yao angalau yawe yenye furaha kutokana na kutengwa kwao na
watu wanaowazunguka hasa wazazi wa Mariam ambao kwa wakati huo wangepaswa kuwa
msaada pekee kwa maisha yao.
“Baby
kuna kitu nimefikiria kwa muda mrefu sana na kupata ufumbuzi,” Mariam
akamwambia Tom aliyekuwa ameegemea kwenye mto, akila.
“Ni
nini hicho mpenzi wangu?”
“Tutaishi
maisha haya hadi lini?”
“Unamaanisha
nini mpenzi?”
“Maisha
haya yasiyo na uhakika wa kesho, tutaendelea nayo hadi lini? Lazima nifanye
kitu mpenzi wangu!”
“Umefikiria
kufanya nini?”
“Nadhani
ni bora nitafute kazi.”
“Sawa,
naungana na wewe!”
Ndivyo
ilivyokuwa, siku iliyofuata Mariam akaanza kutafuta kazi sehemu mbalimbali
jijini Dar es Salaam, alituma maombi sehemu nyingi sana na mwishowe akaitwa
katika Benki ya CRDB kwa ajili ya usaili. Baada ya kufanyiwa usaili akabahatika
kuchaguliwa kuanza kazi rasmi kama Afisa Biashara wa Tawi la Vijana jijini Dar
es Salaam.
Wiki
moja baadaye Mariam akaanza kazi rasmi katika Benki ya CRDB Tawi la
Vijana. Maisha yakabadilika,
alichokifanya ni kumuajiri msichana wa kazi ambaye alikuwa akimhudumia mumewe
Tom. Waliishi maisha ya furaha sana, kwake kumuona Tom akitabasamu ilitosha
kabisa kumfanya awe mwenye furaha.
Kila
ifikapo mwisho wa mwezi alihakikisha anampeleka hospitalini kwa ajili ya
kufanyiwa uchunguzi zaidi. Kila kitu kilikwenda sawa, lakini tatizo lilikuwa
moja tu, kila Tom alipouliza kuhusu mama yake, alijibiwa kwamba yupo kijijini.
Jioni moja, hali ilikuwa tofauti, Tom akamwambia kama ni kweli mama yake
alikuwa amekwenda kijijini, basi aende akamfuate.
“Lakini
alisema atakuja.”
“Kwani
ni muda gani tangu nimetoka hospitalini?”
“Ni
mrefu ndiyo!”
“Sasa
kama ndivyo, unadhani mama anaweza kukaa muda mrefu kiasi hicho bila kuja
kutizama hali yangu? Haiwezekani Mariam, kuna kitu unajaribu kunificha, naomba
nieleze ukweli Mariam, mama yangu yupo wapi?” Tom alibadilika, alionyesha ukali
ambao hata Mariam mwenyewe hakuutarajia kabisa.
Mariam
akashindwa kuzungumza, akajikuta machozi yakianza kuchuruzika machoni mwake
kama maji! Alianza pole pole, lakini akajikuta anaanza kulia kwa sauti kubwa zaidi
huku akitaja jina la mama yake na Tom.
“Kwani
kuna nini?”
Mariam
hakujibu.
“Kuna
kitu unajaribu kunificha Mariam, tafadhali naomba niambie ukweli!”
“Tom,
sina sababu ya kuendelea kuificha siri hii!”
“Siri
gani?”
“Juu
ya mama!”
“Niambie
basi, kuna nini?”
“Naomba
usinifikirie vibaya Tom, ilikuwa lazima nitunze siri hii, lakini ni wazi kwamba
isingewezekana kuendelea kukaa nayo kwa muda mrefu zaidi. Naomba upokee taarifa
hii kama ilivyo. Uikubali, uiamini na uichukue kama ilivyo!”
“Mbona
sikuelewi Mariam, hebu naomba nieleze kinachoendelea, achana na mafumbo ambayo
ni giza kwangu!”
“Tom
mpenzi wangu, nakuomba sana, usipaniki juu ya hili nitakalokuambia mume wangu!”
“Kama
hutaki kusema acha...maana naona unanitibua sasa!”
“Siyo
hivyo mpenzi, ni kwamba....mama alishafariki Tom!” Mariam akasema akihema kwa
kasi sana.
“Unasemaje?”
“Mama
alishafariki....” Mariam hakuweza kumalizia sentesi yake, tayari mvua ya mchozi
ilishafunika macho yake.
Huzuni
ikatanda chumba kizima.
Je,
nini kitatokea? Fuatilia
Beyond
Love- 41
Baada
ya Mariam kuitunza siri ya kifo cha mama yake Tom kwa muda mrefu, hatimaye
ameamua kuanika ukweli hadharani! Amemweleza ukweli Tom, ambaye ameonyesha
kushtuka sana. Je, nini kitatokea? Nini hatma ya wawili hawa? Hebu SONGA NAYO
sasa katika sehemu hii ya mwisho ya simulizi hii yenye mafunzo makubwa kwa
jamii...
“Kwanini
ulinificha jambo hili siku zote?”
“Ilikuwa
ni mapema sana kukuambia mpenzi wangu, lakini nakuomba sana tena sawa, piga
moyo konde, huo ndiyo ukweli ambao hakuna kitu cha kuweza kuubadilisha!”
“Mama...umekufa
nikiwa bado nakuhitaji mama yangu...bado nilikuwa nahitaji sana busara zako
mama yangu...umeniacha na upweke mama! Sina la kufanya mama yangu, nenda mama
nasi tupo njia moja na wewe!” Tom alisema maneno hayo akilia sana.
Kila
alipokumbuka mapenzi ya mama yake kwake, alizidi kuchanganyikiwa, mama yake
alikuwa kila kitu katika maisha yake, kila alipokumbuka shida na dhiki zote
walizopitia ndivyo alivyozidi kupatwa na machungu. Tom alizidi kulia.
“Nyamaza
mume wangu mpenzi, kashaenda huyo, Mungu amemwita katika ufalme wake, hakuna
kinachoweza kumrudisha, mwache apumzike kwa amani. Kazi yetu kubwa kwa sasa ni
kumwombea tu!”
“Mungu
amlaze mahali pema peponi!”
“Amen!”
“Inabidi
unipeleke mahali alipolala mama yangu, natakiwa kupaona, angalau ning’olee hata
majani juu ya kaburi lake!”
“Naomba
uvumilie na hili mpenzi wangu!”
“Lipi?”
“Mama
amezikwa na Halmashauri ya Jiji!”
“Unasema?”
“Huo
ndiyo ukweli Tom, wakati mama anafariki sikuwa Dar, nilipata taarifa hizi
nikiwa Morogoro kama nilivyokuambia mwanzoni!”
“Mama
yangu anazikwa kama mbwa? Anakosa heshima anayostahili binadamu? Nimekukosea
nini Mungu wangu mimi jamani? Kwanini mambo haya yanatokea kwangu tu jamani?
Kwanini? Kwanini lakini?” Tom alipiga kelele, lakini Mariam akajitahidi
kumnyamazisha.
Ilikuwa
kazi ngumu sana, lakini mwisho wake Tom akanyamaza. Kila alipokumbuka sura ya
mama yake, Tom alikuwa akimwaga machozi. Mama yake alikuwa ni kila kitu katika
maisha yake. Maisha yaliendelea kama kawaida, kasoro kubwa ikiwa ni ulemavu
alionao Tom pamoja na kumkosa mama yake mzazi.
Lingine
kubwa zaidi ni kwamba, mpaka wakati huo, wazazi wa Mariam waliamua kumtenga,
hawakutaka kushirikiana naye kwa jambo lolote. Walimwachia maisha yake na Tom,
ambaye kwao alikuwa sawa na shetani. Yote hayo hakuwa aliyeyaweka akilini wala
kuona kama kuna tofauti kubwa sana katika maisha yao. Kwako upendo wa kweli
ndiyo ulikuwa kila kitu.
MWAKA MMOJA BAADAYE
Jambo
kubwa lililofanyika ndani ya mwaka mmoja, ilikuwa ni kurudisha uhusiano kati ya
wazazi wa Mariam na wao, ilikuwa kazi ngumu sana, lakini kwa kupitia wazee
wenye hekima, suala hilo liliisha bila matatizo. Wazazi wa Mariam wakawasamehe
Tom na Mariam kwa yote yaliyotokea, wakafungua ukurasa mpya.
Wakawa
wanatoa ushirikiano kwa kila kitu, hata katika mambo yaliyohusu fedha, kila
kitu kikawa kimepita, wakawa karibu wakihangaikia afya ya Tom pamoja. Mpaka
muda huo Tom alikuwa bado hajaamka kitandani, mwili wake ulikuwa umepooza.
Pamoja
na juhudi za mkewe na wazazi wake kumuhangaikia katika Hospitali mbalimbali,
ndani na nje ya nchi, lakini mafanikio yalikuwa hakuna. Mariam alifikia hatua
ya kuchukua mkopo kazini kwao ili aweze kumhangaikia Tom wake, angalau aweze
kuamka, lakini ilishindikana.
Hilo
lilizidi kuongeza maumivu katika ndoa yao, ambayo yeye aliifananisha na ndoa ya
mateso. Hata hivyo, mara zote Tom alikuwa akimkataza juu ya matumizi makubwa ya
fedha kwa ajili ya kuhangaikia afya yake, akisisitiza kwamba haikuwa rahisi
kupona.
“Lakini
kwanini unasema hivyo mpenzi wangu? Napenda sana kukuona ukiamka tena!”
“Sawa,
lakini naamini nitaamka siku ambayo Mungu mwenyewe atakuwa ameichagua!”
“Hapana
darling, hupaswi kukata tamaa mapema kiasi hicho!”
“Lakini
pia hupaswi kutumia fedha nyingi kiasi hiki katika jambo ambalo linaonekana
dhahiri kuwa ni gumu kufanikiwa!”
“Unanikatisha
tamaa tu mpenzi wangu!”
Hayo
ndiyo yalikuwa maisha yao, kila kukicha Mariam alikuwa akihangaika kutafuta
dawa hadi za kienyeji kwa ajili ya kurudisha afya ya Tom, lakini haikuwezekana.
Pamoja na hayo, kuna jambo moja ambalo lilimshangaza sana Mariam.
Tom,
alikuwa na kawaida ya kumuita Mariam akionyesha kutaka kumwambia jambo, lakini
akifika ghafla anaonekana kusahau. Tatizo hilo liliendelea kwa mwaka mmoja
zaidi, kiasi kwamba Mariam akawa anampuuza, kwani kila anapotaka kusema
anajikuta amesahau.
“Lakini una nini Tom? Mbona kila unapotaka kusema
jambo unasahau?”
“Hata
mimi nashindwa kuelewa, ila ni jambo muhimu sana, kila nikitaka kusema nashangaa
nasahau, lakini kuna siku nitakumbuka, na utaona jinsi jambo hilo lilivyo kubwa
na muhimu!”
“Haya
hebu tungoje huo muujiza!”
Hiyo
ikaendelea kuwa kawaida ya Tom, kila mara alimwita mkewe na anapotaka kusema
anaonekana kusahau. Mariam alihuzunika sana, alishindwa kuelewa mumewe alikuwa
na jambo gani kubwa kiasi kile, na analisahau kila anapotaka kusema. Mariam
akaamua kwenda kwa Dokta wake, ambaye alimwambia kwamba ile ilikuwa hali ya
kawaida na kumbukumbu zake zitaendelea kurejea taratibu.
“Kweli
Dokta?”
“Ndivyo
ilivyo, inaonekana aliumia kidogo, sehemu ya ubongo wake, ndiyo maana anapoteza
kumbukumbu, lakini zitaendelea kurudi polepole!”
“Kweli
kabisa?”
“Nakuhakikishia!”
“Nashukuru
sana Dokta!”
“Ok!”
**********
Ilikuwa
ni Jumamosi usiku, tayari Tom na mkewe walikuwa wameshalala. Ulikuwa ni usiku
wa saa saba na dakika zake. Mariam akashtuliwa na Tom ambaye alikuwa akimvuta
kwa nguvu.
“Kuna
nini?”
“Amka,
amka haraka sana!”
“Nini
saa hizi Tom?”
“Amka
nimeshakumbuka, amka haraka kabla sijasahau!”
“Enhee
sema!” Mariam akasema akiwa ameshawasha taa.
“Sikiliza
kwa makini sana!”
“Nakusikiliza!”
“Nenda
nje sasa hivi, pale kwenye ule mlimao, fukua chini kisha utoe kiroba
utakachokiona!”
“Kina
nini?”
“Kina
madini, nilikuwa najitahidi sana kuvuta kumbukumbu, afadhali sasa nimekumbuka!”
“Unasema
kweli Tom?”
“Huo
ndiyo ukweli, nenda haraka kaangalie kama bado kipo!” Tom alisema haraka haraka
huku akihema kwa kasi sana.
Mariam
akatoka na jembe usiku huo bila kuogopa, kukuta kile kiroba kungemaanisha
kuachana na maisha ya umasikini tena. Maisha yao yangekuwa mapya yasiyo na
chembe ya dhiki. Alipofika nje, zoezi la kuchimba eneo la kuzunguka ule mlimao
lilianza haraka sana.
Hakufika
mbali sana, akaanza kuhisi kitu kigumu, aliendelea kidogo, akaona mfuko wa
salufeti, akauvuta kwa nguvu, ukatoka ukiwa na madini ndani yake. Akatoka nao
mbio hadi chumbani kwa mumewe. Hakusema kitu, walipoufungua walihisi
kuchanganyikiwa! Kile kiroba kilikuwa kimejaa dhahabu tupu!
“Umasikini
kwaheri....kwaheri umasikini...” Tom alipiga kelele akiwa haamini kilichotokea.
“Ndiyo
maana ulikuwa unasahau kila wakati? Yaani unasahau utajiri?” Marim akamwambia
Tom akicheka.
“Yaani
acha tu, Mungu mkubwa mke wangu! Sasa andaa safari kabisa, kesho nenda Nairobi
ukauze sehemu ya haya madini ili upate nauli ya kwenda Marekani ukaeze dhahabu
yote huko!”
“Sawa!”
Usiku
huo hawakuweza kulala, walikuwa wakipanga mipango mbalimbali juu ya maisha yao
yajayo ambayo yangerejea kwenye utajiri kama kawaida.
“Mayasa
alikuwa hafahamu kama pale uliweka hizi dhahabu?”
“Nilimuamini
kwa kila kitu, lakini sijui ni kwanini sikumweleza kuhusu pale, ilikuwa ni siri
yangu mwenyewe!”
“Hakuna
mwingine zaidi ya Mungu mume wangu!”
“Na
ni kweli ni Mungu mwenyewe ndiye aliyefanya yote haya!”
Walizungumza
mambo mengi sana hatimaye wakalala, masaa manne baadaye walikuwa macho, Mariam
akijiandaa kwa safari ya kwenda Nairobi. Saa kumi na mbili kamili, Mariam
aliondoka na kwenda Uwanja wa Ndege, kwakuwa alishapanga mipango ya tiketi
mapema, haikuwa kazi kubwa sana, alifika na kuondoka na ndege ya saa moja
kamili.
Alifanikiwa
kufanya mauzo vizuri kisha akarejea Tanzania kabla ya safari nyingine ya kwenda
Los Angeles, Marekani. Huko akauza dhahabu yote na kurejea Tanzania akiwa na
mabioni yake.
“Pole
sana mke wangu!”
“Ahsante
baby, sasa ni wakati wa kupanga mipango yetu, hatuna muda wa kupoteza zaidi!”
“Ni
kweli!”
Ndicho
kilichofanyika, halikuwa jambo gumu sana kwao, kikubwa kilichofanyika ilikuwa
ni kununua majengo marefu (Towers) mengi jijini Dar es Salaam, Tanga, Arusha na
Mwanza. Hiyo ndiyo ikawa biashara yao kubwa. Fedha zilizobakia wakahifadhi
kwenye akaunti. Maisha yao sasa yakawa ya furaha, magazeti yakaanza kuandika
habari zao kwa fujo!
“Lakini
kuna jambo moja bado!” Mariam akamwambia Tom.
“Jambo
gani?”
“Lazima
usimame tena!”
“Unamaanisha
nini?”
“Pesa
itaongea, lazima tutafute tiba mpenzi wangu!”
“Hapana,
sitaki!”
“Kwanini?”
“Nilishasema
kabla, nitasimama siku Mungu mwenyewe akiamua!”
“Lakini
Mungu alisema jisaidie nami nitakusaidia!”
“Mimi
sitaki hivyo, nataka anisaidie yeye mwenyewe akitaka!”
“Haya
na tusubiri!”
Wiki
moja baadaye, Tom akamwagiza Mariam akamwite Mchungaji wa Kanisa wanaloabudu,
alitaka kufanyiwa maombi maalumu nyumbani kwake. Zoezi hilo lilifanyika haraka
sana, kila Jumapili yule Mchungaji alikuwa akifika nyumbani kwa akina Tom na
kusali pamoja naye.
Wiki
nne tu baadaye, wakiwa katikati ya maombi, Tom alishangaa akipata nguvu za
ajabu sana, akasimama. Halikuwa jambo jepesi kuamini, hata Mchungaji mwenyewe
hakuwa anaelewa jambo hilo kwasababu alikuwa amefumba macho.
“Yesu
ahsante, nasema ahsante sana Mungu wangu...siamini kama kweli leo nimesimama
tena!” Tom akapiga kelele huku akiimba.
Mchungaji
akafumbua macho, hakuamini macho yake, akaendelea kumuomba Mungu bila kukoma.
Mariam aliyekuwa nje, aliingia ndani baada ya kusikia kelele za Tom ndani. Naye
akashangazwa sana na jambo hilo, akaungana na mumewe kumshukuru Mungu.
“Mungu
wa ajabu jamani, leo ameamua kumuamsha mume wangu kitandani!”
“Amen!”
Ilikuwa
ni furaha kubwa kuliko kawaida, Jumapili iliyofuata Tom alikwenda Kanisani,
akapanda Madhabahuni kutoa sadaka ya shukrani kwa Mungu. Hapakuwa na machozi
tena baada ya pale, wakaishi kwa amani na furaha katika maisha yao. Mapenzi ya
kweli ndiyo yaliyotawala maisha yao.
“Nakushukuru
kwa yote mke wangu, umenivumilia katika kila hali Mariam. Sitaki kukumbuka tena
maisha yetu ya nyuma, lakini Mungu ni shahidi wa hilo kwamba wewe ni mwanamke
sahihi wa maisha yangu, mkombozi wangu. Naamini uliandaliwa kwa ajili yangu,
nakushukuru sana mke wangu, wewe ndiye wangu wa milele, nakuahidi sitakusaliti
tena, tuyaache yaliyopita yaende zake, tuanze maisha mapya yaliyojaa mapenzi!
Uliyonionyesha ni Zaidi ya Mapenzi, ahsante sana Mariam,” Tom alisema akiwa
kifuani mwa Mariam, huku machozi yakimiminika kama maji machoni mwake.
“Nilipanga
kukupa mapenzi ya kweli kama zawadi yangu kwako, wewe ndiye mwanaume wangu wa
kweli, nakupenda sana!” Mariam akasema, naye akishindwa kuzuia hisia zake,
akajikuta akimwaga machozi.
Haya
yalifanyika nyumbani kwao Mbezi, muda mfupi baada ya kutoka Kanisani. Wakaendelea
kukumbatiana zaidi, hawakuwa na kitu kingine vichwani mwao zaidi ya penzi la
kweli.
Mwisho.
N:B Nawashukuru sana wasomaji wangu kwa kufuatilia hadithi
hii kuanzia mwanzo hadi mwisho, naamini mmejifunza mambo mengi sana, kubwa
zaidi likiwa ni umuhimu wa penzi la kweli! Nawashukuru kwa kuniunga mkono.
Usikose katika hadithi mpya na nzuri kuliko kawaida.
Mungu
wangu awabariki sana. Ahsateni.

Post a Comment