KISA ANAKUPENDA KWA DHATI NDIYO UMTESE MPENZI WAKO?
Lakini wakati ukweli ukiwa hivyo, wapo wanaochukulia mapenzi kama
kitu rahisirahisi. Kitu ambacho anaweza kuingiza usanii na mambo
yakaenda.
Hapa namaanisha hivi, mtaani kuna watu wa aina mbili. Kuna ambao
wanajua kweli kupenda. Akisema anampenda fulani, anamaanisha na hata
ukimpasua moyoni mwake utakuta mtu huyo amechukua nafasi kubwa sana.
Lakini kuna wale ambao wanaweza kusema wamependa kumbe wametamani au
wana nia zao wanazozijua wenyewe. Unamkuta mwanaume anadanganya kuwa
ametokea kumpenda msichana fulani na ana dhamira ya kufunga naye ndoa
lakini kumbe hana lolote, nia yake amuonje kisha aingie mitini.
Achilia mbali hao, kuna wanaume ambao wanatumia pesa na utaalam wao
wa kuongea kuwarubuni wasichana ili watembee nao kwa kipindi fulani
kisha wakisharidhika, wanawaacha. Wavulana hao wapo na wamekuwa ni
tatizo kubwa huko mtaani.
Lakini pia wapo wasichana ambao wenyewe wanajiita wa mjini. Yaani wao
hawajui kupenda, wanachoangalia ni mwanaume ‘mwenye nazo’.
Wakishampata, watajifanyisha kuwa na mapenzi ya dhati kupita maelezo.
Maneno kama dear, honey, sweet na mengineyo matamu yatatawala midomoni
mwao lakini kumbe wizi mtupu.
Katika mazingira hayo sasa utaona ni kwa jinsi gani mapenzi yamekuwa
janga. Ndiyo maana leo hii wapo wanaotamani kutojihusisha na mambo ya
mapenzi kwa sababu hizihizi za usanii na ujanjaujanja mwingi.
Wakati mambo yakiwa hivyo, kuna baadhi ya watu ambao wamekithiri kwa
tabia ya kuwatesa wapenzi wao kisa wameoneshwa kuwa wanapendwa sana.
Naandika haya nikiwa na malalamiko ya wasomaji wangu wengi wakieleza
namna ambayo kupenda kwao kunawatokea puani.
Wapo watu ambao wakipenda wamependa kweli na hawawezi kujizuia
kuonesha hisia zao kwamba ‘wamekufa’. Hatua hiyo sasa hivi badala ya
kuwa changamoto kwa aliyependwa ili naye aongeze mapenzi, inakuwa
tatizo.
Uchunguzi unaonesha kuwa, sasa hivi mwanaume akioneshwa kupendwa sana
na mwanamke, atavimba kichwa na kumfanyia mwenzake kila aina ya visa
eti kwa kuwa amebaini amependwa na hawezi kuachwa.
Hili halipo kwa wanaume tu. Wapo wanawake ambao nao kwa kujua kuwa
waume zao wamekufa kwao, dharau inaongezeka, heshima inapungua na
kufanya hata yale ambayo wanajua yanawakera wenzao.
Hivi kwa nini tufikie hatua ya kuwatesa watu ambao wameshindwa
kujizuia kuonesha mapenzi yao kwetu? Kupendwa sana imekuwa nongwa
jamani? Hujui kwamba kupendwa ni bahati?
Mbaya zaidi mtu anakutamkia kwamba anakupenda sana na wewe unajibu kuwa nawe unampenda, kumbe hamna lolote.
Matokeo yake sasa kadiri siku zinavyokwenda, unaanza kuonesha
uhalisia kwamba humpendi kwa matendo. Hii siyo sawa. Mimi nadhani kama
humpendi mtu ni vyema ukamwambia mapema ili asikupe nafasi kwenye moyo
wake.
Unapokubali kuwa na wewe unampenda kisha baadaye unaanza kumtesa kwa
kumfanyia mambo ambayo hakuyatarajia, unafanya makosa na ni dhambi hata
kwa Mungu.
Kama kweli unapenda, mdhihirishie kwa matendo ili asiwe na shaka
kwamba huenda ameingia kwenye penzi la kisanii, lakini kama yeye
amekutamkia kuwa anakupenda lakini wewe ukahisi huna mapenzi naye, kuwa
muwazi kwake ili ajue wazi amempenda mtu ambaye hampendi!
Ni hayo tu kwa leo, tukutane tena wiki ijayo kwa mada nyingine.
Post a Comment