ad

ad

MABOSI wa Kamati ya Rufani ya Uchaguzi na ile ya Uchaguzi ya Shirikisho la Soka Tanzania (TFF) - wagoma kujiuzulu.

MABOSI wa Kamati ya Rufani ya Uchaguzi na ile ya Uchaguzi ya Shirikisho la Soka Tanzania (TFF), wamedai hawatojiuzulu kama baadhi ya wadau wanavyowashinikiza, kwani walitenda haki wakati wa mchakato wa uchaguzi mkuu wa shirikisho hilo ulioingia dosari.
Kamati hizo zinaongozwa na Idd Mtiginjola (Rufani ya Uchaguzi) na Deo Lyato (Uchaguzi).

Hivi karibuni, Shirikisho la Soka la Kimataifa (FIFA), lilituma ujumbe wake hapa nchini kushughulikia mtafaruku ulioibuka baada ya baadhi ya wagombea kukatwa na kamati hizo ambapo liliamuru mchakato huo uanze upya baada ya kugundua dosari kadhaa.
Kutokana na hali hiyo, wadau hao wamekuwa wakidai kamati hizo ndizo chanzo cha kuharibu mchakato huo na kusababisha uanze upya.

Wakizungumza kwa nyakati tofauti, wadau hao wakiwemo baadhi ya viongozi wa TFF, ambao hawakutaka majina yao kutajwa kwa madai kuwa wao ndio wahusika wakubwa kusimamia uchaguzi huo, walieleza kukerwa na maamuzi ya kamati hizo.
Kiongozi huyo wa TFF alisema hakuridhishwa na bado haridhishwi na uwepo wa Lyatto, kwa madai kuwa sio mwanasheria kama katiba inavyotaka mwenyekiti wa kamati hiyo kuwa na kudai kuwa ni vizuri akaachia ngazi na shirikisho likasaka mtu ambaye anakidhi vigezo hivyo.

“Mimi nashangaa sana kuona Lyatto sio mwanasheria na anaongoza kamati hiyo; ni ubabaishaji wa viongozi wetu wa juu hapa TFF, na pia haijaniingia akilini, eti wanamuondoa Jamal Malinzi kwa madai hana uzoefu wa miaka mitano katika soka, halafu wanamuacha Yusuph Manji ambaye hana hata mwaka mmoja, hii sio haki kabisa,” alisema mmoja wa wajumbe wa Kamati ya Utendaji ya TFF.
Akizungumzia tuhuma hizo, Lyatto alikiri kuwa yeye si mwanasheria na wala hatamani kuwa mwanasheria na kudai ni kazi ya waliomuweka kumuondoa, kwani alifanya maamuzi yake kama sheria na katiba inavyomruhusu.

Kwa upande wake, Mtiginjola alisema yeye anajiamini na anaiamini kamati yake na kudai kuwa hana mpango wa kujiuzulu, labda kama waliompa dhamana hiyo watamuondoa, lakini sio matakwa ya watu wachache, kwa kuwa alifanya maamuzi sahihi kutokana na katiba na kanuni zinavyomruhusu.

“Wao hawawezi kunitaka mimi kujiuzulu, kwani aliyeniweka ndiye ana mamlaka ya kuniondoa, kwanza mimi nina kazi zangu nyingi za kufanya na pia kamati yangu ina watu makini, ambao hawawezi kuendeshwa kimaamuzi na ndiyo maana hata nilikataa kufanya ‘Review’ kwa kuwa iko nje ya katiba, sheria na kanuni katika kamati yangu,” alisema Mtiginjola.
Powered by Blogger.