Azam yawakabili FAR Rabat leo.
TIMU ya soka ya Azam leo inaikaribisha FAR Rabat ya Morocco
katika mechi ya awali ya raundi ya pili ya Kombe la Shirikisho
itakayochezwa Uwanja wa Taifa, jijini Dar es Salaam.
FAR Rabat
Azam chini ya Kocha wake Stewart John Hall, leo itakuwa na kazi ya
kusaka ushindi kujiweka kwenye nafasi nzuri ya kusonga mbele kabla ya
mechi ya marudiano itakayochezwa wiki mbili zijazo mjini Rabat.
Hata hivyo, Azam wanapaswa kuwa makini zaidi dimbani kukabiliana na
wapinzani wao wenye uwezo na rekodi ya kufanya vema kwenye michuano ya
kimataifa.
Kati ya mafanikio ya timu hiyo iliyoanzishwa mwaka 1958, ni kutwaa
ubingwa wa Kombe la Shirikisho mwaka 2005 na kuwahi kubeba taji la Ligi
ya Mabingwa mwaka 1985.
Kwa kutambua umuhimu wa mechi ya leo, Shirikisho la Soka Tanzania
(TFF) limeitakia kila la kheri Azam katika mechi yake ambayo ni fursa
nzuri ya kutumia uenyeji kupata matokeo mazuri kabla ya kurudiana wiki
mbili zijazo.
Mazingira hayo yanaifanya mechi hiyo itakayochezeshwa na Emile Fred
kutoka Shelisheli kuwa ya ushindani mkubwa kwani wakati Azam ikipambana
kupata ushindi wa nyumbani, FAR Rabat, watakuwa wakipigana kupata
matokeo mazuri kabla ya mechi ya nyumbani.
Aidha kwa kutambua nafasi ya hamasa katika kupigania ushindi, TFF
imetoa wito
kwa wapenzi wa soka kujitokeza kwa wingi uwanjani kuishangilia timu
hiyo pekee kwa Tanzania iliyosalia kwenye michuano ya kimataifa.
Wakizungumzia mechi hiyo, makocha wasaidizi wa timu zote mbili,
Kalimangonga Ongala wa Azam na Lahcen Ouadani wa AS FAR Rabat, kila
mmoja amejigamba
kuwa timu zao ziko tayari kwa mechi hiyo inayotarajiwa kuwa na
ushindani mkubwa.
Ongala kwa upande wake, amesema wanawakabili FAR Rabat baada ya
kuwasoma kupitia DVD za mechi tatu za mwisho ikiwemo dhidi ya Al Nasir
ya Libya waliyokutana nayo kwenye raundi ya kwanza ya Kombe la
Shirikisho.
DVD nyingine mbili za FAR Rabat zilizofanyiwa kazi na benchi la
ufundi la Azam chini ya Hall, ni za Ligi Kuu ya Morocco na kusema
wamefanikiwa kutambua mbinu za wapinzani wao.
Naye Ouadani amesema licha ya kutoifahamu vizuri Azam, wanaijua vizuri
soka ya Tanzania hasa baada ya kuangalia mechi ya mchujo ya Kombe la
Dunia kati ya Taifa Stars dhidi ya Morocco iliyochezwa Machi 24, kwenye
Uwanja wa Taifa, jijini Dar es Salaam na Stars wakashinda 3-1.
Kwa upande mwingine, timu hizo zinakutana leo zikiwa nafasi ya pili
kwenye misimamo ya Ligi Kuu katika nchi zao kwani wakati Azam wakiwa
nafasi hiyo nyuma ya Yanga kutokana na pointi 43, FAR Rabat ya pili kwa
pointi 49 nyuma ya Raja Casablanca.
Aidha, wakati Azam wakitoka kuvuna ushindi wa 3-1 na sare ya 2-2 dhidi
ya Simba katika mechi zao mbili zilizopita, FAR Rabat wamevuna sare
mbili dhidi ya Raja Casablanca na Olympic Safi.
Wakati Azam wakianzia kampeni yao tangu raundi ya awali wakiwatoa
Al Nasr ya Sudan Kusini kwa jumla ya mabao 8-1 kisha kuwang’oa Barack
Young Controllers ya Liberia kwa mabao 2-1, FAR Rabat wameanzia raundi
ya kwanza.
Katika hatua hiyo, FAR Rabat walisonga mbele kwa ushindi wa jumla ya
mabao 2-1 dhidi ya Al Nasri ya Libya ambapo ilipocheza nyumbani, FAR
Rabat ilishinda bao 1-0 kabla ya kutoka sare ya bao 1-1 mjini Tripol.
Kwa upande wa Azam, kikosi kinaweza kuwa hivi: Aishi Manula, Mwadini
Ally, Khamis Mcha, John Bocco na Salum Abubakar waliomo pia kwenye
kikosi cha sasa cha Stars chini ya kocha wake Kim Poulsen.
FAR Rabat inaweza kuwa hivi: Younes Bellakhdar, Abderrahim Achchakir,
Younnes Hammal, na viungo Salaheddine Said, Salaheddine Aqqal na Youssef
Kaddioui.


Post a Comment