ad

ad

Wafuasi wa Ponda wafungwa mwaka mmoja

MAHAKAMA ya Hakimu Mkazi Kisutu Dar es Salaam, imewahukumu kwenda jela mwaka mmoja wafuasi 53 wa Katibu wa Jumuiya na Taasisi za Kiislamu, Sheikh Issa Ponda, waliokuwa wakikabiliwa na kesi ya kula njama na kufanya maandamano haramu.
Hukumu hiyo ilitolewa jana na Hakimu Mkazi, Sundi Fimbo, ambapo alianza kwa kuikumbusha mahakama kuwa mshtakiwa, Salum Bakari Makame, na wenzake 52, wanaotetewa na wakili wa kujitegemea Mohamed Tibanyendera walikuwa wakikabiliwa na makosa manne.

Makosa hayo ni ya kuandamana kwenda ofisi ya Mkurugenzi wa Mashtaka (DPP), Dk. Eliezer Feleshi, kumshinikiza ampatie dhamana Ponda kwa madai kuwa ndiye alikuwa ameifunga dhamana hiyo.

Fimbo alilitaja kosa la kwanza kuwa ni kula njama kutenda kosa kinyume na kifungu 384 cha Sheria ya Kanuni ya Adhabu ya mwaka 2002, kosa la pili ni la kufanya mkusanyiko haramu kinyume na kifungu cha 74 na 75 cha sheria hiyo ambavyo vinasomwa pamoja na kifungu cha 43(2)(4) na 46 cha Sheria ya Jeshi la Polisi ya mwaka 2002.
Kosa la tatu ni la kukaidi amri ya jeshi la polisi iliyowataka watawanyike ambalo ni kinyume na kifungu 79 cha Sheria ya Kanuni ya Adhabu kinachosomwa pamoja na kifungu cha 44 cha Sheria ya Jeshi la Polisi ya mwaka 2002.

Alisema kosa la nne ni la uchochezi ambalo lilikuwa likiwakabili washtakiwa watatu tu ambao ni Makame, Saidi Idd, Ally Nurdin Nandumbi, ambao wote hawa DPP, aliwafungia dhamana tangu walipofikishwa kwa mara ya kwanza mahakamani hapo Februali 18, mwaka huu.
Hakimu Fimbo alisema ili kuthibitisha kesi yao, upande wa jamhuri uliokuwa ukiwakilishwa na mawakili waandamizi wa serikali, Bernad Kongora, Peter Ndjike, Zuberi Mkakatu na Joseph Mahugo na Nassor Katuga walileta jumla ya mashahidi 10 na upande wa utetezi walileta jumla ya mashahidi 54.

Alisema mahakama yake kabla ya kutoa hukumu ilijiuliza maswali manne kuwa je washtakiwa walikula njama kutenda kosa? Walifanya mkusanyiko haramu? Walikaidi amri ya jeshi la polisi iliyowataka wasiandamane na je walifanya uchochezi?
“Baada ya kujiuliza maswali hayo mahakama hii imefikia uamuzi wa kuwaona washtakiwa 52 walitenda kosa la kula njama isipokuwa mshtakiwa wa 48 (Waziri Omar Toli) hakutenda kosa hilo kwa sababu alikutwa akitoka kununua mabeseni; mahakama hii imewatia hatiani kwa kosa hilo,” alisema.

Alisema kuwa kwa vielelezo hivyo, mahakama hiyo imeridhika kwamba walitenda kosa la kwanza, la pili na la tatu na kosa la nne ambalo ni la uchochezi mahakama imeona upande wa jamhuri umeshindwa kulithibitisha.
Akilichambua kosa la pili ambalo ni la kufanya mkusanyiko haramu, hakimu huyo alisema pia mahakama inamuachilia huru mshtakiwa wa 48, isipokuwa washtakiwa wengine wote wametiwa hatiani kwa kosa hilo.

Hakimu Fimbo alisema kila kosa alilowatia nalo hatiani watalitumikia kifungo gerezani kwa mwaka mmoja, hivyo washtakiwa hao watatumikia adhabu ya mwaka mmoja jela.
Kwa upande wake hakimu Fimbo alisema amezingatia maombi ya pande zote mbili na kwamba badala ya kuwahukumu kwenda jela miaka saba, anawahukumu kwenda gerezani mwaka mmoja na akasema yeyote ambaye hajaridhika na hukumu hiyo anaruhusiwa kwenda kukata rufaa mahakama ya juu.

Wakati huo huo mahakama hiyo, imesema kuwa Aprili 18, mwaka huu, itaoa hukumu ya kesi ya uchochezi na wizi wa malighafi za sh milioni 59 inayomkabili, Sheikh Ponda na wenzake.
Hakimu Mkazi Victoria Nongwa aliyasema hayo jana muda mfupi baada ya mashahidi watano wa upande wa utetezi waliopanda wote jana kizimbani kutoa utetezi na hivyo kufanya upande wa utetezi kuleta mashahidi 52.
Hakimu Nongwa alizitaka pande mbili katika kesi hiyo kuwasilisha kwa maandishi majumuisho ya mwisho ya kesi hiyo Aprili 3 na kwamba kesi hiyo itatajwa Aprili 4.
                                                   Habari na na Happiness Katabazi
Powered by Blogger.